Riwaya| Sitasahau Nilipolala na Mwanamke Juu ya Kaburi (23)

sitasahau nilipolala na mwanamke juu ya kaburi

Wimbi lile lilituzoa na kutupeperusha juujuu kabla halijatushusha na kutufanya tupige ukelele wa katikati ya hofu na mashaka. Ukelele wetu ulikatwa na sauti kali iliyotuamuru tunyooshe mikono juu. Aliyesema hayo alisimama upande wa kulia, ndipo tulipogundua tulikuwa karibu na meli kubwa ya mizigo iliyokuwa ikienda nchini kwetu.
Tulitii amri tukanyoosha mikono juu kama mateka wa kivita. Kamba kubwa ikarushwa na kuunasa mtumbwi wetu na kuanza kuvutwa kuelekea iliko meli. Tulifika karibu na meli hiyo tukapatiwa ngazi huku tukiamriwa tupande juu. Tulipanda bila kupinga.
Tulipofika juu mimi na mzee, tulishuhudia watu wengi ambao walibeba silaha za moto. Bila shaka watu hawa walikuwa ni askari binafsi waliofanya kazi ya kulinda meli dhidi ya maharamia. Nilimnong’oneza mzee, “Mzee tumefananishwa na maharamia!” naye akazungumza na watu wale kwa sauti:
“We are not Somalis,” nilishangaa kumsikia mzee akibonga Kiingereza.
Niliweza kuwatambua walinzi wale kuwa ni raia wa Marekani kutokana na bendera zilizokaa juu ya  mikono ya magwanda yao. Hawakujishughulisha na kumjibu mzee, bali kijana mmoja alitusogelea na kutukagua kama tulibeba siraha yoyote. Hakupata alichokitafuta.
“They are not!” alisikika kijana aliyetukagua akiwaambia wenzake. Walipojiridhisha wakatuamuru tushuke chini mpaka kwenye mtumbwi ili twende zetu.


Tulifika chini ya mtumbwi tukakaa taratibu tayari kwa kupiga kasia. Mzee hakuwaacha salama, akapasua yai kwa sauti kuu, “Hey fuc*, ur lucky today im in a good mood, if not I was going to destroy this fuc*ed ship with my own hand.” Hawakuyajali maneno ya mzee wala kutetemeshwa naye, waliendelea na hamsini zao nasi tukaendelea na sabini zetu.
XX    XX    XX
Niliishi na mzee kwa amani na furaha. Taratibu akaanza kunifundisha fani mpya. Haukuwa ulozi, ila alinifundisha fani ya kupambana na walozi. Tulitumia muda wetu kwa kuvua samaki na kufundishana fani hii. Kila mahali palikuwa ni darasa. Tulipokuwa baharini katika kina kirefu alinifundisha mengi hata nikawa na uwezo wa kuwaita samaki niwatakao wakanifuata. Somo hili lilinifanya niigundue siri ya mzee kuvua bila nyavu.
Ni kweli katika mtumbwi tulikuwa tukiondoka na nyavu, lakini hatukuwahi kuzishusha kamwe. Mzee alinionya niitunze siri hii. Akanieleza siri hii ndiyo humanya apende kuvua katika eneo la peke yake ambako wavuvi wenzake huwa hawafiki. Eneo alilopenda kuvua mzee ndipo zilipopita zile meli kubwa kubwa za mizigo zilizojaa walinzi tele.
Tulipokuwa nchi kavu alinifundisha aina za miti na matumizi yake. Hakuisha kuniambia aina hii ya mti inatibu hiki, hii inatibu kile. Wakati mwingine akisisitiza, ukitaka mchawi asiingie kwako, weka mzizi wa mti wa mzaituni pembezoni mwa chumba, hataweza. Basi nilipewa elimu ninayoizungumza hapa na nyingine ambayo sitaweza kuisema. Yote hii alifanya kuniandaa kwa mapambano makali ambayo bila shaka yalikuwa karibuni kuanza.


Siku moja usiku saa nne, nikiwa nimekaa na mzee pembezoni mwa kijinga cha moto tukipiga soga za maisha. Alitua bundi mkubwa mkononi kwa mzee. Mzee alimtoa manyoya ya kichwa kisha akamwacha aende zake.
“Wakati umefika Mako!” alisema akinikazia jicho. Nilibaki nikimtazama nikiwa sielewi ni wakati gani hasa mzee alimaanisha.
“Wakati wa kumkomboa mkombozi umefika Mako!” aliendelea kuzungumza akizidi kunichanganya kabisa.
“Mako! Itakapofika saa nane na nusu usiku, utasafiri kwenda nchi ya Matumbawe kumtafuta Chimota.” Mzee alisema, nikayaona macho yake yaking’aa isivyokawaida. Niliogopa kwa sababu nilikuwa bado sijafanya maandalizi ya kupambana na wachawi waliobobea, katika eneo ambalo hata sikulifahamu.
Itaendelea Jumapili…
“Si ruhusa kuchukua hadithi hii na kuiweka katika mfumo wa sauti, kutoa kitabu, kuweka katika blogu au ‘website’ nyingine, au kufanya chochote kile bila kuwasiliana na mmiliki! Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka!”
Daud Makoba 0754 89 53 21
Shusha maoni yako mdau!


Tazama Povu la Mwalimu Makoba kwa Wasanii Wavaa Hovyo

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne