Uhakiki wa Wimbo Baba wa Stamina Akimshirikisha Profesa Jay
Swali
Kwa
kutumia wimbo wa BABA ulioimbwa na Stamina akimshirikisha Profesa J, fanya
uhakiki wa muziki huo ukizingatia vipengele vya Fani na Maudhui huku ukionyesha
mifano ya maneno yaliyotumika katika wimbo kumdhalilisha mwanaume.
Jibu
Wimbo
Baba ulioimbwa na mwanamuziki Stamina akimshirikisha Profesa Jay na One Six,
ulitoka mwaka 2021 mwezi Januari. Mwezi uliofuata, mwezi Februari, marehemu na
aliyekuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Joseph Magufuli,
alitinga katika studio za TBC na kuomba apigiwe wimbo huo. Kitendo hicho
kiliufanya wimbo huo uzidi kupata umaarufu zaidi ya ulivyokuwa na pengine
kuwafikia watu wengi zaidi.
Baba
ni wimbo wenye majibizano ya pande mbili: mtoto na baba yake. Mtoto anamlaumu
baba kuwa, yeye ndiye sababu ya maisha ya mtoto kuwa mabaya. Baba naye
anazikataa lawama hizo kwa kusema kuwa maisha magumu anayopitia mtoto huyo
kayasababisha mtoto mwenyewe. Katika wimbo huu, tutachambua vipengele vya fani
na maudhui halafu tutaeleza mifano ya maneno yaliyotumika katika wimbo huu
ambayo yanamdharirisha mwanaume.
Wamitila
(2003) anaeleza fani kama dhana inayotumika kuelezea muundo. Maana hii inaweza
kukamilishwa kwa kusema kuwa, fani ni umbo la nje la kazi ya fasihi au mbinu
anazotumia mwandishi au msanii kufikisha maudhui.
Kwa
ujumla, fani ni mbinu anayoitumia mwandishi au msanii ili kufikisha ujumbe kwa
watu aliowakusudia/hadhira. Fani inabebwa na vipengele vingi kama: muundo,
mtindo, mandhari, wahusika na matumizi ya lugha.
Tunaanza
na uhakiki wa vipengele vya fani katika wimbo huu:
Wahusika
ni kipengele cha fani ambacho kimejitokeza katika wimbo. Wahusika waliojitokeza
katika wimbo huu ni:
-
Mtoto
ni mhusika ambaye anaanza kuzungumza katika wimbo. Anasikika akisema,
“Hivi
unajua nimekuvumilia Sana
Angekuwa
mtoto mwingine tayari ungeshampa laana…”
Maneno
hayo yanamdhalilisha baba, mtoto kumwambia baba yake kuwa nimekuvumilia sana ni
ukosefu wa nidhamu na adabu. Pia, kauli hiyo inalenga kueleza kwamba, Baba
amekuwa akifanya makosa mengi ambayo yanavumiliwa na mwanaye.
-
Mhusika
mwingine ni Mama. Mhusika huyu tunamfahamu pale anapodokezwa na mtoto,
“Mama
anasema mwanzo mimba ulikataa…”
Maneno
hapo juu yanamdhalilisha Baba kwa mara nyingine. Kumbe Baba alikataa mimba na
hili si jambo zuri.
-
Baba
ni mhusika anayeonekana katika wimbo huu. Baada ya kushambuliwa kwa maneno
makali ya mtoto wake, baba anasikika akijibu,
“Mwanangu
nimekusikia nakuombea kua uyaone,
Nilijua
umekuja kwangu kuniombea ili nipone,
Kumbe
umekuja kwa shari, kunilaumu na kunihukumu
Inaonyesha
ningesinzia ungeninywesha hata sumu…”
Maneno
haya yanamdhalili mwanaume. Mtoto anadhalilishwa kwa kuambiwa kwamba
angemnywesha sumu baba yake. Hii inaonyesha kuwa mtoto ni muuaji tena hafai.
Inaonyesha waziwazi kuwa, Baba hamwamini mtoto wake.
Kipengele
kingine cha fani kilichojitokeza ni mtindo. Wimbo huu upo katika mtindo wa
kisasa. Japo kuna vina, hakuna mizani inayoonekana na hii inapelekea kazi hii
ikae upande wa kazi zenye mtindo wa kisasa.
Kipengele
kingine cha fani ni mandhari. Yanaonekana mandhari ya nyumbani. Hapa ndipo
majibizano ya baba na mtoto yanafanyika. Mandhari haya ni nyumbani kwao mtoto.
Baba anasikika akilalamika,
“Mwanangu
nimekusikia nakuombea kua uyaone,
Nilijua
umekuja kwangu kuniombea ili nipone,
Kumbe
umekuja kwa shari, kunilaumu na kunihukumu…”
Haya
ni mandhari halisi yanayoeleweka kwa urahisi na kuifanya kazi hii iwe na
uhalisia kwa kuendana na jamii.
Kipengele
kingine cha fani ni matumizi ya lugha. Wimbo huu umetumia lugha rahisi
inayoeleweka vizuri. Baadhi ya vipengele vya matumizi ya lugha vinavyoonekana
ni pamoja na:
-
Matumizi
ya tafsida, msanii ametumia tafsida ‘kinga’ badala ya kondomu ili kupunguza
ukali wa maneno.
Mtoto
anamdhalilisha Baba yake kwa kiwango cha juu. Si tabia njema kwa mtoto
kumuuliza baba swali baya kama hili, “Halafu, hivi hauzijui kinga, au hukujua
peku peku kama italeta mimba…” mtoto amekosa adabu kwa kiwango kikubwa na hii
inamdhalilisha Baba.
-
Matumizi
ya nidaa, msanii anashangazwa na jambo pale anaposema, “Elimu siku hizi ni
bure, ila cha ajabu umeshindwa hata kunipeleka shule.”
Kauli
hiyo inamdhalilisha Baba. Inaonyesha kwamba, Baba hajielewi, pamoja na elimu
kuwa bure, lakini bado kashindwa kumpeleka mtoto wake shule.
-
Matumizi
ya msemo, “kua uyaone”, baba anamwambia mwanae msemo huo ili kujitetea kuwa,
pengine mtoto asidhani maisha ni kitu rahisi tu kama anavyofikiria.
Sambamba
na hayo, sasa tuangazie vipengele vya maudhui:
Dhamira
zimeonekana katika wimbo huu. Baadhi ya dhamira hizo ni:
-
Umuhimu
wa elimu. Kwa vyovyote vile matatizo haya yanasababishwa kwa sababu ya kukosa
elimu. Mzazi alijitahidi kumsomesha mtoto kama anavyolalamika, lakini mtoto
alikaidi shule.
Mzazi anasema, “Niliuza mali zangu
ilimradi wewe usome…”
-
hata hivyo mtoto analalamika kwa nini
hakupelekwa shule. jambo ambalo linaleta mkanganyiko juu ya ni upi hasa ukweli.
Mtoto
anasema, “Elimu siku hizi ni bure ila Cha ajabu umeshindwa hata kunipeleka
shule…”
Baba
alimpeleka mtoto shule kama anavyosema, au mtoto hakupelekwa shule kama
anavyolalamika? Hata hivyo, wote tunakubaliana kwa pamoja kuwa, mtoto hana
elimu.
Dhamira
nyingine ni malezi ya watoto. Mtoto anaonekana amelelewa vibaya na wazazi wake
ndiyo sababu anamtukana na kumdhalilisha baba yake bila aibu wala uonga. Hivyo
basi, wazazi wajitahidi katika malezi ya watoto wao kwani, samaki mkunje angali
mbichi na mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.
Ujumbe
unaopatikana katika wimbo huu ni, jamii ipewe elimu ya malezi ya watoto ili
kujenga taifa bora. Malezi ya watoto ndiyo kila kitu na endapo wana jamii
watayumba katika hili, basi matatizo makubwa yatatokea. Kwa mfano, katika jamii
yetu kipo kikundi cha watoto wadogo wafanyao vitendo vya uharifu maarufu kama
‘Panya road” watoto hawa ni matokeo ya malezi mabaya.
Migogoro
nayo imejitokeza katika wimbo huu. Tunaona mgogoro wa baba na mtoto. Mtoto anamlalamikia
baba yake kwa nini hakumpeleka shule, na baba anamkumbusha mtoto kwamba aliuza
vitu vyake ili amsomeshe. Mgogoro wao unasababishwa na ukosefu wa elimu pamoja
na umasikini uliokithiri ambao ndilo limekuwa tatizo kubwa kwa watanzania
wengi.
Tumeona
vipengele vya fani na maudhui, na ndani yake tumegusia baadhi ya maneno
yanayomdhalilisha mwanaume. Sasa tumalize kwa kuangalia maneno yaliyosalia
ambayo nayo yanamdhalilisha mwanaume:
“Usingemrubuni
mama labda angemuoa bakhresa…” ni maneno ambayo yanamdhalilisha mwanaume. Baba
anadhalilishwa kuwa pengine hakuwa na hadhi ya kuwa na mama yake mtoto.
“Au
ma-nurse walichanganya babangu haukuwa ni wewe…” maneno haya yanamdhalilisha
Baba kwa kuonyesha labda hakuwa na uwezo wa kuwa na mtoto kama yule na hapo tu,
amesingiziwa.
Mbona
mzee mushi namwona anahela
“Mzee
mwakalinga mwenzio anahela, Mzee luta sho ndio kabisa anamihela, Wewe ulikuwa
wapi mpaka unakufa kabwela…” Baba anadhalilishwa kwa umasikini wake, mbaya
zaidi anafananaishwa na wazee wenzake waliofanikiwa. Jambo hili linamuumiza
Baba ambaye hata hivyo ni mgonjwa.
Kwa
kuhitimisha, nyimbo nyingi za kizazi kipya zina mwelekeo wa mapenzi na
burudani. Baba ni miongoni mwa nyimbo chache ambazo hazina muelekeo wa mapenzi
na umejikita katika uhalisia wa mambo ya msingi yanayotokea katika jamii. Haina
maana kwamba mapenzi si kitu cha msingi, lakini hayapaswi kupewa kipaumbele
kikubwa kupita mambo mengine. Baba utaendelea kuwa wimbo mzuri wenye mafunzo
lukuki.
Marejeleo
Mwamanda,
J. (2008) Nadharia ya Fasihi Uchambuzi na
Uhakiki. JPD Company & General Supplies Ltd: Da es Salaam.
Stamina
na Professor Jay na One Six. (2021) Baba.
Inapatikana katika https://www.youtube.com/watch?v=_cim7dsia6Q.
Ilisikilizwa tarehe 21 Julai 2022.
Unahitaji Kufanyiwa Swali Lako? Wasiliana na Mwalimu kwa Kugusa Hapa