Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta | Sehemu ya 10

Komandoo Mako gizani

Nkuu wa Nkoa kaja kwa ku shtukiza… patachimbika humu ndani nakwambia, atatumbuliwa ntu baada ya ntu,” alisema bibi mwingine aliyekuwa anamuuguza mjukuu wake.

“Unapiga simu wapi?” nilimfokea nesi ambaye alionekana kupiga simu kuwaita wakubwa wake. “Usipige simu, usimuite yeyote, hapa nimekuja kwa kushtukiza na nitaingia kila wodi kwa kushtukiza.”

“Sawa mkuu,” walijibu watumishi wale wa afya. Wagonjwa wakatabasamu.

“Sasa sikiliza,” niliendelea. “Wagonjwa watibiwe, pesa italipwa baada ya matibabu, tuhakikishe tunaokoa uhai kwa gharama yoyote. Pesa zipo tu na haziwezi kamwe kufanana na thamani ya uhai wa mwanadamu.”

“Ndiyo mkuu,” walijibu.

“Natoka humu katika ziara yangu hii ya kushtukiza, msipige makelele wala msinifuate, pia msipigiane simu, nakwenda kwenye jengo lile wodi ya wazazi, nawatakia utekelezaji mwema.”

Nilitoka katika wodi ile na kuanza kuelekea wodi ya wazazi. Nilikuwa na hofu kwamba, watu wangeongezeka zaidi, lazima ningegundulika kuwa mimi siyo mkuu wa mkoa. Hii ingekuwa kesi kubwa tena ya aibu. Vilevile sikuwa nimepanga kuwa nitambulike hivyo, ni watu niliowakuta wodini ndiyo walinipachika cheo hicho.

Nilitembea haraka nikazipandisha ngazi za jengo la wodi ya wazazi. Nilikuwa napiga jicho nyuma kwa kuibia, kumbe maelekezo yangu hayakufuatwa, kuna manesi walishapiga simu na nyuma kiasi cha hatua mia mbili, niliona watu wengi wakija nilipo, niliweza kuwatambua watu hao, mmoja wao alikuwa Daktari mkuu wa hospitali hiyo. Alikuwa anakuja nilipo akiongozana na madaktari wengine watano na askari watatu.

Sasa niliiona hatari iliyokuwa inaninyemelea. Daktari mkuu na wenzake wote wasingeshindwa kutambua kuwa mimi sikuwa mkuu wa mkoa hata kama mkuu mpya wa mkoa hakuwa ameanza kuonekana katika Luninga. Wazee hawa wanawafahamu viongozi wote kwani ni jamaa zao.

Nilitembea haraka nikalifikia jengo la wazazi na sasa nilikuwa ndani ya jengo hilo lililo juu kimo cha ghorofa moja. Niliwaacha mbali watu wale lakini nao walikuwa wakija kwa kasi zaidi. Niliingia wodini kama ninaye salimia watu. Jengo hili lina upande wa kushoto na kulia, mimi nilielekea kulia, nikatembea mpaka mwisho na bahati njema, mapokezi hapakuwa na daktari wala nesi na wodi nzima ilikuwa na mgojwa mmoja tu aliyekuwa anaongezwa damu na alilala usingizi.

Nilifungua dirisha kubwa la vioo kisha nikatoka kwa kushuka taratibu, nilipoona kimo cha chini ni kidogo, nilijitupa kikomandoo, kisha kwa kuinama, nikakimbia mpaka ulipo ukuta, nikauparamia kama mjusi na kuukwea mpaka kilele chake, halafu ‘puuu’, nilikuwa nje ya hospitali. Huko nyuma sikujali kama kuna mtu aliniona au hakuniona.

Soma: Mwanamke Uliyekula Pesa Zangu Nakutafuta |Sehemu ya 11


Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne