Niliugua Ugonjwa wa Ajabu Nikatibiwa na Babu wa Kichina 1



Simulizi hii haina uhusiano wowote na tukio la kweli lililowahi kutokea, bali ni matokeo ya fikra adimu za Mwalimu Makoba.
Tajiri Maige aliniita nyumbani kwake. Hii ilikuwa ni mara ya nane, kwa mara zote saba, ameniita asifanikiwe kunishawishi kwa jambo alilohitaji. Alihitaji kunituma nchi za mbali, niende uchina kwa kazi ya kumtafuta binti yake ambaye tangu aondoke nchini kwenda China kusoma, hajapata kurejea tena na sasa yapata mwaka wa saba. Hakuna barua, hakuna simu, hakuna mawasiliano!

“Mako… Mako… Mako…” aliniita tajiri Maige, “safari hii sitegemei jibu la hapana. Kila kitu kipo tayari. Naomba sana, nenda kamtafute mwanangu wa pekee Vida.”

Ukimya ulitawala kwa dakika saba sebuleni pale. Sikuwa tayari kwenda mbali na familia yangu, nilihitaji kupumzika na nilizichoka purukushani. Hata hivyo, nilijiwa na moyo  wa huruma, nikajikuta nikitamka kwa kauli thabiti.

“Nitakwenda peke yangu. Nitarudi na binti.”

Hivyo ndivyo nilivyokubali kuondoka nchini ili kwenda China kwa kazi ya kumtafuta mtoto pekee wa tajiri Maige. Ni binti ambaye aliondoka kwenda kusomea udaktari, lakini hakurejea yapata miaka saba. Tajiri Maige ambaye alifiwa na mke wake miaka tisa iliyopita, furaha pekee aliyokuwa nayo ilikuwa ni kumuona binti yake kipenzi Vida.

Siku ya Jumatatu nilikuwa ndani ya ndege ya kutoka Dar Es Salaam kwenda Beijing china. Nilikaa daraja la kwanza na iligharimu shilingi za kitanzania milioni saba na laki tatu kwa safari moja ya kwenda tu. Waliokaa daraja la pili yaani ‘bussiness’, wao iliwagharimu milioni tano, na waliokaa daraja la mwisho yaani ‘economy’, iliwagharimu shilingi milioni moja. Kukaa daraja la kwanza, ilikuwa raha ajabu na niliona kama dege lile la kampuni ya ‘Fly Emirates’ kama langu!

Zilipita saa mbili baada ya safari yetu kuanza. Hapo ndipo lilipotokea jambo la kuogopesha na kukatisha tamaa. Ndege yetu iligonga kundi kubwa la ndege ambao inaaminika walikuwa kunguru. Injini moja ikazima, hofu ya kifo, ikatufanya tusahau yale matabaka yetu ya daraja la kwanza, la pili na la tatu, wote tulishikwa na hofu kuu. Abiria wengi walilia, wachache walikaa kimya, lakini wakitetemeka.

Itaendelea...


Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Uhakiki wa Riwaya ya Watoto wa Maman’tilie