Njia Nne Zitumikazo Kuunda Misimu ya Lugha ya Kiswahili

Kitu Kinaundwa

Niliketi katika kiti kirefu nikinywa kinywaji ambacho siwezi kukitaja. Katika kiota nilichokuwamo, mhudumu alikaa mbele yangu sehemu iitwayo ‘kaunta’ nasi tulitenganishwa na dirisha kubwa lililokuwa na nondo pana.

“Mwanaidi ongeza kinywaji,” nilisema kwa sauti kali, nilijiamini kwa sababu katika kiota hiki, tulikuwa wawili tu, mimi na Mwanaidi. Kiota cha Mwanaidi hakina wateja wengi na leo nilikuwa peke yangu.

Aliongeza kinywaji kama nilivyotaka, kisha akabadili wimbo na kuweka dansa moja matata. Nilitaka kuinuka ili nisakate dansa, lakini nikajizuia baada ya kukumbuka kuwa mimi ni mwalimu, tena siyo mwalimu wa kawaida, ni mwalimu wa walimu na wanafunzi. Basi nikakaa tuli nikitikisa kichwa na mabega.

Lakini ghafla tukavamiwa na watu watatu. Watu hawa walivaa sare za jeshi la polisi. Bila shaka, walikuwa polisi.

“Kwa nini unafungua biashara yako mpaka saa saba usiku tena ukipiga mziki kwa sauti ya juu?” aliuliza askari aliyekuwa na mbavu nene kuliko wenzake. Mwanaidi hakuwa na cha kujibu. Askari akanigeukia mimi.

“Na wewe ndiyo mteja wake, leo mnaenda kurara polisi. Haya ndiyo majambazi afande!”

“Mimi siyo jambazi afande, mimi ni mwalimu,” nilijitetea.

“Mwalimu wa somo gani?” askari aliyekuwa kimya muda wote aliuliza.

“Kiswahili na masomo mengine ya sanaa,” nilijibu. Baada ya jibu hilo, alisogea karibu yangu zaidi kisha akaniuliza swali lililonifanya nikaandika habari hii.

“Unaelewa nini kuhusu neno misimu? Kwa kutumia mifano, fafanua njia nne zitumikazo kuunda misimu ya lugha ya Kiswahili.”

Bila kupepesa macho, nilimjibu swali lake kwa hoja zifuatazo:

Njia Nne za Kuunda Misimu

Misimu ni semi za muda na mahali maalum ambazo huzuka na kutoweka kutegemea mazingira maalumu. Njia nne zitumikazo kuunda misimu ya lugha ya Kiswahili ni:

1.   Kufupisha maneno

Mfano, neno refu kama kompyuta, kufupishwa na kuwa komp.

2.   Kutohoa

Misimu huweza kuundwa kwa kutohoa kutoka lugha za kigeni. Mfano, mother-maza.

3.   Kutumia sitiari

Mfano, Golikipa-nyani. Mtu mwenye nguvu-simba.

4.   Kutumia tanakali

Mwigo wa sauti ya kitu, hutumika kama jina la kitu hicho. Mfano, bunduki-mtutu.

Hizo ndizo njia zitumikazo kuunda misimu ya lugha ya Kiswahili.

Baada ya majibu hayo, askari walituacha lakini wakimshauri hasa Mwanaidi kuwa, atii sheria bila shuruti. Kila ifikapo saa sita usiku, afunge kiota chake.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne