Uhakiki wa Diwani ya Fungate ya Uhuru



Uchambuzi wa Mashairi

JINA LA KITABU; FUNGATE YA UHURU
MWANDISHI; MOHAMED SEIF KHATIBU
MCHAPISHAJI; DUP
MWAKA; 1988
MHAKIKI; Daud Makoba

UTANGULIZI

Fungate ya uhuru ni diwani inayozungumza bila kificho matatizo yote yanayozipata nchi zinazoendelea. Mwandishi kwa namna fulani anaona kuwa uongozi ndio tatizo la kwanza linalosababisha maafa haya. Mwandishi anawachora viongozi wa Afrika wakiwa katika ‘fungate’ wakisherekea matunda ya uhuru bila kukumbuka sasa ni wakati wa kuachana na sherehe hizo na kuwaunganisha watu kuijenga nchi yao.

Maudhui

Dhamira

1.  Ukombozi wa kisiasa

Tatizo kubwa linalojadiliwa na mshairi ni anasa zinazoendekezwa na watawala. Watawala hawawajibiki badala yake wanaponda starehe na kusababisha uchumi uzorote. Katika shairi la ‘Fungate ya uhuru’ mshairi anasema,
"Karamu za fahari, mabembe ya kupepea.

Namajumba mazuri, wamekwishajijengea.Watembea kawa magari, hivi zimewazowea." Uk.1
Paa, ni mnyama porini,ni mwenye nyingi papara.
Paa,ni kuteka mekoni, moto uwake imara.
Paa, ni toa magambani, samaki atiye sura.
Paa, pia la nyumba, kmakuti au karara.”
Na kazi ikatayarishwa,
Ili uchafu kuondoshwa.”

2.  Kuuheshimu na kuutunza utamaduni wa kiafrika

Katika utamaduni mshairi analizungumzia suala la lugha ya Kiswahili, anawaasa wanajamii waiheshimu na kuitunza ligha hii kwani ni kitambulisho cha utamaduni wetu. Katika shairi la Dafina mshairi anaonesha jinsi ambavyo lugha ya Kiswahili inajitosheleza na utamu ilionao hasa katika mchezo wa maneno,
Paa, ni kuruka angani, kama ndege na tiara.

3.  Usaliti

Mshairi amefanikiwa kujadili kwa kina usaliti unaofanywa na viongozi, anatoa ahadi ya kuwahukumu viongozi wasaliti, pia anauasa umma usicheke na viongozi hawa kwani ndio chanzo cha umasikini na matatizo yote katika jamii. Katika shairi la Nikizipata bunduki, mshairi anasema,
"Nikizipata shembea,
       Takamata viongozi, wasaliti wa nchini,
       Niwachinje kama mbuzi miiko wasoamini…"

4.  Wizi

Mshairi anatoa kauli kali kuwa wizi upo kila sehemu, hata katika nyumba za ibada! Anaionesha jamii ikiwa imeoza, isiyo na uaminifu hata kidogo, katika jamii hii kila mtu anaiba! Ajabu ni kwamba hata vyombo vya usalama vilivyoaminiwa kukabiliana na wezi navyo vinakengeuka na kupita katika mkondo huu. Katika shairi la Wizi mshairi anasema,
“Walinzi hawapo? La hasha!
 polisi hulinda wezi,
 majeshi huhalalisha wezi,
 na dini zawabariki wezi”

5.  Unyonyaji

Mshairi anadadavua bila kuogopa namna ambavyo mataifa yaliyoendelea  yanavyolinyonya bara la Afrika. Rasilimali zote huibiwa na mataifa haya na kuyafanya yatajirike huku nchi za kiafrika zikididi kudidimia katika lindi la ufukara. Mshairi katika shairi la Afrika anasema
       Bara la Amerika, Na Ulaya kadhalika,
       "Wamestaarabika"
 Kunyonya Afrika, Ni kwa mingi miaka,
       Nasi tukafukarika.

6.  Mapenzi

Mshairi anamsimanga mwanamke ambaye alimpenda hapo awali kabla hajabadilika na kuamua kumwacha. Mshairi anaonesha jinsi ambavyo mahusiano ya wawili hubadilika pale ambapo mmoja huamua kuvunja kiapo. Katika shairi la U wapi uzuri wako? Mshairi anatoa yote ya moyoni mwake jinsi ambavyo aliachwa na mwanamke aliyempenda. Hata hivyo mwanamke huyo alikokwenda hakukuwa mahala sahihi kwani alipoteza sifa zake zote za mwanzo.
Bao la mkahawani , kila mtu akalia…
Sasa jamvi la wageni, wajapo huwapokea…
Pia mashairi mengine yanayozungumzia mapenzi ni kama, Nchi yangu, Wewe peke yako, Nia yangu sigeuzi, na Kuntu sauti ya kiza.

Ujumbe

1.  Ili nchi ipate maendeleo lazima iwe na viongozi wachapakazi na waaminifu.
Kama inavyothibitishwa katika shairi la ‘Fungate ya uhuru’. Mwandishi anaonesha jinsi ambavyo viongozi wazembe na wavivu wanavyolikosesha maendeleo taifa.
2.  Lugha ya kiswahili ni kitambulisho cha taifa letu hivyo ni lazima tuitunze na kuithamini wakati wote.
Ujumbe huu unapatikana katika shairi la Dafina.
3.  Wizi ni chanzo cha umasikini na matatizo yasiyokwisha
Mshairi anaonesha jinsi ambavyo jamii inakaliwa na watu wanaoendekeza vitendo vya wizi bila kufanya kazi. Katika jamii hii, mshairi anasema kila mtu anaiba hata askari wenye jukumu la kulinda watu na mali zao nao wanajihusisha na vitendo vya wizi! Ujumbe huu unapatikana katika shairi la Wizi.
4.  Mataifa yaliyoendelea yanazinyonya nchi za kiafrika na kuzifanya ziwe na uchumi duni.
Ujumbe huu unajitokeza katika shairi la Afrika.

Migogoro

1.  Migogoro ya kisiasa

Kuna uhusiano mbaya baina ya serikali na watu wake. Raia wanaonekana kuchoka hata wanahidi kuwaangamiza viongozi wao kama ilivyojadiliwa katika shairi la Nikizipata bunduki.

2.  Migogoro ya kiuchumi

Shairi la Fungate ya uhuru, linaonesha kwa kina mgogoro huu. Hii inathibitishwa kwa uwepo wa matabaka kati ya wenye nacho na wasio nacho. Wasionacho wanaishi maisha duni na manung’uniko makuu, huku wenye nacho wakiendelea kula fungate. Katika shairi la Nikizipata bunduki masikini wanaahidi kupambana na matajiri ili nao waipate keki ya taifa.

Msimamo

Mshairi anamsimamo wa kimapinduzi kwani anashauri kuwa matatizo yote yaliyopo katika jamii kama rushwa, wizi, umasikini na mengine mengi suluhisho lake ni wananchi kuwaondoa viongozi wazembe na wala rushwa na kuweka viongozi imara ambao wataisimamia serikali katika  kujiletea maendeleo.

Falsafa

Mwandishi Mohamed Seif Khatibu, falsafa yake anaamini katika ujamaa, anaona kuwa itikadi ya ujamaa ndiyo inayofaa kufuatwa na nchi za kiafrika ili kuleta usawa, haki na maendeleo ya watu wake, anaamini kuwa ujamaa unaweza kuondoa unyonyaji, matabaka na mambo yanayofanana na hayo katika jamii.

Fani

Muundo

Katika utanzu wa ushairi, muundo tunaangalia idadi ya mistari katika beti, kama mwandishi katika diwani yake atatumia mistari miwili katika kila ubeti, basi tutasema kuwa mwandishi ametumia muundo wa tathnia, na kama atatumia mistari mitatu kwa kila ubeti, tutaseama kuwa mwandishi ametumia muundo wa tathilitha, na mistari mine ni muundo wa tarbia na mistari mitano na kuendelea utakuwa muundo wa takhmisa.
Kwa upande wake, mshairi Mohamed Seif Khatibu katika diwani hii, ametumia muundo changamano kwani mashairi tunayoyaona katika diwani hii ametumia miundo zaidi ya mmoja.

-        Muundo wa Tathnia umeonekana katika shairi la Mjamzito.
“Mjamzito, Amelazwa "thieta"
Lazima kupasuliwa.”
-        Muundo wa Tathlitha umeonekana katika shairi la Waja wa mungu
“Dunia, vyakula hawavioni, mafakiri,
Lakini, vyakula kwao pomoni, mabepari,
Abadani, hawa si waja wa Mungu!”
-        Muundo wa Tarbia umeonekana katika shairi la Afrika.
"Bara la Amerika, Na Ulaya kadhalika,
"Wamestaarabika"
Kunyonya Afrika, Ni kwa mingi miaka,
Nasi tukafukarika."
-        Muundo wa Takhmisa umeonekana katika shairi la Unganeni.
“Wafanyakazi wa Afrika, tuunganeni,
Na wakulima kadhalika, tushikaneni,
Makabwela mnaosumbuka, tukutaneni,
Tujiandae kwa Mapambano, yalo Marefu,
Ushindi ni wetu.”

Mtindo

Mwandishi amatumia mtindo changamano yaani amechanganya mitindo yote ya aina mbili, yaani mtindo wa kimapokeo na mtindo wa kisasa.
Mashairi ya kimapokeo ni kama vile, "Mcheza Hawi Kiwete" [uk. 37-38], na "Ua Si Ruwaza Njema" [uk. 47-48].

Matumizi ya Lugha

i.                 Tamathali za semi
-        Tashibiha
Nabaki kugunaguna, kama nyani kwenye nyika katika shairi la "Ningekuwa na Sauti" [uk.10-11]
-        Sitiari
Bao la mkahawani , kila mtu akalia, katika shairi la U wapi uzuri wako.
-        Takriri
Mbinu hii inajitokeza katika shairi la "Dafina" uk. 8-9 ambapo tunaona mwanzoni mwa kila mstari katika ubeti kuna maneno yanarudiwa rudiwa.
-        Tafsida
Hawezi kujifungua badala ya kutumia neno hawezi kuzaa ambalo ni neno kali sana, katika shairi la "Mjamzito" uk. 7

ii.             Lugha ya picha/taswira
Lugha ya picha iliyotumika ni pamoja na kunguru katika shairi la "Kunguru" [uk. 26-27], tunaposoma shairi hili tunapata picha kuwa, kunguru ni sawa na viongozi ambao tuliwachagua kuondoa matatizo katika jamii kinyume chake wao ndo wakazidi kuleta matatizo badala ya kuyaondoa kama walivyofanya kunguru weusi waliopandikizwa kuondoa uchafu badala yake wao ndo wamekuwa wakileta na kujaza uchafu na kuwa kero kwa jamii, mfano katika shairi hilo mwandishi anasema,

“Kunguru walisafilishwa,
Nchini wakahaulishwa,

Pia katika mshairi la Fungate ya uhuru mwandishi ametumia lugha ya picha kuwaelezea viongozi ambao hawafanyi kazi, wao bado wapo Fungate wanaponda raha.
Fungate ni kipindi ambacho bwana na bibi Harusi hutafuta sehemu ya kujistarehesha na kupumzika, kabla ya kuyaanza majukumu ya ndoa. Fungate hutarajiwa kufanyka kwa muda mfupi tu na kisha baada ya hapo shughuli nyingine huweza kuendelea. Maharusi wanapoendelea kubaki fungate kwa muda mrefu huacha mishangao na kwa vyovyote kazi zao hazitaendelea, isipokuwa watawaumiza wale waliowachangia ili waende fungate. Mshairi anaeleza kuwa,  Viongozi wetu toka uhuru mpaka leo bado wanasherehekea matunda ya uhuru wakiwa wamesahau majukumu yao.

Kufaulu na Kutofaulu kwa Mwandishi

Kufaulu

Kwa kiasi kikubwa mwandishi amefaulu katika vipengele vyote vya fani na maudhui, kwa mfano, kimaudhui, amefanikiwa kuonesha matatizo mbalimbali yanaikabili jamii yake na kuipa njia jamii yake namna inavyoweza kuondokana na matatizo hayo. [rejea dhamira mbalimbali]
Kifani amefanikiwa, ametumia muundo changamani jambo ambalo linaweza kumsaidia msomaji wa kazi yake kujifunza namna ya kuandika mashairi yenye miundo tofauti tofauti, pia ametumia mtindo changamani yaani hakufungamana katika mtindo mmoja tu, ametumia mitindo yote, yaani mashairi ya kimapokeo na kisasa ambayo nayo huweza kumfanya msomaji wake, kuweza kujifunza namna ya kuandika na kutunga mashairi kwa mitindo yote hiyo.

Kutofaulu

Kama ilivyo kawaida huwa hakuna kazi isiyo na mapungufu, hivyo hivyo katika diwani hii kuna mapungufu mbalimbali yanajitokeza ingawa si kwa kiwango kikubwa sana, kwa mfano, baadhi ya njia ambazo mwandishi anazitoa jamii kuzitumia ili kuondokana na matatizo zinaweza kuhamasisha jamii kujichukulia sheria mikononi wakati vipo vyombo vya kisheria vinavyopaswa kufanya hivyo, mfano rejea shairi la, "Ningekuwa na Sauti" uk. 10-11, na shairi la "Nikipata Bunduki" uk. 11.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Uhakiki wa Riwaya ya Watoto wa Maman’tilie