Uhakiki wa Riwaya ya Joka la Mdimu
Mwandishi: Abdallah Saffari
Mhakiki: Mwalimu Makoba
Simulizi kwa ufupi
Joka la mdimu ni aina ya nyoka ambaye hukaa katika majani ya kijani. Kwa kuwa nyoka huyu hufanana na majani, ni ngumu sana kumtambua. Joka hili la mdimu linafananishwa na viongozi. Viongozi hawa wanafanana na sisi kwa kila kitu hivyo ni vigumu mno kutambua hatari yao ya uongozi mbaya, rushwa, mauaji na ulaghai.
Cheche anaumia akishiriki maonyesho ya sherehe za uhuru. Kwa sababu ya kukosekana kwa fedha za kigeni, inashindikana kumpeleka Uingereza kutibiwa, na japo serikali inawajibika kumtibia, haionekani kufanya hivyo wala kujali. Baba yake anavamia benki, anapata fedha na kufanikiwa kumpelekea Uingereza kutibiwa.
Maudhui
Dhamira
Hali ngumu ya maisha
Katika riwaya hii tunauona ugumu wa maisha. Mhusika Jinja Maloni anafanya kazi yoyote ilimradi mkono uende kinywani. Anafanya kazi ya kuchimba makaburi na kupakua vyoo.
Hali hii ngumu ya maisha inasababishwa na uongozi mbaya, viongozi wameshindwa kuzuia rushwa, mfumuko wa bei na ukosefu wa ajira rasmi.
Rushwa
Bila rushwa hakuna huduma, mambo mbalimbali sasa hayafanyiki mpaka utoe chochote kitu.
Tino anatoa rushwa ili mkewe aweze kusafiri.
Cheche anahitaji kwenda kutibiwa uingereza, Dokta Mikwala anapewa rushwa ili aweze kuidhinisha kibali hicho.
Naye Brown Kwacha anatoa rushwa ili kuweza kujipatia kila anachohitaji.
Urasimu
Cheche anaumia katika sherehe za uhuru, lakini ananyimwa haki yake ya kwenda kutibiwa nje. Wahusika wanapiga chenga kila wanapofuatwa.
Mwisho Amani anaamua kutoa rushwa ili aweze kupata haki ya mwanae.
Kutowajibika
Brown Kwacha hawajibiki kwa umma kama kazi yake inavyotaka. Matokeo yake anaitumia ofisi hiyo kwa manufaa yake binafsi.
Nafasi ya mwanamke katika jamii
Mwanamke amechorwa katika mambo mbalimbali, mazuri na mabaya kama inavyoezwa:
Mzazi na mlezi wa familia. Mwema mkewe Tino aliwalea viizuri sana watoto wake Cheche, Tabu na Subira pia alimpenda na kumtunza vyema mumewe.
Pia mke wa Brown Kwacha aliwalea vyema mabinti zake watatu kwa kiasi kikubwa peke yake bila msaada wa karibu wa mumewe.
Mwanamke amechorwa kama chombo cha starehe. Katika riwaya tunaona namna mabaharia wanavyowatumia wanawake kwa lengo la kujifurahisha tu.
Pia, tunamuona Brown Kwacha akiwatumia wanawake kwa kujifurahisha.
Kiumbe duni. Mwanamke anaonekana duni asiyekuwa na mchango wowote. Brown Kwacha anamdharau mkewe na hamshirikishi kwa lolote.
Jasiri, upande mwingine mwanamke anaonekana mwenye ujasiri wa hali ya juu. Pamela anamkataa Brown Kwacha bila kujali fedha wala cheo chake.
Ujumbe
Viongozi wanasababisha hali ngumu ya maisha
Rushwa ni adui wa haki
Viongozi waache urasimu, watende haki kwa wote
Umasikini ni chanzo cha watu kujihusisha na matendo yasiyofaa kama vile uhalifu.
Migogoro
Jinja Maloni na Vibaka
Jinja anaingia katika mgogoro na vijana wanaojaribu kumbaka mwanamke, anawapiga na kumuokoa mwanamke yule.
Mgogoro baina ya Tino na Kondakta na Utingo wa basi
Kondakta na Utingo wake waliona Tino anawachelewesha, walishuka ili waweze kumpiga, lakini walipoona amesimama imara, walirudi ndani ya basi lao.
Mgogoro kati ya vjana waliokuwa wakipigania matenga yaliyokuwa yakishushwa, vijana hawa walipigana bila kuamuliwa na mtu yeyote mwishowe walichoka na kutazamana kama majogoo yaliyokuwa yakitangaza vita.
Mgogoro kati ya katibu mkuu wa wizara ya mila na utamaduni na kijana waliopigana katika uzinduzi wa nyumba ya Brown Kwacha,walikuwa wakimpigania mwanamke aitwaye Esther,walipigana mpaka wakatumbukia katika bwawa la kuogelea.
Migogoro ya nafsi
Tino ana mgogoro wa nafsi, anawaza na kuwazua juu ya namna ya kupata fedha za kuwezesha kumpeleka mtoto wake, Cheche nje kutibiwa.
Mtazamo/msimamo
Mwandishi ana mtazamo wa kimapinduzi.
Mwandishi anaeleza bila kuficha kwamba, viongozi ndiyo chanzo cha matatizo mengi yanayotokea katika jamii.
Falsafa
Mwandishi anaamini kuwa matatizo makubwa yanayojitokeza katika jamii yanatokana na uongozi mbaya.
Fani
Mtindo
Mtindo wa monolojia au masimulizi.
Mtindo wa dayolojia au majibizano
Matumizi ya nafsi ya tatu kwa kiasi kikubwa.
Matumizi ya nyimbo
Muundo
Riwaya ya Joka la Mdimu ina jumla ya sura kumi ambazo amezipa majina ya wahusika, mahali na matukio yanayobeba kisa kizima cha hadithi katika sura husika.
Mwandishi ametumia muundo wa rukia kwani amekuwa akisimulia visa kwa kusimulia matukio mengine na kuyaacha kuelezea matukio mengine katika sura tofauti tofauti.
Wahusika
Amani
Ni dereva taksi
Ni kijana mchapakazi
Ana huruma, hekima na busara
Rafiki yake Tino
Alimsaidia Tino katika tukio la kuiba benki.
Brown Kwacha
Ni mkurugenzi wa idara ya fedha za kigeni
Ni malaya
Anahudumia watu ofisini kwa upendeleo hasa wanawake
Ni mpenda rushwa.
Anajihusisha na magendo na ujangili
Tino
Ni mvuta kwama
Ni baba wa watoto watatu, Cheche,Tabu na Subira.
Ni jasiri sana
Ni mchapa kazi na mwanamichezo.
Jinja Maloni
Ni mtu mkakamavu na asiye mwoga.
Hufanya kazi kama za kupakua vyoo na kuchimba makaburi
Ana upendo na moyo wa kujitoa hasa inapokuja suala la kuokoa mtu
Anapenda muziki.
Dakta Mikwala
Ni daktari bingwa wa mifupa
Ni mlevi
Ni mpenda rushwa/hongo
Shiraz Bhanj
Ni mfanyabiashara mkubwa.
Ni mwajiri wa Amani
Rafiki yake Brown Kwacha
Ni mtoa rushwa
Cheche
Ni mtoto wa kiume wa Tino
Alivunjika kiuno katika michezo ya sherehe za uhuru
Ana tabia njema
Ni mcheshi, mdadisi na mwanamichezo
Alipendwa sana na watu.
Wahusika wengine ni: Zitto, Leila, Josephine, Pamela, na Mwema
Mandhari
Riwaya hii imetumia mandhari ya mjini. Matukio mengi yanafanyika mjini. Huko ndiko kuna rushwa, biashara ya ukahaba, maisha ya kubahatisha na visa vya kila namna.
Matumizi ya lugha
Misemo
Asiye na bahati habahatishi
Tandu kwenda mbele na nyuma ndiyo hulka yake
Asiyezika hazikwi
Mmetupa jongoo na mtiwe
Methali
Asilolijua mtu ni usiku wa giza
Ukiona mwenzio ananyolewa tia maji
Mtaka waridi sharti avumilie miiba
Biashara haigombi
Matumizi ya lugha nyingine
Kiingereza
Mission to Seamen please
Hey man you will pay extra dollars
Kiarabu
Inna lillahi wa inna ilahi rajiunna!
Tamathali za semi
Tashbiha
Zepher 6 ile iliunguruma kama samba aliyeghadhibishwa (uk. 9)
Wote walikimbilia kule wakiminyana kufa au kupona kama kaa wanavyogombea mavi ya mvuvi(uk. 21)
Maduka makubwa yalichipua mithili ya uyoga
Miguu yake ilikazana mithili ya upinde uliotaka kufyatuliwa
Tashihisi
Utumbo ulimlaumu
Mvua ikarindima kwa kiburi na kuviadhibu vibati vibovu
Lakini hata fikra nazo zilikuwa kama zimempiga chenga
Sitiari
Sote kobe
Sarahange wetu mbogo kweli siku hizi
Mbinu nyingine za kisanaa
Onomatopea/tanakali sauti
Saa mezani iliendelea kugonga ” ta ta ta”
Akazungusha ufunguo wa gari lake na kutaka kuliwasha lakini ikatokea sauti kali fupi “ta nye nye”
Takriri
Funga ,shinda! Funga,shinda! Sauti za mashabiki zikarindima tena
Shinda! Shinda! Shinda! Kibanda kilitetemeka tena
Shetani! Oyee! Shetani! Oyee! Shetani chinja!
