Jinsi ya Kuzuia Kusinzia Darasani Mwalimu Anapofundisha
Kabla
mwalimu hajaingia darasani, unakuwa na nguvu za kutosha na unazungumza na
wanafunzi wenzako. Mwalimu anapoingia, hali inabadilika, kadri anavyoongea na
wewe ndiyo usingizi unazidi kukolea. Badala ya kuelewa kipindi, unaishia
kusinzia. Sasa mwalimu katoka na usingizi nao haupo. Ni kama umerogwa eeeh? Hapana,
hujarogwa hilo ni tatizo la kawaida na karibia kila mwanafunzi hukutana nalo. Tatizo
la kusinzia darasani.
Kusinzia
darasani kunaweza kukufanya uyachukie masomo na mwisho wake upate matokeo
mabaya ya darasani kwani kile ulichotakiwa kukielewa hutakielewa kwa sababu ya
kukosa usikivu. Tatizo hili linahitaji tiba, na zifuatazo ni njia za kufanya
ili kuzuia kusinzia darasani.
1.
Pangilia
vizuri muda wako wa kulala
Lala
muda unaofanana na amka muda unaofanana kila siku hata katika siku za mwisho wa
wiki. Kwa mfano, kama unalala saa sita usiku na kuamka saa moja asubuhi, fanya
hivyo siku zote. Muda wa kulala ni saa nane, hata hivyo kama ratiba yako ni
ngumu, bado ni sahihi kulala saa sita au saba. Hakikisha unalala kwa angalau
saa sita kwa siku, chini ya hapo ni hatari kwa afya yako na utaendelea kusinzia
darasani.
2.
Lala
kidogo mchana
Baada
ya kutoka darasani, lala kidogo kwa muda wa dakika 30. Hii itakuepusha kupata
usingizi utakapokuwa darasani.
3.
Fanya
mazoezi
Fanya
mazoezi ya kawaida ili kuchangamsha mwili wako. Wanafunzi wangu wenye tatizo la
kusinzia darasani huwa nawashauri wafanye mazoezi haya: kukimbia, kuruka kamba,
na ‘push up’.
4.
Punguza
kazi nyingi
Ni lazima
kufanya kazi, lakini kazi nyingi zitakufanya mchovu na mwili utahitaji
kupumzika na hapo ndipo usingizi unapovamia. Hivyo punguza mambo mengi. Zile safari
za kumfuata msichana au kaka yule ndiyo chanzo cha uchovu unaokufanya usinzie
darasani.
5.
Usile
kupita kiasi muda mfupi kabla ya kulala
Mwanafunzi
wangu mmoja aliyekuwa na tatizo la kusinzia darasani, nilimshauri mambo manne
hapo juu bila mafanikio, ndipo nilipokuja kugundua kuwa, kumbe mwanafunzi huyu,
hula ugali mkubwa na maharage ndipo analala usiku. Jambo hili siyo jema, linachosha mwili na kesho utasinzia darasani.
Haikatazwi
kula muda mfupi kabla ya kulala, lakini kula kidogo na kaa angalau kwa saa moja
kabla hujalala.
Kama
una tatizo la kusinzia darasani, jaribu mambo hayo matano, natumaini utapata
matokeo mazuri na utafurahia masomo.