Tofauti ya Semantiki, Pragmatiki na Semiotiki

Mchoro wa ua

Swali

Semantiki, pragmatiki na semiotiki ni taaluma zinazojishughulisha na maana. Huku ukitoa mifano dhahiri, eleza kwa ufasaha kiini cha tofauti baina ya taaluma hizo.

Jibu

Wataalamu wengi wametoa maana ya Semantiki. King’ei (2010), Semantiki, ni taaluma ya isimu inayofafanua maana katika lugha.

TUKI (2004), Semantiki, ni tawi la isimu ambalo hujishughulisha na uchambuzi wa lugha katika kiwango cha maana.

Katika mtazamo huu, Semantiki ni utanzu wa isimu unaochunguza maana katika lugha ya mwanadamu ukitafiti maana za fonimu, mofumu na maneno na tungo.

Nayo Pragmatiki imetolewa maana na wataalamu wengi, Leech (1981), anasema semantiki inaangalia  maana ya matamshi, maumbo na Miundo katika lugha. Anaendelea kusema  Maana ni sehemu ya umilisi na ufahamu wa lugha, kujifunza Lugha ni kukubaliana na maana za vipengele vyote vilivyopo katika lugha.

Richmond (2012), anasema kwamba ni tawi la Lugha linalojihusisha na matumizi ya lugha kwa kuzingatia Muktadha wa wazungumzaji husika. Hivyo Thomason anadai kuwa pragmantiki inahusu zaidi mambo mawili: Matumizi na Muktadha.

Kwa ujumla, pragmatiki ni taaluma ya semiotiki ambayo huchunguza ishara na maana zake ndani ya muktadha wa jamii husika, ni utanzu wa isimu unaochunguza maana ya lugha ya binadamu katika miktadha yote inayomzunguka.

Semiotiki imefasiliwa na wataalamu mbalimbali, na hizi ni maana zilizotolewa na baadhi ya wataalamu hao. Kwa kuanza na mtaalamu Massamba (2004), yeye anasema kuwa, semiotiki ni taaluma ya kisayansi inayojishughulisha na uchunguzi na uchanganuzi wa mifumo ya ishara mbalimbali ikiwa inazingatia zaidi uhusiano baina ya kiwakilishi na kitajwa.

Pia mtaalamu Ferdinand de Saussure kama alivyonukuliwa na Morris (1971) amefasili semiotiki ni uhusiano kati ya alama na kitu, jambo au hali ya kitu inavyowakilishwa, akaendelea alama ni kiashiria na kitu ni kiashiriwa. Hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya kiashiria na kiashiriwa.

Kwa ujumla, semiotiki ni taaluma inayojishughulisha na uchunguzi wa ishara na alama pamoja na uhusiano kati ya alama na kitu husika.

Zifuatazo ni tofauti kati ya Semantiki na Pragmatiki:

Semantiki hueleza maana kwa kuzingatia misingi ya lugha yenyewe lakini pragmatiki hueleza maana kulingana na mahusiano ya kiusemezano yanayokuwepo kati ya msemaji na msemeshwaji. Katika pragmatiki maana hutolewa huku ikihusishwa au kutegemeana na mzungumzaji wa lugha, hii inamaana kuwa katika pragmatiki, maana ya neno au tungo inategemea nini mzungumzaji anakusudia kusema. Mfano, mtu anaweza kusema leo niko ovyo akiwa na maana ya kwamba hana hela WAKATI  katika semantiki, maana hutolewa ikiwa safi na hutolewa kama jinsi inavyopaswa kuwa kutoka katika lugha husika, na maana hiyo ndiyo huchukuliwa kama ndiyo njia ya mawasiliano.Mfano, mtu ana kuwa wazi tu kusema kuwa leo sina hela.

Semantiki huichukulia lugha kuwa ni mfumo dhahania wa alama lakini pragmatiki huichukulia lugha kuwa ni kifaa cha mawasiliano kinachoweza kutumiwa kadri ya matakwa ya msemaji.

Semantiki huelezea maana ya msingi tu lakini pragmatiki hueleza maana inayokusudiwa na msemaji na ile inayoeleweka kwa msemeshwaji. Neno katika semantiki ndilo hubeba maana ya msingi na hulenga maana halisi ya neno kama jinsi ambavyo wazungumzaji wa lugha hiyo walivyolizoea toka enzi na enzi. Maana hii ya msingi huwa haibadiliki katika jamii zote zinazotumia neno hilo. Mfano, neno “baba” huwa na maana moja tu ya msingi ambayo ni mzazi wa kiume wakati katika pragmatiki, hali hiyo ni tofauti, ambapo neno hutazamwa katika mtazamo wa kidhima huku likihusishwa na muktadha ambapo neno hilo limetumika.Mfano, neno “mtoto” hubadilika kulinga na muktadha ambapo kwa muktadha mwingine hutumika kama mpenzi Hii ni kwa mujibu wa Carston (1998) na Louise McNally.

Semantiki na pragmatiki ni mapacha wawili wanafanana na kutofautiana kwa kuwa kilengwa chao ni kimoja. Kwa hiyo, mtumiaji wa lugha anapaswa kuzifahamu zote mbili kwa kuwa ni vigumu kupata maana katika semantiki tu, bali maana nyingine huhitaji kuhusishwa na muktadha husika.

Tofauti nyingine ni, Maana ya kipragmatiki kwa kiasi kikubwa huathiriwa na nia au kusudio au saikolojia ya mzungumzaji na siyo kama jinsi ambavyo sentensi inavyomaanisha.Mfano, mtu anaweza kutumia neno ambapo akawa na lengo la kuficha uma isijue nini kinaendelea kwani anaweza kusema umekiona wapi kitabu changu leo wakati huo akiwa na maana ya mpenzi wake WAKATI katika semantiki, kusudio na nia ya mzungumzaji ni sharti ikubaliane na kanuni za lugha husika, ikiwa ni pamoja na kufuata taratibu za muundo wa sentensi yaani mpangilio wa viambajengo katika sentensi.Mfano, mtu ana kuwa huru kuongea kile ambacho anakimaanisha yaani kama ni kitabu basi anakuwa anamaanisha kitabu kweli na sio vinginevyo  (Carston, 1998).

Katika semantiki viwango vinavyochunguzwa ni pamoja na fonimumofumanenovirai na sentensi lakini Pragmatiki huchunguza zaidi namna lugha ianvyotumika katika muktadha mbalimbali. Mfano, muktadha wa buchani mtu anaweza kusema mimi utumbo na akaeleweka vizuri kabisa.

Semantiki imegawanyika katika matawi mawili yaani semantiki ya kileksika ambayo hujihusisha na maana za maneno na mahusiano ya maana katika sentensi na tawi la pili ni semantiki ya virai au sentensi ambayo hujihusisha na maana za maneno katika kiwango cha kisintaksia WAKATI HUO Pragmatiki hujidhihirisha katika mazingira mawili yaani maana inayopatikana katika mazingira ya kiisimu. Mfano, kuna baadhi ya maneno hayawezi kupata maana mpaka yatumike na maneno mengine katika sentensi, maneno hayo kama vile na, juu ya kwa. Mfano, amekuja kwa basi. Sura ya pili ni maana inayopatikana katika matumizi yake katika muktadha fulani katika ulimwengu wa watumia lugha .Mfano, maana za maneno zitakazotumika katika muktadha wa stendi, mfano mtu anaweza kusema nitafutie vichwa vitatu na akaeleweka vizuri katika muktadha huo.

Kwa upande wa semiotiki, tunasema kuwa:

Alama zinazoshughulikiwa huwa katika maumbo mbalimbali. Zinaweza kuwa katika umbo la maneno, picha, sauti, harufu, ladha, vitendo au vitu.

Maana katika semantiki huangalia pia maneno kihistoria na kisasa yaani etimolojia.

Pia, semiotiki ni kama bwawa ambamo semantiki huchota baadhi ya alama na kuzitumia katika mfumo wa lugha. Semantiki ni taaluma ndogo ndani ya taaluma kubwa ya semiotiki.

Lakini ieleweke kwamba, alama zinazotumiwa katika lugha hazina uhusiano wa moja kwa moja kati yake na maana inayohusishwa na alama hizo yaani lugha ni mfumo wa sauti za kinasibu, si usababishi au ufanano.

Hivyo basi Semantiki inatofautiana na semiotiki kwani semantiki inashughulikia alama za lugha yaani kila lugha huwa na alama zinazoashiria kitu fulani wakati alama za semiotiki hazihusu lugha yaani huwa ni maana za mawasiliano, mfano ishara za mawingu, wanyama kama bundi ishara ya uchawi.

Kwa kuhitimisha: Semantiki, semiotiki na pragmatiki, zinatumika sana katika na watumiaji wa lugha katika ulimwengu na ni vigumu kuzitofautisha kwani hujikita kuchunguza maana za maneno katika muktadha tofauti tofauti kama sehemu ya mfumo wa mazungumzo sambamba na kufafanua mfumo fungamanifu wa mazungumzo katika lugha. Hata hivyo, kuzisoma taaluma hizi kutaondoa ugumu huo.

Marejeo

Alghamdi, R (2013)Similarities and Differences between Semantics and Pragmatics.

Carston,R (1998) The Semantics/Pragmatics Distinction: a view from relevance theory. Katika UCL Working Papers in Linguistics.

Geoffrey Finch (2012), Linguistic; Terms and Concepts. Palgrave. Macmillan publishers.

Massamba P. B. D (2004) Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha. Dar es Salaam: TUKI.

Morris, Charles W. (1971), Writings on the general theory of signs, The Hague: Mouton.

Peirce, Charles S (1934), Collected papers: Volume V. Pragmatism and pragmaticism. Cambridge, MA, USA: Harvard University Press.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Vichekesho vya Kuchekesha na Kuvunja Mbavu 1