Uhakiki wa Diwani ya Mashairi ya Chekacheka

Uhakiki wa Diwani ya Mashairi ya Chekacheka
Mwandishi; Theobard Mvungi
Wachapishaji; EP & D.LTD
Mhakiki; Mwalimu Makoba

Maudhui

Dhamira

1. Kutetea Haki

Mshairi anamshauri kiongozi wa nchi aendelee kuwasha moto dhidi ya watu wote wanaodhulumu haki za wengine. Katika shairi la MWINYI UMEWASHA MOTO ANGALIA USIZIMWE, mshairi anasema,

“Tumaini la wanyonge, kwamba ipo serikali,
Ile nchi ya mazonge, ya wenye meno makali,
Wanyang'anyao matonge, wanyonge hawana hali,
Mwinyi ukiwa mkali, ndio raha ya raia.”

2. Demokrasia

Mshairi anapinga mfumo wa chama kimoja. Kwake yeye, mfumo huu, unawanyima watu uhuru wa kutoa maoni yao na kukosoa pale mapungufu yanapojitokea. Shairi hili liitwalo TAIFA WAMELIZIKA liliandikwa kipindi ambacho Tanzania ilikuwa katika mfumo wa chama kimoja. Hata hivyo bado lina uhalisia hasa ukizingatia uminywaji wa demokrasia na uhuru wa vyama vya upinzani leo hii. Mshairi anasema,
“Mezikwa demokrasi, Chama kimoja ndo' ngao
Watu hawana nafasi, kutetea nchi yao
Mawazo ya ukakasi, mawazo ya mtitio…”

3. Mapenzi

Mshairi anaeleza jinsi mapenzi yanavyoweza kumtesa mtu hasa pale unayempenda anaposhindwa kukuelewa. Katika shairi la NJIWA KIUMBE MTINI mshairi anasema,

“Nimejaribu kuongea, ndege awe mkononi,
Yeye juu hurukia, namuomba samahani,
Nyimbo ananiimbia, nyimbo zachoma moyoni,
Basi mie taabani, njiwa akitabasamu.”

4. Uhusiano wa Kimataifa

Katika shairi la INDIRA, mshairi anaomboleza kifo cha mpigania uhuru wa nchi hiyo-Indira. Shairi hili linaonyesha jinsi tulivyo na ushirikiano na nchi nyingine. Mshairi anasema,

“Wengi tumesononeka,
Oktoba kututoka,
Umeondoka haraka,
Kwa kweli ulitukuka.”

5. Ukasuku

Ukasuku ni kitendo cha kurudiarudia yale yaliyokwisha semwa. Pia, ni kuandika jambo bila kutafakari sana. Hapa mshairi anawashauri waandishi wasiwe makasuku. Anasema,

Kadhalika tafakari, Mshairi uwe nyati,
Laghai usiwakiri, wasikura kwa nyati,
Ati ukweli ni shari, uwapigie magoti,
Kataa hotuba tupu, Kandamiza la jamii.

Ujumbe

1. Viongozi watetee haki za raia wao.
2. Waandishi waepuke ukasuku bali waandike mambo yatakayosaidia ujenzi wa jamii mpya.
3. Vyama vya upinzani vipewe nafasi ili kuleta changamoto zitakazochochea maendeleo.
4. Tanzani iendelee kushirikiana na nchi nyingine kwani umoja ni nguvu.

Falsafa

Mwandishi anaamini kuwa, tukiungana pamoja tutawezesha ujenzi wa jamii mpya.

Msimamo

Mshairi ana msimamo wa kimapinduzi, matatizo yaliyopo katika jamii, anaamini yataondolewa endapo watu wataamua kuungana pamoja.

Fani

Matumizi ya lugha

Tamathali za semi

i. Tashibiha

Moyo kiburi hatari mfanowe kama radi (uk. 13)

ii. Tashihisi

Moyo jifunze busara, iwe ndiyo yako taa

iii. Sitiari

Kadhalika tafakari, mshairi uwe nyati

Ujenzi wa Taswira

- Taswira Zionekanazo

Kwa upande huu wa taswira, tuna mifano michache. Angalia shairi la 'Tuambae Ukasuku' (uk. 3) lilivyojenga taswira zake. Tutatumia beti zifuatazo:

Hakuna athubutuye, ati nyati kumtuma
Aibebe niizigoye, au chuchu kumkama
Na sogi amjaziye, ampandishe kilima
Nyati si mkubalifu, mfugaji atazikwa.
Kadhalika tafakari, mshairi uwe nyati
Ati ukweli ni shari, uwapigie magoti
Mshairi jihadhari, usishikwe kama funbo
Usiwe kama kunguru, woga umejaa tumbo (uk. 3)

Katika mistari hiyo iliyodondolewa, tunaweza kuziona taswira muhimu za kimaumbile zinazojitokeza. Kwanza, tunaiona taswira ama picha ya nyati mkali ambayo 'mtu' hathubutu kumtuma mtu. Kuwa na ukali kama wa nyati si jambo la mchezo, ni la hatari. Tunaweza kuuona ukali wa nyati anayekamuliwa chuchu. Ni jambo la hatari.

Taswira za Hisi

Taswira za aina hii si nyingi katika diwani hii, lakini ni muhimu kuzitaja pia. Katika shairi lake la 'Kuna Nini Huko Ndani' (uk. 4) tunaisikia sauti ya mshairi ikisema na kugundua harufu za kunukia. Kunukia huku kunaleta athari za hisia kali zinazosababisha mtu kuwa na tamaa kali zaidi. Mshairi anasema:

Kuna nini huko ndani, mbona jiko lanukia?
Rihi yajaa puani, na muda wajiendea
Kisoiva kitu gani, inbona mate mwalutoa.
Naona mwajigawia, mwapishi ninawahofu (uk. 4)

Taswira za Mawazoni

Taswira nyingine ni za mawazoni tu. Kwa mfanu, mshairi anatuletea shairi lake moja ambalo anaongea na 'kimoyo' (uk. 12) chake. Anasema kwa mfano:

Wewe kimoyo sikia, mbona unanipa tabu?
Si mimi wanionea, kwamba wewe yakusibu
Ni pole nakuainbia, pole sina matibabu
Kimoyo, sinilaumu, uwezo umekuwa haba (uk. 12)
Ingawa tunajua kuwa kila mtu ana moyo, lakini mtu kuzungumza na moyo ni jambo la mawazoni tu. Linaathiri maisha ya mtu kwa kuzingatia kweli kwamba mtu huyo ana mgogoro na nafsi yake!

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne