Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Saba

Taji la Mfalme


Akiendelea kushangaa, alishtushwa na sauti ya vishindo, alipotazama mbele, aliona Jitu kubwa refu lipatalo futi hamsini na unene wake ni kama mibuyu miwili. Bwana Mako mwenye futi tano nukta nane, alionekana kiumbe mdogo ilhali Duniani alikotoka yeye ni miongoni mwa watu warefu. Basi kwa kuhofia, alikimbia akajificha nyuma ya mbao mojawapo ya ndege.

“Usijifiche,” jitu lilisema kwa upole, “nimekuona tangu unadondoka na chombo chako. Siwezi kukudhuru kiumbe mdogo.”

Bwana Mako alisogea karibu na Jitu akizungumza, lakini kwa sababu ya ule urefu wake, Jitu halikuweza kumsikia, hivyo lilimbeba likamweka juu ya bega lake mahali palipo karibu na sikio mazungumzo yakaendelea.

“Asante kwa msaada, hapa nipo wapi?” aliuliza Bwana Mako.

“Hapa ni Mailanda, nchi ya mfalme Solupa, katika bara la pili kati ya matatu yaliyopo katika sayari yetu isiyo na jina.” Jitu lilijibu. Bwana Mako akagundua kuwa, ndege yake ilimshusha katika sayari nyingine ya watu hao wakubwa.

Waliendelea kuzungumza, Bwana Mako alisimulia alivyotengeneza ndege yake na jinsi alivyosafiri, alisimulia yote bila kuacha kitu. Mwisho jitu liliahidi kumsaidia kurudi nyumbani, lakini lilimtaka limpeleke nyumbani kwake ili apumzike. Wakati wanaondoka, lilimuweka Bwana Mako katika mfuko wa shati, kisha likayabeba mabaki yote ya ndege kwa mkono mmoja na kuanza kutembea kuelekea uliko mji.

Jitu lilifika nyumbani kwake likiwa limemuweka Bwana Mako mfukoni. Mke wa Jitu pamoja na watoto wake wawili, walikaa sebuleni. Jitu lilipoingia tu, watoto walilikimbilia wakifurahi kurejea kwa baba yao. Hata hivyo, Jitu halikuwa na furaha kwa sababu siku hiyo halikurudi na chochote cha kulisha familia. Kumbe Jitu lilikuwa masikini!

Jitu lilisogea mpaka alipokaa mkewe, likamshika mkono wa utosi kuashiria kwamba halikufanikiwa kupata chochote. Mke wa Jitu asiye na maneno mengi, aliwaamuru watoto waingie vyumbani kulala kuisubiri kesho.

Bwana Mako aliyaona yote haya akichungulia kutoka mfukoni mwa shati alimokuwa. Nalo jitu lilikwenda mpaka katika kitanda kikubwa likakaa na kumtoa.

Bwana Mako asiye na hofu tena, aliliamuru Jitu limuweke sikioni apate kuliambia jambo.

“Rafiki mwema,” Bwana Mako alianza kusema, “nimeona wewe ni masikini, kiasi kwamba huna chochote cha kulisha wanao. Lakini rafiki, nakuahidi kukufanya tajiri mkubwa katika jamii yako.”

“Ha! Ha! Ha!” Jitu lilicheka, “kwa umbo lako, huwezi kufanya kazi yoyote wala jambo ukaondoa umasikini wangu, nadhani utakuwa umechanganyikiwa kwa sababu ya ile ajali kiumbe mdogo.”

“Ni nani huyo unayezungumza naye?” mke wa Jitu aliuliza, kumbe muda wote alikuwa akimtazama mumewe akiwa katika maongezi.

“Kabla sijakuambia, niitie watoto ili niwaeleze kwa pamoja habari za huyu kiumbe mdogo.”

Watoto walifika na Jitu lilisimulia namna lilivyompata Bwana Mako. Mwisho Bwana Mako alikwenda kulala na watoto. Walimbeba na kurushiana kwa zamu, isingekuwa uhodari wao wa kudaka, Bwana Mako angeanguka na kuvunjika mbavu.

Soma: Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya Nane

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Uhakiki wa Tamthiliya ya Kilio Chetu