SAFARI YA KUUSAKA MWEZI (sehemu ya nane)
Looh! Sikuamini, niliiona Mapandagila 214 ikiwa
imeegeshwa mbali kidogo, niliruka kwa furaha nikamkumbatia Chokusi,
akanikwaruza ubavuni kwa vile vyuma vyake, sikuhisi maumivu. Lakini tena
nikakumbuka jambo, nikauliza.
“Lakini
nilipodondoka iliharibika kabisa… nitawezaje kupaa tena?”
“Niliitengeneza…
kwa sasa iko vizuri na itakufikisha salama huko uendako.”
Nilimkumbatia tena kwa furaha, lakini kabla
sijamwachia, akanipiga mweleka, wote tukalala chini.
“Askari
wanakuja na makombora, wamekwishagundua kuwa umetoroka, tambaa mpaka katika
ndege yako, usinyanyue kichwa wala kugeuka nyuma, kwa heri.
Chokusi alirudi katika shimo haraka, mimi nilitambaa
kama nyoka kuelekea ilipokuwa Mapandagila 214, nikayasikia makombora mazito
yakirushwa, nikakaza mwendo.
Kombora moja lilinikosa mguuni, nikajivuta kushoto,
nikatazama juu, ndege nyingi ziliranda… nilikwishaonekana, sikuwa na ujanja,
nikajivuta mpaka katika jiwe kubwa nikaegama huku nikipiga hesabu za kuifikia
Mapandagila 214 bila kuguswa na makombora yale.
Nikiwa nimeegama katika jiwe hatua chache kuifikia
Mapandagila, kombora kubwa lilirushwa, Mapandagila 214 ikasambaratishwa
vipandevipande. Nililia kwa uchungu wa
kukipoteza chombo hiki kilichokuwa fahari ya nchi yangu, chombo kilichotumia
pesa nyingi na maarifa kukitengeneza kilisambaratishwa maramoja bila huruma.
Sikujua ni vipi ningetoka salama katika mikono ya adui.
Ndege za adui zilitua, wanajeshi wengi wakashuka na
kuanza kuja mahali nilipokuwa, ujanja wangu wote ulibaki mfukoni.
Lakini ghafla, makombora mazito yalirushwa na
kuzisambaratisha ndege za adui, kisha chuma kizito kikashushwa, kikawavuta wale
watu wa chuma na kuwanasa kama gundi. Niligundua baadae kuwa chuma kile ilikuwa
sumaku yenye nguvu sana.
Nilipepesa macho, nikakiona chombo cha masafa ya anga
kikitua, ubavuni kiliandikwa MAPANDAGILA 428. Nilitabasamu kwa furaha kwani
niligundua chombo kile kilitoka Duniani na bila shaka kilikuja kuniokoa.
Baada ya chombo kile kutua, mlango ulifunguliwa
akatoka msichana mdogo mrembo aliyevalia mavazi meupe, nikapepesa macho vizuri
ili niweze kumuona, sikuamini macho yangu baada ya kuibaini sura yake, alikuwa
Minza binti mfalme kutoka nchi yangu ya Vumu, sikuweza kujizuia niliachia
kicheko cha furaha.
itaendelea Jumapili...