Jinsi ya Kusoma Bila Kusahau Ulichosoma

Nyuki katika ua.
Kwa muda mrefu nimekuwa nikiitwa na waziri niende kumfundisha binti yake ambaye ni mwanafunzi jinsi ya kusoma bila kusahau alichosoma. Binti huyu ana tatizo la kusahau anaposoma na kupelekea matokeo mabaya ambayo mwisho wake ingekuwa kurudia darasa ama kuhamishwa shule. Baada ya kumpiga chenga waziri kwa muda mrefu, hatimaye siku moja wakati wanafunzi wapo likizo, nilipata muda, haraka nikaelekea nyumbani kwa waziri.

“Umebeba nini?” aliniuliza mlinzi wa waziri baada ya kunikagua kwa kifaa cha ukaguzi.

“Beretta.” Nilijibu.

“Iache hapa ukitoka utaichukua.”

“Sawa.” Nikafanya alivyotaka kisha nikaingia ndani. Waziri alinipokea kwa furaha tele. Tulizungumza habari za siasa mpaka tukachoka, sasa nikaomba nionane na yule niliyemfuata. Kama nilivyosema awali, binti waziri amekuwa akisoma kwa bidii lakini anasahau anachosoma.

Nilikuwa uso kwa uso na msichana mdogo anayesahau kila akisoma. Nilihisi kama ananiogopa, hivyo nikaamua kumuuliza swali la kumfanya anizoee.

“Mimi ni mtu au ng’ombe?” niliuliza, binti akacheka, nikahesabu meno yake, ishirini na nane, hapo nikagundua nilikaa na msichana mdogo wa miaka 16.

Baada ya mazungumzo ya hapa na pale, hatimaye nikampa somo lililobadili maisha yake:

JINSI YA KUSOMA BILA KUSAHAU ULICHOSOMA

     1.   Penda unachosoma

Ukisoma kitu unachopenda kuna uwezekano mkubwa wa wewe kukumbuka. Ni nyimbo ngapi unaweza kuziimba, wala hukufanya bidii yoyote kuzikariri nyimbo hizo lakini zipo kichwani. Ni kwa sababu ulizipenda nyimbo hizo. Hivyo unaposoma, penda kile unachosoma. Soma ukitabasamu, usikunje sura, elimu siyo vita!

     2.   Kuwa na malengo wakati wa kusoma

Unapoanza kusoma, jiulize, ‘kwa nini ninasoma kitu hiki?’ kwa mfano, kama unasoma mada ya uandishi, basi lengo lako ni kuelewa uandishi wa vitu mbalimbali kama vile barua, insha, risala, hotuba na vitu mbalimbali, hivyo inategemewa mwisho wa kusoma kwako, utakuwa umefahamu vitu hivyo.

     3.   Jipime mwenyewe unaposoma

Unaposoma, kuwa na kalamu na daftari. Baada ya kila kipengele, jipime ili kuona kama unakumbuka. Kwa mfano kama unasoma mada ya ‘establishment of colonialism’ na umefika kipengele cha ‘methods used to establish colonialism’ fanya hivi. Kwanza andika kipengele hicho juu ya daftari, ‘methods used to establish colonialism.’ Baada ya hapo zisome njia hizo. Ukimaliza kuzisoma, ziorodheshe njia hizo bila kuangalia katika daftari. Unaweza kujikuta umekumbuka moja, mbili na pengine unaweza kukumbuka zote. Baada ya kuorodhesha, tazama zile ambazo ulizisahau kisha endelea na kipengele kinachofuata.

     4.   Jenga picha katika kichwa chako

Tunakumbuka zaidi picha kuliko maneno. Kwa mfano, unaposoma somo la Historia (leo sijui kwa nini mifano yangu ipo katika somo la historia.) unaposoma somo la historia, mada ya ‘colonial social services’, jenga picha kichwani mwako, kuwa kama unaona huduma za kijamii zilizotolewa na wakoloni, jenga picha ya shule za zamani, barabara na reli. Jenga picha ya mabomba na nyumba za wakoloni bila kusahau hospitali zao. Ukifanya hivi, huwezi kusahau.

     5.   Rudia tena na tena

Ukirudia mara nyingi, utakumbuka mara nyingi. Usisome mara moja ukaona umemaliza, rudia tena na tena. Pale unapofundishwa darasani isome mada hiyo. Unapokuwa na muda soma tena. Unapotangaziwa mtihani soma tena. Mada moja ukiirudia kuisoma mara saba kwa vipindi tofautitofauti, huwezi kuisahau!

     6.   Fanyia mazoezi ulichokisoma

Njia hii ni bora na inasaidia kukumbuka kwa haraka zaidi. kuna njia mbili za kufanyia mazoezi kile ulichokisoma:

Njia ya kwanza ni kumfundisha mtu kile ulichosoma. Soma, kisha muite rafiki, anza kumfundisha ulichosoma.

Njia ya pili soma mada fulani, kisha ita marafiki katika majadiliano ili kujadiliana kuhusu mada hiyo. Wakati wa majadiliano, toa hoja zako kuhusu mada hiyo. Utakuwa umefanyia mazoezi ulichosoma.

Nilimalizana na binti waziri. Nikaondoka zangu. Baada ya miezi kadhaa, nilianza kupokea meseji za pongezi kutoka kwa waziri. ‘Mwalimu Makoba, binti hasahau masomo siku hizi. Anafaulu vizuri na hawezi kurudia darasa.’
Akirejea tena, nitamfundisha mbinu saba za kufaulu mtihani wowote shuleni.

Hata wewe unaweza kusoma bila kusahau masomo yako endapo utazingatia mambo niliyofundisha hapo juu.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne