Namna Sahihi ya Kusoma Itakayomsaidia Mwanafunzi Kufaulu

Msichana amelala akiwa kaegamia meza.
Wanafunzi wenzako wanasoma kidogo, lakini wanafaulu vizuri. Wewe unakesha darasani, huna muda wa kupumzika, lakini matokeo yako ni mabaya! Tatizo lipo katika namna unavyosoma. Hata ukikesha, hutaweza kufaulu endapo hutakuwa na namna sahihi ya usomaji.
Hizi ni mbinu sahihi za usomaji ambazo zitakusaidia uweze kufaulu mitihani yako:

     1.   Weka malengo

Usisome bila malengo. Lazima kuwe na sababu ya wewe kusoma. Miongoni mwa sababu za kusoma zinaweza kuwa: kufaulu mtihani, kumaliza shule au chuo, kupata alama nzuri, kuwafurahisha wazazi na wewe mwenyewe ama kupata ujuzi kwa ajili ya kazi utakayofanya siku zijazo.

     2.   Chagua sehemu sahihi ya kusomea

Unashauriwa kuchagua sehemu ambayo ina mwanga wa kutosha na ambayo haina makelele. Wapo wanafunzi ambao wanapenda kusoma katika sehemu zenye kelele, kama una uwezo huo siyo vibaya. Hata hivyo ushauri wangu ni kuwa, sehemu isiyo na kelele nyingi ni nzuri zaidi kwa kusoma.

     3.   Epuka vitu vitakavyokuzuia kusoma

Kusoma ukiwa unasikiliza redio au unaangalia televisheni kutakufanya uache kusoma kwa muda na umakinikie kusikiliza au kutazama kitu fulani kitakachokufurahisha. Vivyo hivyo kusoma ukiwa na simu yako huku ukipokea simu na kujibu meseji Haifai. Ukiamua kusoma, hakikisha kazi inakua moja tu. Kusoma.

     4.   Penda kusoma

Usisome kwa kujilazimisha. Usisome kwa sababu ni muda wa kusoma na usipofanya hivyo utafokewa. Penda kusoma, tambua kwamba, elimu unayoipata hapo ndiyo maisha yako ya baadae.

     5.   Tumia muda vizuri

Usiwe mtu wa kuahirisha mambo. Panga ratiba na ifuate. Pia, orodhesha mambo yote unayotaka kuyafanya katika siku fulani kisha hakikisha yote unayafanya na kuyakamilisha. Usiwe mtu wa kukamilisha mambo kesho, kamilisha mambo leo.

     6.   Usiwe na hofu ya mtihani

Ili usiwe na hofu ya mtihani, jiandae mapema. Kadri maandalizi ya mtihani yalivyomazuri, ndiyo hofu ya mtihani inavyozidi kupungua. Pia, katika mtihani, usijilinganishe na wengine. Usifikirie, “Makubi atapata alama nyingi kuliko mimi.” Wala, “sijui kitu kabisa, mtihani huu nakwenda kufeli.”
Epuka mawazo hasi, fikria mawazo chanya pekee. Weka mawazo haya unaposoma, “nakwenda kufaulu mtihani huu kwa sababu nimejiandaa vizuri.”

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Uhakiki wa Riwaya ya Watoto wa Maman’tilie