SAFARI YA KUUSAKA MWEZI (sehemu ya tatu)
Minza alitusalimu, kisha akakaa pembeni, sikutaka
kupoteza Muda niliingia ndani ya Mapandagila 214, tayari kwa safari ya kuusaka mwezi.
Nilikaa ndani ya Mapandagila 214, nikaiwasha,
ikaunguruma kama simba, nilitaka kuwaonesha kuwa mimi ni mtaalamu wa kuendesha
Mapandagila ndani na nje ya nchi ya Lahaja. Taratibu nikairusha hewani,
niliizungusha polepole katika uwanja ule wa nyumba ya mfalme, nikakunja kona na
kuirusharusha kama mpira, halafu nikaitembeza kwa mwendo wa konakona mithili ya
kiluwiluwi ndani ya maji, hapo nikaona mfalme na watu wake wakinipigia makofi.
Sikutaka kulewa sifa, nikapiga gia kubwa, Mapandagila ikapaa juu, hapo nikatuma
taarifa makao makuu,
“Mapandagila
inatembea mwendo wa sauti tisa za kunguru dume!”
Chombo kilikimbia kwa mwendo wa kasi mpaka kikaitoka
Dunia. Nikasikia katika mtambo wangu wa mawasiliano watu wa makao makuu wakinipongeza
kwa hatua hiyo. Nikatabasamu kwa ushindi mdogo nilioupata.
Lakini ghafla, nililiona jeshi la vichawi vya anga
likinifuata kwa kasi,
“Makao
makuu jeshi la vichawi vya anga linanishambulia.” Nilituma taarifa.
“Ongeza
kasi, kimbia mwendo wa sauti 18 za kunguru dume.”
Niliongeza kasi kama nilivyoamuliwa, kwa mbali
nikaliona kombora lililotumwa na vichawi vya anga, nikalikwepa, likarushwa
kombora jingine, nikakwepa. Chombo changu kilijaa makombora mengi, lakini
sikutaka kuyatumia kwani ilikwishaamuliwa kuwa zama za uadui zilikwishapita na
mauaji hayakuwa na nafasi tena.
Vichawi vya anga vilikuwa vingi kama nyuki,
viliendelea kunishambulia kwa makombora mazito nami niliendelea kuyakwepa
makombora hayo, mpaka nilipokuja kupigwa kombora moja ambalo lilifanya
mawasiliano yakatike, chombo kikayumba, nikashindwa kukiongoza kikanipeleka
kule nisikotaka.
Chombo changu – Mapandagila 214 baada ya masaa saba ya
kupoteza mwelekeo kilidondoka katika ardhi nisiyoifahamu, kikasababisha mshindo
mkuu! Nikiwa nina hofu na nchi hii mpya niliamua kuimba wimbo wa kishujaa ili
kupunguza wasiwasi.
“Shujaa,
kokote natua,
Mojaa,
namba naijua,
Nitapambana,
mpaka ushindi” niliimba wimbo huu mpaka niliposikia sauti ya mtu ikinitaka
nitoke ndani ya Mapandagila 214. Nilifungua mlango nikatoka nikiwa na hamu ya
kumuona kiumbe aliyegundua uwepo wangu.
Nilishtuka nilipomuona, alikuwa mrefu azipataye futi
sita lakini hakuwa mtu wa kawaida, bali lilikuwa jitu la ajabu, tena jitu la
chuma! Sikuwahi kumuona mtu aliyetengenezwa kwa chuma, nilishangaa sana, lakini
kumbe wakati naendelea kumshangaa, naye alikuwa akinishangaa, hakuwahi kumuona
mtu aliyetengenezwa kwa nyama!
“We
ni nani na umetoka wapi?” Aliniuliza kwa upole.
“Nimetoka
sayari inayoitwa Dunia, naelekea sayari iitwayo Vumu, huko nakwenda kuutafuta
mwezi wetu ulioibwa na watu waishio huko.”
“Chombo
chako kimeharibika, hutaweza tena kupaa, twende ukapumzike mpaka pale
kitakapotengenezwa.”
Nilikubaliana naye, akainyanyanyua Mapandagila 214 na
kuibeba kama mtu mzima abebavyo ndoo ya maji, nilistaajabu sana nguvu za jitu
hili la chuma.
Tukiwa njiani kuelekea
katika mji wa jitu hili, nilijitahidi kuuliza maswali.
Itaendelea jumapili...