Safari ya Kuusaka Mwezi | Sehemu ya Kwanza
Naitwa Nkenye, nina umri wa miaka Tisa, leo nataka
niwasimulie tukio lililotokea katika Nchi yetu ya Rahaja miezi miwili tu
iliyopita. Tega sikio…
Ilikuwa usiku wa manane niliposikia kelele za watu nje
ya nyumba yetu ya nyasi. Niliamka haraka kisha nami nikaelekea nje ili nikapate
kujua kilichokuwa kikiendelea. Huko nje nilikuta watu wote wamesimama wakipiga
kelele huku wakiwa wameangalia juu.
“Mwizi! Mwizi! Mwizi!”
Nami nilitazama juu ili nione kilichowaliza, Loooh! Nilikiona
kijitu kichafu kimevaa koti jeusi toka sayari ya mbali kikiwa kimeubeba mwezi
wetu kikikimbia nao kuelekea mbali huko juu angani. Kabla sijashusha uso wangu
chini giza kuu liliingia hata hatukuweza kuonana.
Vijana wa usalama wa nchi, waliwasha mienge ya moto
hapo tuliweza kuonana tena, wote tulikuwa na masikitiko makubwa. Nilimuona mama
na kaka yangu Mowasha wakilia kwa huzuni.
Watu wote walitamani kusikia chochote kutoka kwa mkuu
wa usalama wa nchi ambaye alikuwepo katika eneo hilo, baada ya matarajio mengi
mkuu wa usalama wa nchi alikohoa kisha akazungumza,
“Ndugu zangu mwezi umeibwa na kijitu toka sayari ya
mbali, ni lazima mwezi wetu upatikane kwani bila mwezi kutakuwa na giza kali
sana ambalo litarahisisha wezi kufanya kazi zao. Vilevile, Dunia bila mwezi,
siku huisha kwa masaa sita tu, hivyo siku zetu za kuishi zitapungua… lazima
mwezi upatikane tuishi miaka mingi!”
“Ndioooo!” Sote tuliitika kwa nidhamu ya hali ya juu.
“Nawaombeni kesho tujitokeze mbele ya kibaraza cha
mfalme saa mbili kamili asubuhi, ili tuweze kuwajulisheni njia tutakayotumia
kuurejesha tena mwezi wetu.” Mkuu wa usalama wa nchi alimaliza kuongea kisha
wote tukasambaa kuelekea majumbani kumalizia usingizi.
Mimi niliongozana na mama, kaka yangu Mowasha na baba
yangu shujaa aliyeitwa Mako. Hatukuzungumza lolote njiani, tulihuzunishwa sana
na tukio lile la kuibwa mwezi. Nilihuzunika zaidi nilipofikiria kuwa hata siku
zetu za kuishi zingepungua!
XX XX XX XX
Saa mbili asubuhi Wananchi wote tulikusanyika kwenye
kibaraza cha mfalme kama ilivyoamriwa. Mfalme akiwa amevalia joho jeupe
alisimama akasema,