Ufahamu na Ufupisho | Kiswahili Kidato cha Tano na Sita
Ufahamu
ni kujua au kulielewa jambo hatimaye kuweza kulifafanua. Mtu anaweza akaona,
akasoma, ama akasikia jambo na akaelewa au asielewe. Akielewa atakuwa na uwezo wa
kufafanua au kutoa taarifa zinazohusiana na habari hiyo.
Ufahamu wa kusikiliza na ufupisho
Ufahamu
wa kusikiliza ni ule ambao mhusika anapata taarifa hiyo kwa kusikiliza habari
hiyo. inawezekana kupata habari hiyo kwa kusimuliwa au kusomewa.
Ili
kupata habari inayosikilizwa au inayosomwa, msikilizaji azingatie mambo haya:
- Kuwa
makini kwa kila kinachosimuliwa au kinachosomwa.
- Kuhusisha
mambo muhimu na habari isimuliwavyo.
- Kujua
matamshi ya mzungumzaji.
- Kubainisha
mawazo makuu.
Kujibu maswali kutokana na habari uliyoisikiliza
Mbinu
za kujibu maswali kutokana na habari ya ufahamu wa kusikiliza ni:
- Kusikiliza
kila swali kwa makini.
- Kutafakari
kila swali, yaani kutafuta maana ya swali kwa kulihusisha na matini
aliyosimuliwa.
- Kujibu
kila swali kwa ufupi na kwa usahihi, azingatie kiini cha swali na yaliyo katika
matini.
Kufupisha habari uliyoisikia
Ufahamu
wa habari uliyosikia una maana ya kueleza habari uliyoisikia kwa ufupi kwa
kutumia maneno yako mwenyewe.
Hatua za ufupishaji wa habari uliyoisikia
1. Kusikiliza
habari kwa makini.
2. Kubaini
na kutambua mawazo makuu katika kila aya.
3. Kuunganisha
mawazo makuu na kueleza habari hiyo kwa maneno yako mwenyewe.
Habari
hufupishwa mpaka kufikia theluthi ya habari ya awali.
Kichwa
cha habari hupatikana mara baada ya kubaini mawazo makuu. Pia, kichwa cha
habari hakitakiwi kuzidi maneno matano isipokuwa kama itaelekezwa vinginevyo.
Ufahamu wa kusoma na ufupisho
Ufahamu
wa kusoma ni kuzingatia maana ya neno, sentensi na habari yote. Msomaji
anatakiwa aweze kutambua mpangilio wa herufi, maneno na kuzitofautisha. Hivyo
basi, msomaji hutakiwa kueleza jinsi alivyoelewa habari aliyosoma.
Ufahamu
wa kusoma ni ule uelewa ambao hupatikana kwa: kusoma kwa sauti, kusoma kwa
haraka na kimya na kusoma kwa makini.
Katika ufahamu wa kusoma, msomaji anatakiwa kubainisha:
- Mawazo
makuu.
- Maana
ya maneno na misemo.
Kujibu maswali yanayotokana na makala uliyosoma
Ili
kujibu maswali, msomaji anatakiwa kufuata hatua zifuatazo:
- Soma
makala inayohusika.
- Soma
maswali yaliyoulizwa ili kujua kinatakiwa nini?
- Rudia
kusoma makala yote. Safari hii soma kwa makini zaidi.
- Tumia
kalamu ya risasi kuweka alama katika sehemu ambazo unahisi ni majibu.
- Baada
ya kusoma tena habari na umeweka alama ya sehemu ambazo unahisi ni majibu, sasa
jibu maswali.
Maswali
yanaweza kutungwa katika namna ya maswali mafupi na maswali marefu.
Maswali
mafupi huhusisha: maswali ya kuchagua, maswali ya kukamilisha jibu na maswali
ya kuoanisha.
Maswali
marefu ni yale yanayotaka kujibiwa kwa kuweka maelezo marefu.
Ufupisho (muhtasari) wa habari uliyosoma
Ufupisho
wa habari uliyosoma ni kitendo cha kuelezea habari hiyo kwa ufupi. Ufupisho
hukamilika pale msomaje anapounganisha mawazo yake mwenyewe ilimradi tu, habari
hiyo iwe na mawazo sawa na ile habari anayoifupisha.
Ufupisho husaidia katika shughuli mbalimbali kama:
- Wakati
wa kutayarisha ripoti na kumbukumbu za mkutano.
- Uhariri
wa habari.
Kanuni za ufupisho
- Kuwa
na stadi zitakiwazo katika kusoma yaani ufahamu, ugunduzi na upangaji wa mambo
maalumu yatakiwayo.
- Habari
iwe fupi.
- Taarifa
na maneno muhimu tu ndiyo yanayohitajika.
- Habari
ieleweke, isipoteze kiini chake.
- Hoja
na mawazo yaungane, yafuatane na yachukuane.
- Sentensi
ziwe kamili.
Hatua za ufupisho
- Soma
habari yote mpaka uielewe.
- Chagua
taarifa au maneno maalumu.
- Kulinganisha
taarifa muhimu na habari ya asili.
- Kuandika
muhtasari kama ilivyotakiwa.
- Kukamilisha
usawa wa ufupisho na habari ya asili.
Maswali
1. Soma kwa makini kifungu hiki cha habari
kisha jibu maswali yanayofuata.
UTUPU
ni hali ya kutokuwa na kitu. Huenda ukawa utupu wa pochi, chumba, mali, akili
na hata utupu wa mwili. Wahenga wa zamani (sio hawa wa mitandaoni), waliupuuza
utupu kwa kusema, Mkono mtupu haurambwi.
Hali
ya utupu hivi sasa inazidi kubadilika kwa kasi. Utupu umegeuka kitu. Utupu unategemewa
kumvusha mtu kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
Tazama
nyimbo za wanamuziki zilivyo. Wasichana wanaotumika humo wanacheza utupu kabisa. Hawaogopi lolote na
hata aibu hawaoni.
Zamani
wazee walipotaka kumwaga laana, walitishia kuwaonesha watoto wakorofi utupu.
Enzi hizo kuonekana kwa utupu ilikuwa ni laana kubwa. Wapo ambao
walichanganyikiwa na kuwa wehu kwa sababu ya kadhia hii.
Vibinti
vya zama hizi vinapiga picha za utupu bila kuogopa chochote. Ukiviuliza kwa
nini vinafanya hivyo, utasikia vinajibu kuwa vinapenda kuwa hivyo… vinapenda
kukaa utupu. Ujinga mtupu.
Hali
ya mabinti kukaa utupu kwa kiasi kikubwa imepunguza hamu ya vijana kuoa. Ndio,
vijana wanaona kila kitu. Sasa aoe ili aone nini kingine.
Maadili
yamebadilika sana sasa. Ni kweli kuwa hapo zamani mwanadamu alitembea utupu.
Lakini tamaduni hubadilika kulingana na wakati. Mwanadamu tangu kupata
ustaarabu wake, utupu si jambo la kuonyesha hadharani.
Bado
ninaendelea kutafakari nguvu hii ya utupu kukamata hisia za watu imetoka wapi?
Ni kweli wanaowachezesha mabinti wakiwa watupu namna ile watafurahi wakiwaona
watoto wa kuwazaa wao wakifanya vile? Lazima sasa turejee katika maadili.
Heshima iwepo.
Jamaa
mmoja aliwahi kunieleza kuwa, utupu kuzidi kuonekana mara kwa mara kumemwaga
laaana kali katika jamii. Ndiyo maana kila kukicha limeibuka lile, mara
limetokea hili.
Sina
uhakika kama kuna sheria inayoeleza lolote kuhusu mavazi. Ni wakati wa
kulitafakari hili kabla hali haijawa mbaya zaidi.
Ni
utupu wa fikra kuamini kuwa utupu unaweza kukupatia mafanikio. Sana utaambulia,
kupata umaarufu wa mpito.
Maswali
a. Toa maana ya maneno haya kama
yalivyotumika katika habari uliyoisoma.
i. Wahenga.
ii. Laana.
iii. Sheria.
iv. Zama.
v. Tamaduni.
b. Mwandishi ana maana gani anaposema
“waliupuuza utupu kwa kusema, Mkono mtupu haurambwi.”
c. Unaelewa nini kuhusu mabinti wa zama
hizi? Toa maelezo kwa mistari isiyozidi mitatu.
d. Kwa kutumia aya ya tatu, mwandishi ana mtazamo
gani kuhusu wanamuziki.
2. Fupisha habari uliyoisoma kwa maneno 100.