Dhana ya Uolezi Inavyojitokeza Katika Lugha ya Kiswahili
Swali
Fasili
dhana ya uolezi kisha ufafanue kwa ufasaha unavyokitokeza katika lugha ya
Kiswahili.
Jibu
Kwa
mujibu wa Resani (2014), Uolezi ni istilahi iliyoazimwa kutoka lugha ya
Kigiriki yenye maana ya kuashiria kwa kutumia lugha. Ni kipashio muhimu cha kipragmatiki
cha kuwakilisha lugha na miktadha ya kiusemi.
Akifafanua
zaidi kuhusu dhana ya uolezi, mwandishi anaeleza:
Katika isimu, uolezi ni dhana
inayotumiwa kurejelea hali ambayo, ili mtu aweze kuelewa maana ya maneno fulani
na virai fulani vilivyotumiwa katika tamko fulani, basi hana budi kuuelewa
muktadha ambamo msemaji na wasemeshwaji huwa. Maneno ambayo yana maana thabiti
ya kisemantiki, lakini vilevile yana maana halisi ambayo hudabilikabadilika
kutegemea wakati au mahali, basi yana sifa ya uolezi. (Resani, 2014:79)
Uolezi
ni uonyeshaji maalumu wa vitu, mahali, watu, hali au uelekeo katika muktadha
husika wa mazungumzo (Makoba, 2018).
Si
rahisi kwa mtu asiyeelewa muktadha husika kujua ni kitu gani kinarejelewa kwa
wakati huo. Mfano, ukija, yeye utamkuta pale. Maneno yaliyopigiwa msitari ni
violezi na siyo rahisi kwa mtu asiyeelewa muktadha husika kuelewa vitu
vilivyorejelewa na maneno hayo. Uelewekaji wa maneno hayo, unategemea muktadha.
Kiolezi
hurejelea neno au kiambo ambacho huhushisha semo na mahali, nafsi na hali. Urejeleo
wa kiuolezi hutegemea muktadha. Hivyo violezi ni maneno maalumu katika lugha
yatumikayo kuleta urejelezi wa kimuktadha. Uolezi ni dhana itumikayo katika
pragmatiki kuakisi uhusiano unaorejelewa katika muktadha wa msemaji na msikilizaji.
Kwa
ujumla, uolezi ni uashiriaji unaotumia lugha. Uashiriaji huu, hufanywa katika
mazungumzo na kwa yeyote asiyeelewa muktadha husika, itamuwia ngumu kuelewa
kitu kinachoerejelewa. Hivyo basi, uelewekaji wa maneno hayo unategemea
muktadha.
Ili
kuielewa zaidi dhana ya uolezi, tutazame aina zake na kupitia aina hizo,
itafafanuliwa kwa ufasaha namna uolezi unavyojitokeza katika lugha ya
Kiswahili.
Uolezi
nafsi, huu ni uolezi unaodhihirishwa katika usemi kwa kutumia viwakilishi
vinavyorejelea nafsi, kama vile: mimi,
yeye, yule, nyinyi, hawa.
Uolezi
nafsi unajitokeza katika lugha ya Kiswahili kwanza, hutumiwa na msemaji
anapojirejelea mwenyewe au anaporejelea msemeshwaji au mtu wa tatu katika
mawasiliano. Pili, katika Kiswahili maneno haya hutumika katika hali ya umoja
na wingi, na huhusiana na ngeli mahususi.
Uolezi
wakati, huu ni uhusiano wa maneno fulani yanayorejelea wakati katika muktadha
fulani. maneno hayo ni kama vile: sasa, leo, kesho, keshokutwa, baadaye,
mtondo, mtondogoo, jana, juzi, siku zijazo na maneno mengine mengi ambayo
hurejelea wakati.
Uolezi
wakati unajitokeza katika lugha ya Kiswahili kwa namna mbalimbali. tutumie
mfano wa wafanyabiashara wanaoogopa kukopwa, katika maduka yao hutundika ilani
inayosomeka, “Bwana mkopo amesafiri, atarudi kesho.” Hufanya hivi kwa kufahamu
kwamba kesho haiishi. Pia, watu wanapopanga ratiba mbalimbali kuhusu mambo kama
sherehe na mengineyo, hutumia uolezi wakati.
Uolezi
mahali, huu ni uolezi ambao unahusu mahali pa kitu kwa kuwiana na mahali pa
tamko. Uolezi huu unaweza kuhusu mahali pa msemaji na msemeshwaji, au mahali pa
watu au vitu vinavyorejelewa katika tamko.
Katika
lugha ya Kiswahili, uolezi mahali upo wa
aina tatu:
Viashiria
vya uolezi wa mahali pa karibu kabisa na msemaji. Kwa mfano, maneno kama hapa,
huku na humu.
Viashiria
vya uolezi wa mahali pa karibu kidogo na msemaji. Kwa mfano maneno kama, hapo,
huko na humo na,
Viashiria
vya uolezi wa mahali pa mbali na msemaji. Kwa mfano, maneno kama: pale, kule na
mle.
Uolezi
wa mahali unajitokeza katika lugha ya Kiswahili kwani kwa kawaida inaeleweka
kuwa, maneno yanayoashiria uolezi mahali yanahusishwa na mahali alipo msemaji.
Kwa mfano, katika utungo, “Duka la Mangi liko mtaa wa pili.” Kirai mtaa wa pili
humaanisha mtaa wa pili kutoka hapa nilipo sasa.
Uolezi
jamii ni aina nyingine ya uolezi. Uolezi jamii hurejelea taarifa za kijamii
ambazo hutumiwa katika viyambo. Maana ya tungo hutegemea uhusiano wa kijamii
uliopo baina ya msemaji na msemeshwaji. Maneno hupata maana kamili yanapotumiwa
kuhusiana na wahusika fulani.
Uolezi
jamii unajitokeza katika lugha ya Kiswahili kwa namna mbalimbali kwa mfano, mtu
anapokuwa anamtambulisha mke wake anaweza sema, “Huyu ni mke wangu mpenzi.”
Lakini anapomtambulisha mke kwa kusema huyu ni Mariam, inapunguza ladha fulani.
Uolezi
mwingine ni uolezi matini. Huu ni uolezi ambao unaonyesha urejelezi ulio ndani
ya makala. Makala hiyo inaweza kuwa ya kuandikwa au kusemwa. Kwa jina jingine,
makala ya kusemwa inaitwa kilongo. Kwa mfano, tunaweza kurejelea kwa kusema,
‘hii ni hadithi ya Sungura na Fisi.’ Katika usemi huu, neno hii hurejelea
sehemu ya kilongo itakayofuatia.
Uolezi
matini unajitokeza kila siku katika lugha ya Kiswahili maneno ya kuongeza kama,
zaidi ya hayo, kwa kuongezea, mintarafu ya hayo huonekana katika lugha. Pia
maneno ya kusababisha kama, kwa sababu, kutokana na na kwa hivyo. Mengine ni viwakati, mfano,
baadaye, kwanza, baada ya muda, baada ya saa moja na virejeleo vya matukio,
mfano, Maimuna anamjua yeye, hivi vyote vinajitokeza katika lugha ya Kiswahili.
Pia,
uolezi mwelekeo nao ni aina ya uolezi ambao utatusaidia kuona namna uolezi
unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili. Huu unahusu nafasi ya kitu kimoja
kimwelekeo kikilinganishwa na nafasi ya kitu kingine. Uolezi mwelekeo ni pamoja
na juu na chini. Maneno kama: magharibi, mashariki, kaskazini na kusini.
Hivyo
basi maneno kama Afrika Mashariki, Tanzania kanda ya Magharibi, Nyanda za juu
kusini, ni mifano inayodhihirisha wazi namna ambavyo uolezi unajitokeza katika
lugha ya Kiswahili.
Hivyo
basi, dhana ya uolezi ni dhana ambayo inaeleweka kwa urahisi na inajitokeza
katika lugha ya Kiswahili. Kupita aina za uolezi, tumeweza kuona namna uolezi
unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili, kumbe, ni vigumu sana kuuona uolezi
unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili bila kutazama aina zake. Tunaweza
kusema kuwa, uolezi katika lugha ya Kiswahili unajitokeza katika matini, jamii,
mahali, wakati na nafsi.
Marejeleo
Leech,
G. (1981) Semantics. London: Penguin.
Makoba,
D. (2018) Semantiki na Pragmatiki ya
Kiswahili | KI 311: Inapatikana katika https://www.mwalimumakoba.co.tz/2018/04/semantiki-na-pragmatiki-ya-kiswahili-ki.html.
Ilisomwa tarehe 31 Mei 2022.
Resani,
M. (2014) Semantiki na Pragmatiki ya
Kiswahili. Dar es Salaam: Karljamer Print Technology.