Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta | Sehemu ya Saba

Usiku wa manane
Saa nane usiku nilikuwa nje ya mlango wa nyumba. Nilivalia sweta jeusi, suruali nyeusi na viatu vyeusi hata nikawa sehemu ya giza. Nilifungua kitasa kwa funguo yangu bandia isiyoshindwa kufungua milango mingi. Mlango ukatii kwa kufunguka taratibu.

Niliiingia na kuufunga mlango taratibu, kisha nikaanza kutembea kwa tahadhari kubwa. Sikutaka kuwasha taa, kwanza sikufahamu vilipokaa viwashio, nikatumia tochi yangu. Ilikuwa nyumba ya vyumba sita. Katikati korido, pembeni kushoto vyumba vitatu na pembeni kulia vyumba vitatu.

Nikiwa nasogea, nilikwaruzwa na kitu mguuni, nikazima tochi haraka halafu nikaganda kama sanamu, mkono ukiwa kiunoni nilipoipachika Beretta.  Baada ya sekunde tatu, nikawasha tochi, nikaishia kumuona paka mkubwa, silaha ikarudi kiunoni, sikuwa pale kupambana na nyau!

Vyumba vitano havikufungwa, nilivichunguza vyote, nikaona dalili za watu kulala humo kwa kurundikana. Niliona magodoro chakavu yaliyopangwa kivivu, ndoo nne za kuogea kwa kila chumba na vipande vya sabuni.

Baada ya kumalizana na vile vyumba vitano, sasa nikakiendea kile chumba cha sita kilichokuwa kimefungwa. Nilitumia funguo yangu, mlango ukafunguka. Tofauti na vile vyumba vingine vilivyokuwa na magodoro machafu na mrundikano wa taka, hiki kilikuwa kizuri, tena kuna kitanda kikubwa na chini pamesakafiwa kwa vigae vya kuteleza. Hata wewe tayari umegundua kwamba, hiki ni chumba alichoishi Babuu.

Nilikichunguza lakini sikupata chochote cha maana. Zaidi niliiishia kuona misokoto miwili ya bangi iliyokuwa imefichwa ndani ya mto wa kulalia. Nilipangilia kila kitu vyema kisha nikaondoka kurejea katika makazi yangu.

Soma: Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta |Sehemu ya Nane


Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Sifa Bainifu za Irabu ya Kiswahili Sanifu