Chimbuko la Fasihi na Sanaa, Mtazamo wa Kiyakinifu na Kidhanifu
Mitazamo miwili inaeleza kuhusu
chimbuko la fasihi: Wa kwanza ni ule wa kidhanifu na wa pili ni mtazamo wa
kiyakinifu.
Mtazamo wa Kidhanifu
Mtazamo huu hoja zake zimo katika
kudhani tu na kamwe hoja hizo haziwezi kuthibitika kisayansi.
Mtazamo huu unaeleza kwamba,
fasihi hutoka kwa Mungu na mwanadamu huipokea fasihi kutoka kwa Mungu huyo.
Wataalamu ambao maandiko yao
yanakubaliana na mtazamo huu miongoni mwao ni F. Nkwera na John Ramadhani.
Mfano Nkwera anakubaliana na
nadharia hii kwa kusema: “Matengenezo ya sanaa huonekana kuwa ni shughuli ya
kiungu yenye kumwiga Mungu ambaye ndiye msanii wa kwanza.”
Ukiuchunguza kwa undani mtazamo
huu unaelekea kuamini kuwa, mwanadamu hahusiki katika utengenezaji wa fasihi,
bali hupewa fasihi hiyo ikiwa tayari imetengenezwa. Haya ni mawazo yaliyochakaa
na yanayoibua maswali mengi kuliko majibu.
Pia, mtazamo huu unamtenga msanii
na jamii yake na kumpa uwezo mkubwa mno wa kuwa karibu na Mungu kuliko watu
wengine wa kawaida.
Mtazamo huu umewaathiri zaidi
waandishi wengi wa mashairi. Mara nyingi katika beti zao huanza kwa kumshukuru
Mungu kwa kuwapa uwezo wa kuandika na humaliza kwa kumshukuru Mungu tena kwa
kuwajaalia uwezo huo wa kuzipanga beti zikasomeka.
Mtazamo wa kiyakinifu
Mtazamo huu unakuja na hoja
ambazo angalau zinaweza kuthibitika kisayansi. Unaeleza kuwa, chanzo cha fasihi
ni mwanadamu mwenyewe na mazingira yake.
Hadithi, methali, vitendawili,
nyimbo, tenzi, majigambo, mafumbo n.k vilitungwa na kusimuliwa kwa lengo la
kufunza, kukosoa, kuadibu, kuamsha fikra, na kuiburudisha jamii baada ya kazi
ili kuipunguzia uchovu.
Sanaa hii ilirithishwa kutoka
kizazi hadi kizazi kwa njia ya masimulizi. Baadaye mwanadamu kaendelea sana
kiteknolojia na ameweza kuhifadhi na kusambaza fasihi kwa njia za haraka zaidi.
Njia zinazotumika leo hii ni: kanda za kunasia sauti, kanda za video, runinga,
kompyuta na intanenti. Hivyo hoja ya kuwa chanzo cha fasihi ni mwanadamu
mwenyewe inakubalika.
Marejeo:
Nkwera, F. (1978) Sarufi na Fasihi
Sekondari na Vyuo. TPH: Dar es Salaam.
J.A Masebo & N. Nyangwine.
(2007). Fasihi kwa Ujumla: Nadharia ya
Fasihi. Nyambari Nyangwine Publishers: Dar es Salaam.