Mfalme Anataka Kuniua | Sehemu ya 10

 

Taji la Mfalme

Mako alitembea taratibu mpaka aliposimama askari. Umbali wa askari mmoja na mwingine ulikuwa hatua hamsini na tano. Alipomfikia, alimsabahi.

“Hujambo Ai.”

“Sijambo Mako, pole,” alijibu askari, kisha akaendelea, “umefuata nini hapa, huruhusiwi kuwa eneo hili, nikuchome singe?”

“Ni bora kufa kwa kuchomwa singe kuliko kunyongwa bila hatia. Sikiliza Ai, nipo hapa kwa sababu nataka unisaidie. Nisaidie kuchelewa kupiga filimbi.”

“Mako, unataka nikusaidie kutoroka?”

“Kutoroka nitatoroka mwenyewe, nisaidie kuchelewa kupiga filimbi. Usipige filimbi mpaka nitakapozama mtoni.”

Ai ni binti yatima, wazazi wake walifariki kwa ajali ya mtumbwi alipokuwa na umri wa miaka kumi na nne. Hakuzaliwa mjini Kanakantale, alizaliwa kijijini Kanakado, hata hivyo baada ya kupoteza wazazi, alichukuliwa na dada yake mpaka hapo Kanakantale.

Alipofika Kanakantale, maisha ya dada yake yalikuwa magumu tena ya ufukara wa kutisha. Yeye na dada yake walifanya kazi ya kuuza matunda kandokando ya barabara za mji.

Siku moja Mako akipita mjini, alimuona binti mrefu mweupe akiuza matunda. Alimfuata na kumuuliza mambo mengi. Mwisho alibaini mtoto yule alipenda sana elimu ila hakupata nafasi. Basi Mako akachukua jukumu la kumsomesha Ai mpaka leo hii ni askari katika gereza la Kanakantale.

Basi Mako alimtazama Ai usoni, akabaini Ai asingeweza kumsaliti, akakimbia kwa kasi mpaka ulipo uzio wa gereza, kisha akapanda kwa nguvu na kuruka upande wa pili. Baada ya hapo akakimbia kwa kasi kama roketi, mpaka mtoni, kikasikika kishindo cha mwanaume, ‘chubwii’.

Kuona hivyo, Ai akapiga filimbi, ‘pyeeeeeee!’

“Mako ametorokaaaaaah!” alitamka kwa sauti askari mwanamke. Askari wengi, waume kwa wake wakasogea tayari kuanza msako.

Msako wa mfungwa aliyetoroka ulianza. Ai alikuwa na wakuu wake akijaribu kueleza ilivyokuwa. Alieleza katika hali ya kushangaza, mfungwa huyo alimfuata akimuomba msaada wa kupatiwa huduma ya matibabu kwani alidai anaumwa. Lakini ghafla mfungwa alikimbia, akaruka ukuta na kuelekea mtoni.

Vikosi vya askari wakiongozwa na mbwa wakali, viliingia msituni. Wengine walipanda mitumbwi na kuelea mtoni wakimsaka Mako.

Jioni hiyohiyo katika nchi ya Kanakantale, ilitangazwa yeyote atakayesaidia kupatikana kwake, angezawadia ng’ombe elfu moja. Zoezi la kumtafuta likawa siyo la askari pekee, likawa la watu wote. Kila mmoja akitamani kuukimbia umasikini kwa kutoa taarifa za mtu huyo aliyetoroka jela.

Mashujaa wa vita wakaingia kila eneo kumsaka. Mako alitafutwa na jamii nzima!

Mako aliibuka katika maji, akatembea kwa tahadhari mpaka katika kichaka akajificha. Alikaa hapo mpaka giza nene lilipotanda. Alianza kutembea kuelekea alikokujua yeye. Alitembea kandokando ya barabara lakini palipokuwa na miti ili asionekane. Mako alijua kuficha umbo!

Wakati akiendelea kutembea tena aliyeloa chapachapa, aliona picha kubwa katika mti mmojawapo, ilikuwa picha yake na iliandikwa maneno, YEYOTE ATAKAYESAIDIA KUKAMATWA KWA MAKO, ATAZAWADIWA NG’OMBE ELFU MOJA. Haraka alilichukua tangazo hilo na kulichana. Hata hivyo, asingeweza kuyachana mabango yote ambayo mpaka muda huo yalienea nchi nzima.

Ghafla mbele yake aliona kundi kubwa la askari wakija na mienge ya moto. Akadondoka chini kama furushi kisha akatambaa mithili ya nyoka mpaka katika mtalo mkubwa. Askari waliendelea kuja wakiwa na mbwa wao. Kadri walivyozidi kusogea alipojificha Mako, ndivyo mbwa wale walivyozidi kubweka kwa sauti. “Woooh! Wooooh! Woooh!”

Huu ni Mwisho wa Sehemu ya bure ya Riwaya hii, Isome Riwaya yote ili kufahamu kilichotokea kwa Tsh. 2,000/= tu. Gusa Hapa Kununua Riwaya yote.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne