Uradidi Unavyojitokeza Katika Lugha ya Kiswahili

Ndege Pacha


Swali:

Onesha kwa mifano ya kutosha onesha namna uradidi unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili.

Ili kutimiza mahitaji ya kila siku ya wanadamu, wanahitaji kuwasiliana, hata hivyo ipo changamoto ya msamiati. Changamoto hiyo ni kukosekana kwa msamiati unaohitajika ili kutaja kila dhana. Kutokana na upungufu wa msamiati unaohitajika kutaja kila dhana, watumiaji wa lugha hutumia mbinu mbalimbali za kuboresha msamiati uliopo ili ubebe dhana za ziada. Miongoni mwa mbinu zitumiwazo ni uradidi. Uradidi ni dhana inayojitokeza katika lugha nyingi kwa lengo la kuboresha msamiati uliopo ubebe dhana za ziada. Katika lugha ya Kiswahili, tukiacha dhima nyingi nyingine kama zile zilizobainishwa na Ashton (1944:316-318), uradidi unaweza kutumika katika mosi: kuimarisha au kudhoofisha maana, pili, kuongeza na kupunguza msisitizo wa dhana inayozungumziwa. Kwa hiyo, wakati mwingine mtumiaji wa lugha ya Kiswahili hulazimika kutumia mbinu ya uradidi ili kuwasilisha dhana ambayo ama haina msamiati unaojitegemea au mzungumzaji hajui msamiati unaofaa kutumika katika muktadha unaohusika.  Dhana hii ya uradidi hujitokeza zaidi katika lugha ya mazungumzo ambapo wazungumzaji wanakuwa huru kutumia mbinu zozote wanazozijua ili kuwezesha mawasiliano yafanikiwe kwa kiwango kinachostahili. Katika makala haya, tutaonesha namna uradidi unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili.

Kwa mujibu wa Rubanza (1996), anafasili uradidi kuwa ni njia ya kuunda maneno mapya katika Kiswahili, kama ilivyo katika lugha zingine ni kurudufu au kwa maneno mengine ni kurudia maneno. Neno lote zima linarudiwa au sehemu ya neno linarudiwa. Linaporudiwa neno zima kitendo hicho huitwa urudufu kamili na linaporudiwa sehemu ya neno ni urudufu nusu.

Kwa mujibu wa Matinde (2012), uradidi ni utaratibu unaotumika katika kuunda maneno ambayo sehemu ya neno lote hurudiwa na kuunda neno au msisitizo fulani. Fasili ya Matinde ina upungufu katika kufasili hasa nini maana ya uradidi kwani si lazima neno lote lirudiwe, huweza kuwa sehemu tu ya neno.

Hivyo tunaweza kusema kuwa, uradidi ni kanuni au utaratibu katika lugha wa kuunda neno/maneno mapya kwa namna ya kurudia sehemu ya neno au neno zima. Ili hali sehemu ya neno ikirudiwa huitwa urudufu nusu na ikiwa ni sehemu nzima ya neno hujulikana kama urudufu kamili.

Katika lugha ya Kiswahili, uradidi unajitokeza katika namna zifuatazo:

Kwanza uradidi hujitokeza kama uradidi kamili. Uradidi kamili ni uradidi ambao neno zima hurudiwa. Uradidi huu hutumia kanuni ya neno jumlisha neno kuleta neno jipya.

 Mifano:

Kanuni: Neno + neno = Neno jipya.

Peta + peta   =   petapeta

Pole + pole   =   polepole

Haraka  + haraka  =  harakaharaka

Cheka + cheka  =  chekacheka

Pilika + pilika = pilikapilika

Pika  + pika = pikapika

Shamra + shamra   =  shamrashamra

Cheza  +  cheza  = chezacheza

Kimbia  + kimbia  = kimbiakimbia

Sema+sema= semasema

Zima+zima= zimazima

Ruka+ruka= rukaruka

Pia, uradidi hujitokeza kama uradidi nusu. Uradidi nusu ni aina ya uradidi ambao sehemu tu ya neno hurudiwa.

Mifano:

Ki + zungu + zungu    = kizunguzungu

Ki + wili + wili =           kiwiliwili

Ki + nyume + nyume = kinyumenyume

Ki + nyevu + nyevu    = kinyevunyevu

Ki + mbele + mbele     = kimbelembele

Ki+china+china = Kichinachina

Ki+baba+baba=kibabababa

Ki+leo+leo=kileoleo

Katika mifano hiyo tumeona uambatanishaji wa mofimu tatu, yaani mofimu {ki-} na mofimu huru mbili. Kiambishi awali {ki-} kinadondoshwa katika neno la pili. Kanuni: {ki} +{m-huru} + {m-huru} = Neno.

Hivyo ndivyo uradidi unavyojitokeza katika lugha ya Kiswahili. Uradidi ni miongoni mwa njia ambazo zimekuwa zikitumika katika kuongeza msamiati wa lugha ya Kiswahili. Mbali na uradidi, zipo njia zingine zinazotumika kuunda msamiati wa lugha ya Kiswahili. Njia hizo ni: Utohoaji na uambatanishaji.

Marejeo

Massamba, D.P.B (2009). Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha. Dar-Es Salaam: Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.

Matinde, R. S. (2012). Dafina ya Lugha Isimu na Natharia. Kwa Sekondari, Vyuo Vya Kati na Vyuo Vikuu. Mwanza: Serengeti Educational Publishers.

Rubanza, Y. I. (1996). Mofolojia ya Kiswahili. Dar-Es Salaam: Chuo Kikuu Huria Cha Tanzania.

Unahitaji Kufanyiwa Swali Lako? Gusa Hapa Kuwasiliana Nami.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne