Mawazo Makuu ya Kahigi Katika Makala ya Structural and Cohesion Dimensions of Style


MAWAZO MAKUU YA KAHIGI KATIKA MAKALA YA STRUCTURAL AND COHESION DIMENSIONS OF STYLE

Soma makala ya Kahigi (1997) ya Structural and Cohesion Dimension of Style: Consideration of Some Text in Maw (1974) na uelezee mawazo makuu ya mwandishi katika kurasa zisizozidi tatu.

Profesa Kulikoyela Kahigi ni mwanaisimu, mwanasiasa na mshairi maarufu. Mtaalamu huyu, amefanya tafiti nyingi katika isimu ya kibantu, mitindo katika isimu na leksikografia. Makala ya Kahigi, ni matokeo ya kitabu cha Maw (1974). Makala ya Structural and Cohesion Dimension of Style: Consideration of Some Text in Maw, imegawanyika katika maeneo makuu matano ambayo ni, utangulizi, mtazamo wa ushikamani, ushikamani katika matini mbalimbali za kiswahili, vipengele vya kimuundo na vipengele vya kiushikamani na mwisho kamaliza kwa kutoa hitimisho. Kama inavyoelezwa katika kamusi ya TUKI (2004), wazo ni jambo ambalo mtu analifikiri. Hivyo basi mawazo makuu ya mwandishi katika makala hii yanajadiliwa katika aya zifuatazo.
          Wazo kuu la kwanza la mwandishi ni, mtazamo wa ushikamani na uhusiano wa kiushikamani. Mwandishi anaeleza kuwa, ushikamani huhusiana na kufanya matini iunganishwe pamoja kwa kutumia nyenzo kama, urejeleo, ubadala, udondoshaji na uunganishaji. Taaluma hii ilianzishwa mnamo karne ya 16 na 17 na wanaisimu wa kipindi hicho hususani H&H. Katika mtazamo huu, mwandishi anajadili dhana ya uhusiano wa kiushikamani kuwa “ni uhusiano wa kimaana kati ya vipashio au vijenzi katika matini na baadhi ya vijenzi vinginevyo vya msingi katika kufasili matini” (H & H uk.8). Uhusiano huu unafafanuliwa zaidi kwa mfano ufuatao.
Kwanza, mvulana humchagua msichana amwonaye afaa kwa ndoa. Kisha huwaambia wazee wake.”
Katika mfano huo, neno kisha linarejelea kwanza, na kamwe haliwezi kueleweka mahali hapo kama kusingekuwa na neno kwanza. Hivyo maneno hayo yanahusiana. Pia, mwandishi anaeleza aina tano za uhusiano wa kiushikamani ambazo ni, urejeleo, ubadala, udondoshaji, uunganishaji na ushikamani wa kileksika. Pasipokutumia vigezo hivyo, ni vigumu kuupata ushikamani.
          Wazo jingine la mwandishi ni, ushikamani katika matini mbalimbali za kiswahili. Wazo hili linajaribu kuangalia kama kuna ushikamani wowote katika matini za kiswahili. Ili kusaidia uelewa, mambo ya kuzingatia katika uchambuzi wa matini yanatajwa kuwa ni: idadi ya vijenzi vya ushikamani, vipashio katika sentensi inavyofanya kazi kiushikamani, aina ya ushikamani inayohusika katika kila ufungamanifu na umbali wa ushikamani. Katika hoja hii, Kahigi anatumia kauli za kitafiti ambazo zinajumuisha uchunguzi juu ya sifa bainifu za ushikamani wa kisarufi na kileksika na sentensi zinazochukuliwa kama nduni za kielimu mitindo za kila matini. Kama zinavyoelezwa hapa chini.
Utafiti wa kwanza umefanyika katika hoja zilizoandikwa na matokeo yake ni haya: hoja hizi hujumuisha takriri, maneno ya usawe na maneno vipashio ambayo hayawezi kuainishwa kwa urahisi. Mtoa hoja huepuka kurudiarudia maneno bali huyachagua katika seti mbalimbali za kileksika. Utafiti wa pili unazungumzia kifungu habari cha drama, hiki kinatoa sifa zifuatazo: kuna ushikamani wa kiubadala kwa kiasi kikubwa, kuna udondoshaji kwa kiasi kikubwa, maswali ya hapo kwa hapo, pia matini inaonekana kuwa na uwiano wa juu zaidi wa vijenzi vya umbali na urefu wa kudumu. Utafiti mwingine ulifanyika katika kifungu habari cha kisiasa, ushawishi wa mazungumzo na masimulizi.
Mwandishi hakuishia kuwa na mawazo hayo tu, bali wazo jingine tofauti na hayo yaliyopita linapatikana ambalo ni, uhusiano uliopo kati ya matini andishi na sifa za ushikamani. Uhusiano ulipatikana kwa kuangalia matini mbalimbali za kiswahili ambazo ni, Uhuru, Julai 26, 1969 (Usumbufu katika mchezo wa kandanda), mkusanyiko wa matangazo kutoka Taifa Tanzania, Aprili 13, 1968, Wasifu wa Siti Binti Saad, S. Robert, Kifungu cha habari kilichosimuliwa na Yakubu wa Tanga na makala nyingine nyingi zimechambuliwa na kuonesha uhusiano wa matini andishi na sifa za ushikamani.

Kwa kuhitimisha, malengo ya makala hii ya Profesa Kahigi ni mawili, lengo la kwanza ni kuongeza ushikamani katika uchambuzi wa mtindo wa kiswahili kama ilivyooneshwa na Maw (1974), na lengo la pili ni kuangalia kama kuna uhusiano wowote kati ya muundo na ushikamani. Mawazo makuu yanayoonekana katika makala hii, yana mchango mkubwa sana katika taaluma ya ushikamani.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne