Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta | Sehemu ya Sita

Mwanamume gizani
Siku zote nilikuwa naishia nje nimtafutapo Asi pembezoni mwa nyumba aliyokuwa akiishi. Sasa niliamua, niingie mpaka ndani, huenda Babuu alimkataza kutoka.

Nilifika katika nyumba ile, nikagonga mlango kwa dakika nyingi bila kufunguliwa. Mlango ule ulikuwa mkubwa tena wenye pande mbili zilizokutana katikati ambako palikuwa na kitasa. Baada ya gongagonga bila majibu, nilijaribu kuzungusha kitasa, hapo nikagundua palifungwa. Sikuelewa kama mwenye nyumba alikuwa ndani au alitoka, hayo ndiyo matatizo ya vitasa!

Hata hivyo nilihisi wenye nyumba hawakuwepo. Niliamua kupeleleza kidogo kuhusu nyumba ile na wakazi wake, kwa kuwa sikutaka kujulikana kama nilikuwa ninapeleleza, niliamua kutafuta watoto wadogo, hawa wasingeweza kunitilia shaka lolote.

Niliingia katika chumba kimoja cha biashara kilichokuwa kimeandikwa ‘play station’. Ndani yake mlikuwa na watoto waliokuwa wanacheza michezo mbalimbali ya kompyuta. Nami nilikwenda moja kwa moja mpaka katika sehemu moja iliyokuwa wazi, nikaomba niwekewe GTA, haraka nikawekewa na nikaanza kucheza.

Haikuchukua hata dakika moja, watoto watano walikuwa nyuma ya mgongo wangu wakitazama jinsi nilivyokimbizana na maaskari katika mchezo ule wa GTA.

“Nani anaweza kunisaidia kuwakimbia hawa askari?” niliuliza.

“Mimiiiiii!” watoto wote walijibu. “Wewe unaonekana unajua sana, kaa hapa uendelee, halafu nyinyi wengine, mtakuwa mkipeana naye zamu, nitalipia hela ya siku nzima leo mcheze tu mpaka mfike mwisho. Halafu wewe rafiki yangu, hebu njoo hapa nje mara moja nataka nikutume kitu,” nilisema nikimshika mkono mtoto mmoja, makadirio miaka tisa, ambaye alionekana mjanja zaidi ya wengine.

Nilikaa katika kiti nje ya chumba kile cha michezo. Niliyekaa naye tayari nilishamfahamu jina lake, aliitwa Iki.

“Iki, ile nyumba nani anakaa?” niliuliza nikinyooshea kidole nyumba ambayo nilimuona Asi akiishi.

“Anayeishi hapo ni mgeni,” alijibu Iki akichungulia wenzake walivyokuwa wakiifaidi GTA.

“Iki tukimaliza mazungumzo, nitakulipia sehemu ya peke yako ucheze bila kupeana zamu na mtu. Haya endelea, anayeishi hapo ni mgeni, eheee…”

“Kahamia juzi juzi tu.”

“Aliyekuwa anaishi hapo mwanzo ni nani?”

“Bibi Martina, sasa watu walisema yeye ni mchawi kwa hiyo akaamua kuhamia Mbeya kwa mtoto wake Boni.”

“Sasa Iki hiyo nyumba anaishi mtu mmoja tu?”

“Hapana, Dada Asi anaishi naye, huwa anakaa pale nje na anapenda sana kuongea na watu, kuna siku alikuja humu akaomba tumfundishe kucheza gemu. Alisema yeye hela siyo tatizo, kuna kaka yake huwa anapita na humpatia shilingi elfu moja kila siku.”

Nilitabasamu niliposikia jibu hili. Nilitambua wazi kuwa, zile elfu moja ni zile ambazo nimekuwa nikimpa kila nilipopita. Kumbe alizitumia kujifunza kucheza gemu kama alivyosema Iki. Iki hakunyamaza, raha ya watoto wadogo hawana hofu na wakifunguka hufunguka kwa kusema yote wayajuayo. “Ila kuna siku…” alidokeza halafu akanitazama usoni, akaona kunitazama haifai, akainamisha kichwa chake chini. “Kuna siku mama alisema mle ndani kuna wasichana wengi tu!”

“Kuna kingine alisema baada ya hapo?” niliuliza nikitazama pembeni ili Iki asiniogope.

“Hapana, hata yeye hajui sana.”

Niliridhishwa na majibu ya Iki. Nikamuita kijana aliyeshughulika na ofisi ile, nikampatia kiasi cha fedha nikimsisitiza Iki aachwe acheze ‘game’ peke yake bila bughudha, wale wengine niliowaacha wakipeana zamu, niliongeza malipo yao pia.

Taarifa za Iki kuwa mle ndani kulikuwa na wasichana wengi zaidi zilinishtua. Nilipanga usiku wa siku hiyo, lazima ningeingia ndani ya ile nyumba ili nifanye uchunguzi wa mambo mawili matatu.

Soma: Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta |Sehemu ya Saba

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne