Jinsi ya kujibu maswali ya kiswahili katika mtihani wa taifa - swali la 15
Wakati naandika makala hii, muundo wa mtihani wa Kiswahili ulikuwa bado haujabadilika. Hivi sasa kuanzia mwaka 2019, muundo unaotumika ni tofauti. Hata hivyo, makala hii pamoja na kutofautiana na muundo wa mtihani, bado ina mashiko! Isome. "Mwalimu Makoba."
Utangulizi
Kwa mfumo wa
utungaji wa mitihani ya kiswahili unaotumiwa kwa sasa-kabla ya mwaka 2019, swali la 15 ni la lazima
kujibiwa na mwanafunzi afanyaye mtihani wa kumaliza kidato cha nne. Mfumo huu
ulianza kutumika mwaka 2008 ukaachwa mwaka 2019. Swali la 15 lina alama 15, alama hizi ni nyingi
sana na zikikosekana zinaweza kuleta maafa makubwa katika matokeo ya
mwanafunzi.
Kwa bahati
mbaya wanafunzi wengi huliacha swali hili la lazima na kupoteza alama zote 15.
Wale wanaojikaza kisabuni kulifanya swali hili hukosa mbinu za jinsi ya kulijibu
na hujikuta wakishindwa kulitendea haki na kuambulia alama za simanzi. Wachache
hufaulu, pengine ni wale waliopata kusoma kijitabu hiki.
Kijitabu hiki
kinatoa maelezo ya kina juu ya jinsi ya kulijibu swali la 15, mbinu hizi
zitawawezesha wanafunzi kufaulu vyema mitihani yao. Pia mada zinazojadiliwa humu, zitaongeza ubunifu wa wanafunzi na kuwafanya waongeze maarifa yao ambayo ndiyo msingi wa kila kitu.
Mambo
yanayohusika katika swali la 15.
Swali hili huhusisha mambo matatu tu;
i.
Utungaji wa hadithi
ii.
Utungaji wa tamthiliya
iii.
Utungaji wa mashairi
Hivyo
mwanafunzi atatakiwa awe na mbinu za utungaji wa mambo hayo kwani kila mwaka
swali hubadilika, huenda mwaka huu ukaambiwa utunge tamthiliya na mwaka ujao
ukatakiwa kutunga shairi.
Mbinu za utungaji wa mashairi
Katika utungaji
wa mashairi, yakupasa kufahamu mambo manne muhimu.
i.
Namna ya kutunga utenzi
ii.
Namna ya kutunga mashairi ya
kimapokeo
iii.
Namna ya kutunga ngonjera
iv.
Namna ya kutunga majigambo
Namna ya kutunga utenzi
i.
Utenzi uwe na vina na mizani nane
ii.
Utenzi uwe na sifa ya tarbia. Tarbia
ni muundo wenye mistari minne katika shairi/utenzi
Sasa hebu
tazama mfano huu uliojibiwa kutoka swali la necta 2008.
Swali
“Tenzi zina kanuni maalumu”. Tunga utenzi wenye beti tatu
(3) unaohusu ugonjwa wa UKIMWI.
Jibu
UGONJWA WA UKIMWI
UKIMWI umevamia,
Jamii o inalia,
Wavuvi mabaharia,
Wote unawachukua.
Hii simanzi jamani,
Heri itupwe motoni,
Tutoke korokoroni,
Tupumue kwa amani.
Kujikinga ni rahisi,
Mwenzenu nimedadisi,
Fundisha yako nafsi,
Ngono haina nafasi.
Namna ya kutunga ngonjera
Ngonjera ni shairi lenye
wahusika wawili wanaojibizana. Kwa mfano; ubeti wa kwanza, mwalimu, na wa pili,
mwanafunzi.
Unapotunga
ngonjera zingatia haya;
i.
Wahusika wanaojibizana
ii.
Urari wa vina na mizani
iii.
Mwisho wahusika wakubaliane kuhusu
jambo moja
Swali la necta
la mwaka 2009 limejibiwa vyema kama mfano;
Swali
Umeteuliwa kushiriki katika shindano la uandishi wa ngonjera
la Afrika ya Mashariki. Tunga
ngonjera yenye beti nne (4) kuhusu maandalizi ya uchaguzi wa
mwaka 2010.
Jibu
MAANDALIZI YA UCHAGUZI MKUU 2010
Mzee
Uchaguzi umefika,
viongozi kuchagua,
Hakuna kubabaika, kama moto wa mabua,
Rushwa hiyo kwangu taka, busara kuibagua,
Mzee ama kijana, lazima kupiga kura.
Kijana
Wala Sitapiga
kura, kupoteza muda wangu,
Chagua wauza sura, wasioona uchungu,
Kiona vyao vipara, ni vyeusi kama vyungu,
Nasema kura sipigi, uchaguzi ukifika.
Mzee
Kijana elewa
sasa, faida za kuchagua,
Tena si vyema kususa, taja angukia pua,
Na usitoe ruksa, serikali kuiua,
Mzee ama kijana, lazima kupiga kura.
Wote
Kushiriki
uchaguzi, ni bora si kulalama,
Hatuachi uchokozi, kwa uchaguzi salama,
Hakuna kumwaga chozi, kwako we baba na mama,
Mzee ama kijana, lazima kupiga kura.
Namna ya kutunga mashairi ya kimapokeo
Unapotunga mashairi ya kimapokeo
zingatia yafuatayo;
i.
Urari
wa vina na mizani
ii.
Lugha
ya mkato
Swali la necta mwaka 2010 linatumika kama mfano;
Swali
Tunga shairi la kimapokeo lenye beti nne (4) kuhusu
unyanyasaji wa kijinsia.
Jibu
UNYANYASAJI WA KIJINSIA
Kunazo jinsia
mbili, ya kike na ya kiume,
Zote hizi ninakili, zastahili falme,
Changamoto ya akili, hii jinsia ya kiume,
Kunyanyasa mwanamke, wote tuseme yatosha.
Yu shambani
analima, mume pombe ajinywea,
Yeye baba yeye mama, umri wazidi mwendea,
Kutwa yu kashika tama, kipigo kesha pokea,
Kunyanyasa mwanamke, wote tuseme yatosha.
Mumewe
anapokufa, mali anadhurumiwa,
Hachukui hata sofa, mwanamke aonewa,
Mwisho apata kifafa, na kukonda kama muwa,
Kunyanyasa mwanamke, wote tuseme yatosha.
Kalamu
nashusha chini, wanaume eleweni,
Dhambi mwajaza pomoni, mwanamke heshimuni,
Haki sawa zipambeni, zienee kooni,
Kunyanyasa mwanamke, wote tuseme yatosha.
Utungaji wa majigambo
Majigambo ni sanaa ya unenaji yenye utendaji na inayotumiwa na wasanii
kujigamba ama kujinaki na kutangaza sifa zao.
Tofauti iliyopo kati ya mashairi na majigambo ni kuwa, majigambo yapo kwa
ajili ya kujigamba tu kuhusu umahiri au ushujaa wa mtu wakati mashairi huweza
kuzungumzia mambo mbalimbali yahusuyo jamii. Vilevile majigambo si lazima yawe
na vina na mizani.
Mfano huu toka swali la necta 2012, unafafanua zaidi
Swali
Umeteuliwa
kuwa mmoja kati ya waandaaji wa shindano la sanaa za maonesho litakalofanyika
wakati wa kusherehekea siku ya walimu duniani mwaka 2013. Andika majigambo
yenye beti nne ya mhusika ambaye ni mwalimu.
HAKUNA KAMA MIMI
Mimi ni
mwalimu bora, dunia yote yajua,
Na nishikapo bakora, wanafunzi hutambaa,
Nafundisha lugha bora, kiswahili manufaa,
Jamani nasema hivi, hakuna alo ka mimi.
Mi ndo kubwa
la vibaka, nilombaka popobawa,
Mchawi we utachoka, mi tabibu bila dawa,
Nguo iso na viraka, ninatinga kama kawa,
Mwalimu mwalimu kweli, ukinigusa tanata.
Nilimfundisha
Mudi, leo hii ni profesa,
Pia mwingine Daudi, mpaka kawa na pesa,
Kazi yangu maridadi, naoa bila ya posa,
Jamani nasema hivi, hakuna alo kama mimi.
Kalamu naweka
chini, tabasamu li usoni,
Nimenena ya moyoni, yalotoka akilini,
Katu sikai shimoni, mwalimu kazi kazini,
Mwalimu mwalimu kweli, ukinigusa tanata.
Utungaji wa hadithi fupi
Katika utungaji wa hadithi fupi, vipera vingi vya hadithi
huhusika, vipera hivyo ni kama, soga, ngano, vigano, tarihi, visasili, visakale
n.k. hivyo ni vyema kuvijua vipera hivyo. Hata hivyo katika utungaji wa hadithi
kanuni zake ni zilezile hata kama unatunga katika kipera tofauti.
Mambo yafuatayo ni sharti yazingatiwe
katika utungaji wa hadithi fupi
- Hadithi
fupi inakuwa na mhusika mkuu mmoja ambaye anajitokeza sana kuliko wahusika
wengine.
- Wahusika
wachache.
- Mandhari
finyu.
- Hadithi
fupi inakuwa inaongelea dhamira kuu moja tu ambayo inaonekana toka mwanzo
hadi mwisho wa hadithi.
Mfano huu unafafanua zaidi;
Swali
Tunga hadithi fupi kuhusu kisa chochote cha kusisimua.
PURUKUSHANI USIKU WA MANANE
Ilikuwa usiku wa siku ya Jumatano, Mowasha alijilaza katika
kitanda chake cha teremka tukaze kwa furaha kuu. Ajabu ni kwamba hakukumbuka
hata kuvua viatu, alilala navyo!
Kilichompa furaha Mowasha hakikuwa kitu kingine bali fedha
aliyoipata baada ya kuuza pamba yake, pamba aliyohangaika kuilima leo ilimpa
mamilioni, kweli mchumia juani hulia kivulini.
Akiwa amelala tena hajitambui kwa sababu ya usingizi, ghafla
alistushwa kwa kupigwa kofi zito la mgongo, kofi hilo lilimpa simanzi na
kumfanya alie kwa maumivu.
“Toa fedha uishi.” Jambazi mmoja alimwamulisha Mowasha,
Mowasha akamtazama bwana huyu usoni akagundua ya kuwa jambazi huyu alikuwa
mweusi kama kipande cha giza!
Jambazi yule aliendelea kumchapa makofi mazito ya uso
Mowasha, kuna wakati jambazi alisikika akisema, “Toa fedha niko kazini!”
Mowasha baada ya kuona anaweza kufa, akainama chini ya
mvungu wa kitanda chake akatoa kitita kikubwa cha fedha, jambazi bila kupewa
fedha zile akazikwapua na kutokomea kusikojulikana.
Mowasha alihuzunika sana baada ya kuibwa fedha zake,
alionekana mnyonge kama mtoto wa panya aliyekutana na paka mkubwa, lakini
hakukata tamaa, aliendelea na shughuli za kilimo, safari hii hakulima pamba
peke yake, alilima machungwa, nyanya na matikiti. Hivi sasa anamiliki nyumba
mbili za ghorofa.
Kwa kuzingatia kanuni zilizotolewa hapo
juu, hebu jipime kwa kufanya swali hili la necta mwaka 2011.
Eleza muundo wa soga. Tunga soga ya kusisimua kuhusu kisa
cha kubuni.
Utungaji wa tamthiliya
Mambo ya kuzingatia katika utungaji wa tamthiliya
Katika utunzi wa tamthiliya kuna mambo kadhaa ya kuzingatia,
mambo hayo ni kama yafuatayo:
- Chagua
jambo unalotaka kuandikia
- Panga
namna msuko wa visa na matukioa utakavyokuwa
- Buni
wahusika wako kulingana na kile unachotaka kukiandika
- Chagua
mandhari yanayofaa kulingana na visa vyako
- Tumia
mtindo wa majibizano kati ya wahusika
- Gawa
tamthiliya katika maonyesho
- Weka
maelekezo ya jukwaa. Haya huelezea kile kinachotendeka kwa wakati ule.
Maelezo ya jukwaa huwa katika maandishi ya italiki.
Tazama mfano wa tamthiliya hii ambayo imezingatia vigezo
vyote vya utunzi wa tamthiliya.
Swali
Tunga tamthiliya fupi kuhusu kisa chochote kinachothibitisha
kuwa mwanamke si mnyonge.
Jibu
VITUMBUA VITAMU
ONYESHO LA KWANZA
(Jukwaani wanatokea Kipisi na Mwantumu,
Kipisi anatembea haraka na kumkamata mkono Mwantumu)
Kipisi: Habari yako sista…
Mwantumu: salama karibu biashara. (Anashusha chini sufuria lililojaa vitumbua, Kipisi anachukua vitumbua
viwili na kuanza kutafuna)
Kipisi: Asante sista, nimetafuna viwili, vitumbua vitamu
sana. Kwa heri!!
Mwantumu: Kwa heri hiyo vepee? Nilipe fyeza yangu, shilingi
mia mbili.
Kipisi: sikulipi, fanya unachoweza.
Mwantumu: ahaa… kwa kuwa mi mwanamke ndo unanichukulia poa
sio? Sasa leo nitakuonesha utamu wa mihogo pilipili.
(Mwantumu anamkunja shati Kipisi, kisha
anampiga mweleka na kumfanya kipisi adondoke chini kama gogo.)
Kipisi: we mwanamke nuksi, chukua pesa yako usije niua bure.
Zingatia kuwa swali liulizwapo, huelezea urefu unaotakiwa
katika hiyo tamthiliya yako.
Sasa hebu jipime kwa kufanya swali hili la necta mwaka 2014
Tunga tamthiliya fupi kuhusu umuhimu wa elimu kwa vijana wa
Tanzania ya leo. Tamthiliya hiyo isipungue maneno mia tatu (300).
TAMATI
Marejeo
Mitihani ya necta taifa somo la
Kiswahili mwaka 2008 – 2015