Uchopezi na Udhanilizi wa Kisemantiki Katika Kiswahili
Swali
Fafanua
kwa kutumia mifano madhubuti kutoka katika lugha ya kiswahili uchopezi na
udhanilizi wa kisemantiki.
Jibu
Uchopezi
na udhanilizi ni dhana zinazopatikana katika Semantiki. Dhana hizi
zinawakilisha mahusiano ya ukweli yanayochunguzwa na semantiki. Dhana hizi
zinafafanuliwa kwa kutumia mifano kutoka katika lugha ya Kiswahili.
Kwa
kuanza na dhana ya uchopezi inafafanuliwa
kwa kutumia mifano madhubuti kutoka katika lugha ya Kiswahili.
Uchopezi
ni uhusiano wa sentensi mbili ambapo ukweli wa sentensi ya pili hudhihirisha
ukweli wa sentensi ya kwanza (Crystal, 1998).
Kwa
mfano: Athuman amemuoa Aisha.
Aisha
ameolewa.
Sentensi
ya pili, inadhihirisha ukweli wa sentensi ya kwanza na hivyo kukubaliana na
maana iliyotolewa na mtaalamu Crystal.
Kwa
mujibu wa Lyons (1977), uchopezi ni uhusiano uliopo kati ya P na O ambapo P na
Q zinasimama kama vihusishi ambapo ukweli wa Q hujidhihirisha kutokana na
ukweli wa P. maana hii ya mtaalamu Lyons japo si rahisi kueleweka, lakini
inarejea kuwa, katika uchopezi sentensi ya pili hudhihirisha ukweli wa sentensi
ya kwanza.
Matinde
(2012) anadai kuwa uchopezi ni dhana inayotumiwa na wanaisimu amali kufafanua
uhusiano wa sentensi mbili au zaidi na hatimaye hufasiri maana za sentensi hizo
kutokana na mtiririko wa mantiki.
Kwa
ujumla, uchopezi ni dhana itumiwayo na wanaisimu maana katika kutoa ufafanuzi
juu ya uhusiano wa sentensi mbili au zaidi. Pia hufasiri maana za sentensi hizo
kutokana na mtiririko wa mantiki baina ya sentensi moja na nyingine.
Mahusiano
ya uchopezi baina ya sentensi ni ya kimaana. Hudaiwa kuwepo pasipo kuzihusisha
sentensi hizo na muktadha.
Katika
dhana hii, maana ya sentensi moja huweza kuhusishwa na sentensi nyingine pasipo
kurejelea muktadha.
Mifano:
A.
Mwanamuziki ameuawa na majambazi.
B.
Mwanamuziki amefariki.
A.
Daktari amemponya mgonjwa.
B.
Mgonjwa amepona.
Njia
ya kawida ya kueleza uhusiano baina ya a na b hapo juu ni kwamba, mtu huweza
kuchukulia kuwa a ni kweli kutokana na b yaani kama a ni kweli, basi hata b ni
kweli.
Kwa
mujibu wa sentensi a na b, tunaweza kusema kuwa, kwa sababu mwanamuziki
ameuawa, basi bila shaka amefariki. Vivyo hivyo kwa sentensi ya pili.
Pia, zifuatazo ni aina za uchopezi:
Uchopezi
wa kileksika. Huu ni uchopezi ambao lesksimu au maneno mawili au zaidi hurejea
maana moja au maana iliyokaribiana.
Mifano:
A.
viongozi wa Tanzania wanakula rushwa
B.
Mlungura ni halali kwa viongozi wa Tanzania.
Kwa
mtazamo wa uchopezi, a na b, zinachopezana.
Aina
nyingine ya uchopezi ni uchopezi wa kimuundo. Hii ni aina ya uchopezi ambao hudhihirishwa
na miundo ya sentensi mbili ambazo huwa na maana moja. Hii hujidhihirisha
katika sentensi zenye kauli tendi na kauli tendwa.
Mifano:
A.
Walimu wa shule ya msingi Kitero wamefaulisha wanafunzi wao.
B.
Wanafunzi wa shule ya msingi kitero wamefaulu.
Kwa
upande mwingine, udhanilizi
unafafanuliwa kama ifuatavyo:
Udhanilizi
ni dhana ya isimu amali ambayo hutokana na msemaji kudhani kuwa msikilizaji
waka ana ufahamu au taarifa ya awali kuhusu kile anachokisema (Matinde, 2012).
Kwa
mfano: Zengakona amefariki. Katika usemi huu msemaji anadhani kuwa msikilizaji
ana ufahamu wa awali kuhusu mtu aitwaye Zengakona. Pia, Zengakona alikuwa
mgonjwa.
Hudson
(2004) anadai kuwa udhanilizi ni kile kinachodhaniwa kuwa kina ukweli katika
sentensi kutokana na maelezo mengine.
Kwa
mfano: mtoto amepiga chafya tena.
Usemi
huu una udhanilizo kuwa mtoto alipiga chafya kabla hajapiga kwa mara nyingine.
Kwa
ujumla, udhanilizi ni kipengele kilicho katikati ya mpaka wa semantiki na
pragmatiki. Kimejadiliwa sana na wanasemantiki pamoja na wana pragmatiki. Hivyo
ni kitengo ambacho wataalamu wengi wanakiweka katika kitengo cha pragmatiki.
Mifano
ya udhanilizi:
A.
Umenunua gari jingine?
B.
Ulikuwa na gari kabla ya hili?
A.
Nyumba ya heri ni nzuri.
B.
Heri ana nyumba.
Kwa
hiyo sentensi a inadhaniliza sentensi b. Jambo linalodhanilizwa huchukuliwa
kuwa linafahamiwa na msemaji pamoja na msikilizaji. Katika sentensi a,
kuidhaniliza sentensi b, ina maanisha kwamba, ukweli wa sentensi a lazima
utokane na ukweli wa sentensi b.
Kwa mujibu wa Matinde (2012), udhanilizo una sifa kuu tatu ambazo ni:
Sifa
ya kwanza, udhanilizi haubadiliki hata pale sentensi msingi inapokanushwa. Kwa
mfano, sharifa ameingia darasani. Sentensi hii ikikanushwa inakuwa Sharifa
hajaingia darasani. Sentensi hii inabaki na udhanilizo uleule kuwa kuna
mwanafunzi anaitwa Sharifa.
Sifa
ya pili, udhanilizi haubadiliki hata pale sentensi msingi inapobadilishwa na
kuwa sentensi ulizi. Kwa kutumia mfano wa sentensi ya kwanza, sentensi itakuwa,
Sharifa ameingia darasani? Sentensi hii bado ina udhanilizo uleule kuwa Sharifa
ni mwanafunzi.
Sifa
ya tatu, udhanilizi unaweza kubadilika kutokana na uchopekaji, udondoshwaji na
upangaji wa vipashio katika sentensi ya msingi. Kwa mfano, Sharifa ameingia
darasani kufundisha kozi ya semantiki na pragmatiki. Sentensi hii ina kipashio
kipya ambacho ni, kufundisha kozi ya semantiki na pragmatiki. Kipashio hiki
kimebadilisha muundo wa sentensi na bila shaka udhanilizi wake na kuwa Sharifa
ni mwalimu wa kozi ya semantiki na pragmatiki.
Pia, zifuatazo ni aina za udhanilizi:
Udhanilizi
wa ukweli. Udhanilizi huu unatokana na matumizi ya maneno ambayo hubainisha
ukweli wa sentensi au tamko. Udhanilizi huu hubainishwa na matumizi ya vitenzi
kama vile: juta, gundua, tambua na furahi. Udhanilizi huu hujitokeza katika
mfano ufuatao:
Najuta
kuolewa na Juma. Tunapata udhanilizi kuwa, mwongeaji ni mwanamke, ameolewa,
Juma ni mumewe.
Aina
nyingine ya udhanilizi ni udhanilizi wa kileksika. Huu ni udhanilizi unaotokana
na muundo wa sentensi au kauli ya kwanza kusaidia kubashiri maana japo
haikusema bayana. Udhanilizi huu hutegemea matumizi ya baadhi ya maneno na
virai ambavyo ni mahsusi.
Kwa
mfano: “Jitihada zake zimemwezesha kung’oa kisiki kile.” Ufasiri wake ni kuwa
amefaulu kung’oa kisiki.
Pia,
udhanilizi wa kimuundo. Katika udhanilizi huu, baadhi ya miundo ya sentensi au
sehemu ya sentensi husika huchukuliwa kuwa na ukweli lakini sehemu ya pili
huuliza swali. Msemaji anaweza kutumia miundo hii kuibua ukweli wa taarifa
zinazotokana na sentensi.
Kwa
mfano: zainabu amepigwa na nani? Hapa tunapata udhanilizi kuwa, kuna mtu
anaitwa Zainabu, amepigwa lakini aliyempiga hajulikani.
Udhanilizi
kinzani ni aina nyingine ya udhanilizi. Huu ni udhanilizi wa kimuundo ambao
hubainisha ukinzani wa uongo na ukweli wa taarifa zilizomo kwenye usemi.
Udhanilizi huu haubainishi uongo tu bali pia kinyume cha matarajio. Ukinzani
hutokana na vishazi viwili vinavyokinzana katika usemi.
Kwa
mfano: Ungelikuwa mwalimu ungelifundisha vizuri. Maana yake ni kwamba, huyo
siyo mwalimu na hajui kufundisha vizuri).
Aina
ya mwisho ya udhanilizi ni udhanilizi usokweli. Huu ni udhanilizi ambao hauna
ukweli ndani yake.
Kwa
mfano: Juma ameota amefunda ndoa. Maana yake ni kwamba, ndoa haijafungwa,
lakini Juma alilala usingizi.
Kwa
ujumla, udhanilizo na uchopezo ni dhana mbili zinazotofautiana kimtazamo na
kimuundo katika sentensi. Uchopezi hutazama maana katika sentensi. Hivyo basi,
kwa kifupi, udhanilizo huja na dhana na fikra sahihi kwa msemaji au msikilizaji
kutokana na maelezo. Na uchopezi ni tukio la uhusiano wa sentensi au maana
kutegemea mtiririko wa mantiki. Ili kuwepo na uchopezi ni lazima kuwa na
sentensi mbili au zaidi zenye mahusiano ya kimantiki, ambapo ukweli wa sentensi
au usemi wa kwanza. Vivyo hivyo usikweli wa sentensi ya pili hujibainisha
katika sentensi ya kwanza.
Marejeleo
Leech,
G. (1981) Semantics. London: Penguin.
Makoba,
D. (2018) Semantiki na Pragmatiki ya
Kiswahili | KI 311: Inapatikana katika https://www.mwalimumakoba.co.tz/2018/04/semantiki-na- pragmatiki-ya-kiswahili- ki.html. Ilisomwa tarehe 25 Juni 2022.
Resani,
M. (2014) Semantiki na Pragmatiki ya
Kiswahili. Dar es Salaam: Karljamer
Print Technology.
TUKI.
(2010) Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Nairobi: Oxford University Press.
Unahitaji Kufanyiwa Swali Lako? Wasiliana na Mwalimu kwa Kugusa Hapa.