Riwaya| Sitasahau Nilipolala na Mwanamke Juu ya Kaburi (24)
Wakati naendelea kushangaa, alinipiga
na yale manyoya ya bundi utosini. Nikapoteza fahamu.
Niligutuka nikiwa katikati ya
msitu mnene. Ilikuwa asubuhi. Kabla sijafanya lolote, nikasikia sauti kali,
“Upo katika nchi ya Matumbawe!” niliitambua sauti ile. Ilikuwa sauti ya Mzee.
Sauti iliyojaa kitetemeshi!
Matumbawe yaliyosemwa sikuyaona.
Niliona msitu mnene hata nikahofia kama nitapata njia ya kupita. Nilijizoa
taratibu nikasimama. Nikawaza nielekee wapi, nikaamua kuelekea mashariki.
Sikujua nilikokwenda, ila
nilitambua kilichonifikisha hapo ni msako wa mjuu wa Mzee Samike, Chimota.
Nilitembea hovyo kama nyumbu aliyeridhika na unyumbu wake katika msitu wa
ujinga. Hakukuwa na njia, maana yake ni kwamba, mahali hapo hakuwahi kupita
mwanadamu.
Nilitembea kwa mwendo mrefu, jua
lilikuwa kali lakini halikunichoma kwa sababu ya wingi wa miti. Muda wote
nilikuwa chini ya kivuli nikivuta hewa safi katika nchi hii ya Matumbawe.
Safari yangu ilichukua masaa
mengi hata jua likazama na kuifanya dunia ipoteze nuru. Hapo nikawaza
nitawezaje kuwa katika msitu mnene peke yangu? Vipi kama nitapatwa na madhara?
Vipi nikishambuliwa na wanyama wakali. Sikupata jibu na sikuwa na namna
nyingine isipokuwa kulala chini ya miti ili kukikucha niendelee na safari.
Nilikuwa mpweke nikijipa moyo kuwa Samike angenisaidia muda wowote
nitakapopatwa na tatizo.
Kuna jambo lilinishangaza, japo
nilitembea kwa zaidi ya masaa 12, sikuhisi njaa, sikuhisi kiu, tumbo langu
lilikuwa limejaa vyema. Nilishangazwa na uwezo huu mpya.
Nilikaa chini ya mti mkubwa. Giza
lilikwisha tanda nami sikuwa na uwezo wa kuendelea na safari. Kitendo cha
kukaa, kiliamsha jambo jingine. Usingizi mnono ulinivamia nikalala bila kuota.
Niliamshwa asubuhi na ndege mmoja
mdogo mwenye mseto wa manyoya mekundu na meupe. Alinidonoa donoa miguu mpaka
nikaamka. Nilimtazama rafiki huyu mpya nikitabasamu. Naye alijibu kwa kupiga
kelele za furaha, “Jiuuuh! Jiuuuuh! Jiuuuuh!”
Sikuwa na muda wa kupoteza,
nilifuta vumbi suruali yangu ambayo hapo zamani katika upya wake ilikuwa
nyeupe, lakini sasa haikuwa na rangi iliyoeleweka kutokana na kuvaliwa mara kwa
mara.
Nilitembea mwendo wa kawaida kwa
sababu nilikokwenda sikupajua na sikuwa na haraka. Kuna wakati mbele yangu
niliona simba, nikabadili njia ili nisigeuzwe kitoweo. Nikaendelea kutembea kwa
kujiamini kama nilikuwa mmiliki wa msitu ule na vyote vilivyomo.
Huku nikiendelea kutembea, ndege
mdogo aliyeniamsha aliruka juu akinifuata. Nadhani kwa sababu ya umri wake
mdogo hakuijua siri ya dunia kuwa maisha yamejaa uhasama na kuwindana. Masikini
alidhani kila kiumbe ni rafiki. Hata hivyo alikuwa katika mikono salama. Mimi
nilitembea, yeye akapaa juu yangu.
Wakati nikiendelea kutembea,
nilisikia ngurumo mbele yangu. Hata yule ndege aliogopa akaruka mbali nisiweze kumwona. Ngurumo zile zilikatika,
nikaona kitu cha kuogofya.
Lilisimama joka kubwa sana mbele
yangu. Niligeuka nyuma haraka ili nikimbie, nyuma yangu napo palisimama joka
kubwa kama lile la mbele. Nikajaribu kupenya kushoto, njia haiupitika, palikuwa
na mti mkubwa wa mbuyu. Kulia nako vivyo hivyo, hapakupitika kwa sababu ya mti
mnene uliojaa miba mikali.
Basi nikawa nimesimama katikati
ya majoka yale makubwa yaliyojaa hasira nisiyejua la kufanya.
Wakati nikiendelea kushangaa kwa
hofu, joka la mbele lilifungua kinywa chake likatema moto. Joka la nyuma nalo
likajibu mashambulizi. Sikuwa na ujanja tena. Nikakaa chini kusubiri hukumu
yangu. Nilikiona kifo kibaya kabisa kikininyemelea, kifo cha kumezwa na majoka
mawili yanayotema moto!
Itaendelea Jumapili…
“Si ruhusa kuchukua hadithi hii na kuiweka katika mfumo wa sauti, kutoa kitabu, kuweka katika blogu au ‘website’ nyingine, au kufanya chochote kile bila kuwasiliana na mmiliki! Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka!”
Daud Makoba 0754 89 53 21
Shusha maoni yako mdau!