Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta | Sehemu ya Kwanza
Nilipita siku ya Jumatatu huko Mwananyamala katika nyumba za ndani sana. Baada ya kuvuka mitaro mitatu, nikaona nyumba iliyokuwa na baraza kubwa. Hapo barazani alikaa binti mrembo sana ambaye kwa uzuri wake angetosha kushtua, kuchanganya na kupunguza ufanisi wa akili ya mwanamume yeyote. Binti huyu aliyekuwa na sura iliyochongeka kwa mfano wa umbo la yai, alivalia dela lililoficha umbo lake.
Nilitembea hata nikawa mkabala na mahali alipokaa,
nikaporomosha salamu huku nikipunga mkono, “Habari.”
“Nzuri,” msichana alijibu akibadili mkao, nami
nikaendelea na hamsini zangu.
Nilipita siku ya Jumanne huko Mwananyamala katika nyumba
za ndani sana. Baada ya kuvuka mitaro mitatu, nikaona nyumba iliyokuwa na
baraza kubwa. Kama jana, binti yule alikaa, nami nikaporomosha salamu,
“Habari.”
“Nzuri,” msichana alijibu akibadili mkao, nami
nikaendelea na hamsini zangu. Lakini wakati nikitembea, nilisikia vishindo
vikija. Nilipogeuka, niligongana uso kwa uso na msichana niliyemsabahi.
“Kaka…” aliita akitazama chini kwa aibu. “Naomba nisaidie
elfu moja.”
Sikufikiria mara mbili, nilitoa mfukoni noti moja ya
shilingi elfu moja nikampa. Kisha nikatoa kikaratasi na kalamu, nikaandika
1,000/=.
Nilipita tena siku ya Jumatano eneo hilohilo. Baada ya
salamu, binti alinifuata akaniomba elfu moja, nikampa kisha nikaandika katika
kikaratasi changu.
Nilipita kwa mara nyingine eneo lile siku ya Alhamisi.
Binti akaomba elfu moja. Nikampatia kisha kama kawaida nikaandika katika
kikaratasi. Sasa hesabu jumla ilisomeka shilingi za Kitanzania elfu tatu.
Basi nilivutiwa na upitaji wa njia ile, Ijumaa nayo
nikapita. Kama kawaida binti akaniomba elfu moja, nikampa kisha nikaandika
kwenye kikaratasi changu. Wakati nataka kuendelea na hamsini zangu, alinidaka
mkono akaniomba tukae kibarazani kwa muda.
“Huwa unaandika vitu gani ukinipa hela zako?” msichana
aliuliza akinitazama bila aibu, huenda alikwisha nizoea.
“Huwa naandika hela ninazokupa. Sasa zimefika shilingi
elfu nne,” nilijibu nikitabasamu.
Binti aliangua kicheko, kisha akasema, “Mwanaume bahiri
wewe, sijawahi kuona… jina lako nani wewe?”
“Naitwa Mako.”
“Oooh… kumbe!”
“Unafanya kazi gani bwana wewe?”
“Sisi wengine kazi zetu huwa hazitajwi,” nilijibu kisha
msichana akacheka tena.
“Ukipita hapa huwa unakwenda wapi?”
“Huwa nakwenda maeneo tofauti, leo nakwenda Kibo Peak
kutuliza kichwa.”
“Oooh, nikipata nafasi ya kutoroka nitakuja… Usiondoke
mapema,” kabla hajaendelea, vilisikika vishindo vikija kutokea ndani.
“Babuu anakuja, kimbia haraka asikuone,” alinisisitiza,
nami nikakimbia kwa kasi kumshinda mwanariadha Usain Bolt. Njiani niliwaza
mambo mawili: Babuu ni nani? Na huyu msichana niliyeongea naye jina lake nani?
Nilipata kona nzuri nikajificha, nikatazama ili nimuone huyo Babuu, hakuwa mzee
kama lilivyo jina lake, alikuwa kijana au mwanamume wa makamo makadirio miaka
arobaini mwisho hamsini. Alivaa mavazi chakavu, juu kichwa kipara na chini
alikuwa na kandambili. Sikutaka kuchunguza sana, nikaondoka.
Soma: Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta | Sehemu ya Pili