Maendeleo ya Kiswahili Kidato cha Tatu

Tawi la mti na kinyonga

Asili ya Kiswahili

Zipo nadharia nyingi zinazoelezea kuhusu asili ya Kiswahili. Wengine wakisema Kiswahili ni kiarabu, pijini, lugha ya vizalia na nadharia nyinginezo. Katika nadhari hizo, nadharia inayosema kuwa Kiswahili ni Kibantu, inaelekea kuwa kweli kwa sababu imejawa na ushahidi wa kuthibitisha madai yake.

Ushahidi wa kimsamiati unaothibitisha ubantu wa Kiswahili

Mizizi ya msingi ya misamiati ya lugha ya Kiswahili na zile za kibantu hufanana sana.

Mfano:

Kiswahili

Kikurya

Kinyiha

Kijita

Maji

Amanche

Aminzi

Amanji

Jicho

Iriso

Iryiso

Eliso

Ukitazama mifano hapo juu, utagundua kuwa, mizizi ya lugha za kibantu inafanana kwa kiasi kikubwa na ile ya lugha ya Kiswahili.

Ushahidi wa kimuundo unaothibitisha ubantu wa Kiswahili

Muundo wa lugha za Kibantu hufanana kwa kiasi kikubwa na ule wa lugha ya Kiswahili. Kwa mfano, namna viambishi vinavyopachikwa katika mzizi wa maneno hufuata kanuni ileile kama inavyotumika katika lugha ya Kiswahili yaani viambishi vinaweza kupachikwa kabla au baada ya mzizi.

Mifano:

Kiswahili             Kisukuma                       Kisimbiti                Kinyiha

A-na-lim-a             a-le-lem-a               a-ra-rem-a                      i-nku-lim-a

a-na-chek-a          A-le-sek-a               a-ra-sek-a               a-ku-sek-a

Kwa kuangalia mifano hii utagundua kwamba katika kutenganisha viambishi hufuata kanuni moja kwamba mahali kinapokaa kiambishi kwa mfano cha njeo, ndipo pia hukaa kwa upande wa lugha za kibantu, kwa mfano –na- na –ra- katika lugha ya kisimbiti. Hivyo tunaweza kusema kuwa kuna unasaba baina ya lugha hizi.

Jinsi miundo ya Kiswahili inavyofanana na miundo ya lugha nyingine za kibantu

Miundo ya sentensi za Kiswahili, inafanana na ile ya sentensi za kibantu. Miundo yote, ina sifa ya kuwa na kiima na kiarifu.

Kwa mfano:

Kiswahili – Juma/ anakula ugali

Kisukuma – Juma/ alelya bugali

Kukua na kuenea kwa Kiswahili nchini Tanzania katika enzi ya waarabu

Waarabu waliingia Tanganyika miaka mingi sana iliyopita. Inakadiliwa kwamba, walifika kabla ya karne ya 10. Biashara yao kubwa ilikuwa pembe za ndovu na kukamata watu ambao waliwauza kama watumwa. Ama kwa ufupi, waarabu walijihusisha na biashara mbalimbali. Pamoja na biashara hizo, waarabu walichangia kwa kiasi kikubwa sana kukua na kuenea kwa lugha ya Kiswahili.

Ukuaji wa Kiswahili kimsamiati nchini Tanzania katika enzi ya waarabu-mchango wa waarabu katika kukua na kuenea kwa kiswahili

Waarabu hasa katika pwani ya Afrika Mashariki walifanya biashara, ikiwamo biashara ya watumwa. Ilikuwapo misafara mbalimbali ya biashara kutoka pwani hadi bara. Katika misafara hiyo Kiswahili ndiyo iliyokuwa lugha ya mawasiliano hivyo Kiswahili kikaenea pia katika sehemu za bara. Kuna mambo kadhaa waliyofanya Waarabu ambayo yalichangia kukua kwa lugha ya Kiswahili. Waarabu walichangia kukua kwa lugha ya Kiswahili kama ifuatavyo:

1. Biashara

Waarabu walifanya biashara kati ya pwani na sehemu za bara, katika biashara yao walichangia uenezaji wa lugha ya Kiswahili. Lugha kuu ya mawasiliano na ya kibiashara iliyotumiwa na wafanyabiashara wa Kiarabu ilikuwa ni Kiswahili.

Kwa hiyo kwa njia hii waliweza kueneza Kiswahili kuanzia pwani hadi maeneo ya bara kama vile Morogoro, Dodoma, Tabora, Kigoma hadi Mashariki mwa Kongo.

2. Dini

Dini ilichangia ueneaji wa lugha ya Kiswahili kupitia mawaidha na mafunzo ya madrasa. Waarabu walipokuja walitaka kueneza dini ya Kiislamu katika maeneo waliyofikia. Hivyo, walianzisha madrasa ambayo walitumia kufundisha huku wakitumia lugha iliyokuwa ikitumiwa ambayo ni lugha ya Kiswahili.

3. Maandishi ya Kiarabu

Waarabu pia walileta hati zao zilizotumiwa katika maandishi ya lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo kupitia hati za Kiarabu maandishi mbalimbali ya lugha ya Kiswahili yaliweza kuhifadhiwa. Hivyo Kiswahili kilikua kutokana na kuhifadhiwa katika maandishi na kusomwa wakati wowote.

4. Kuoana

Vilevile Waarabu waliofika pwani waliweza kuoana na Wabantu. Hii ilisababisha kuzaliwa kwa watoto ambao walizungumza lugha ya kati kutoka kwa wazazi wao. Na kwa sababu hiyo watoto walichukua maneno mengi kutoka kwa baba na mama yao na hivyo kusababisha kuzungumza lugha ya Kiswahili.

Kukua na kuenea kwa Kiswahili nchini Tanzania katika enzi ya wajerumani

Wajerumani waliingia katika pwani ya Afrika Mashariki katika miaka ya 1875, walifanya kila jitihada kuwatawala Waafrika ambapo katika utawala wao walifanya biashara, waliendesha shughuli za kiutawala, za kidini na kielimu. Katika shughuli zote hizo Kiswahili kilitumika kama lugha ya mawasiliano.

Walipongia katika pwani ya Afrika Mashariki walikuta Kiswahili kimekwisha enea kwa kiasi kikubwa. Hivyo, walishindwa kutumia lugha yao ya Kijerumani, wakaamua kujikita katika lugha ya Kiswahili.

Wajerumani walikuza na kueneza lugha ya Kiswahili kupitia mambo haya:

1. Kutoa mafunzo ya lazima ya lugha ya Kiswahili kwa wafanyakazi wa serikali

Wajerumani waliweka sheria kwamba, lazima kila mfanyakazi wa serikali ajue lugha ya Kiswahili. Hivyo, wafanyakazi wote wa serikali ya kijerumani wakiwemo maakida, walijifunza lugha ya Kiswahili ili wapate kigezo cha kuajiriwa au kubaki na ajira zao. Hata Wajerumani wenyewe walilazimika kujifunza kiswahili ili waweze kuwasiliana na wenyeji kwa urahisi na hivyo kurahisisha shuguli zao za kiutawala.

2. Ujenzi wa shule

Shule zilifunguliwa kufundisha watu weusi ili waje wawe wasidizi wao katika utawala wa wajerumani, na lugha iliyokuwa ikitumika kufundisha masomo ilikuwa ni lugha ya Kiswahili.

3. Kuenea kwa utawala wa Wajerumani nchi nzima

Kwa kuwa utawala wa Wajerumani ulikuwa nchi nzima, basi kila ofisi palizungumzwa lugha ya Kiswahili na hii ilisaidia Kiswahili kuweza kukua na kuenea zaidi.

4. Shughuli za kilimo

Manamba au vibarua walilazimishwa wajue lugha ya Kiswahili. Waliporudi nyumbani, walisaidia kueneza lugha hii.

5. Mahakama

Wafanyakazi waliwahoji na kuandika hukumu kwa watuhumiwa kwa kutumia lugha ya Kiswahili. Hivyo Kiswahili kilikua na kuenea.

Hivyo ndivyo Wajerumani walivyosaidia kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili. Kumbe, pamoja na mabaya yote ya Wajerumani, walitenda baadhi ya mema. Waswahili walisema, pamoja na ubaya alionao fisi, hakosi mke.

Maswali

1. Kiswahili ni Kibantu kwa asili yake. Fafanua kwa kutumia ushahidi wa kimsamiati na kimuundo.

2. fafanua tofauti iliyopo kati ya pijini na krioli.

3. Asili ya Kiswahili ni Kiarabu. Eleza dai hili kwa kutumia kigezo cha msamiati.

4. Lugha ya Kiswahili ilikuwa inazungumzwa hata kabla ya ujio wa wageni. Thibitisha dai hili.

5. i. Utofauti wa kimatamshi, kimaumbo na matumizi ya maneno ya lugha kuu moja katika maeneo mbalimbali huitwa ___________

a. lafudhi b. lahaja c. rejista d. msimu e. toni

ii. Hamsini, laki, kasri na fikri ni miongoni mwa maneno yanayothibitisha kuwa Kiswahili ni________

a. kiarabu b. krioli c. kibantu d. pijini e. chotara

iii. Kiisimu, upi ni mtazamo sahihi kuhusu chimbuko la Kiswahili?

a. Ngozini b. Shungwaya kuu c. kiarabu d. pijini na krioli e. Pwani ya Afrika mashariki

iv. Lahaja ya Kishela inazungumzwa katika eneo lipi kati ya haya?

a. Tanga b. Kisiwa cha lamu c. Mombasa d. Unguja mjini e. Kisiwa cha pemba

v. Hoja za msingi zinazosema kuwa Kiswahili ni Kiarabu, zimeegemea katika___________

a. msamiati na dini ya Kiislamu b. msamiati c. msamiati wa waarabu kuoa waafrika d. dini ya kiislamu na biashara ya watumwa e. msamiati na lugha za Kibantu

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne