Wanasiasa Wanahama Mchana Kweupe, Hata Aibu Hawaoni| Makala za Mwalimu

Wanasiasa Wanahama Mchana Kweupe, Hata Aibu Hawaoni
Ni ujinga kama tutafurahia kufa kwa upinzani! Nchi isiyo na watu wenye mawazo tofauti, inasikitisha na kutia simanzi! Ole wetu Watanzania.
Kipindi hiki kimekuwa na purukushani za wanasiasa kuvihama vyama vyao kwa wingi zaidi kuliko katika kipindi chochote ambacho nimekuwa nikizifuatilia siasa za Tanzania. Katika hama hama hii, wengi wanadai yale waliyokuwa wanayataka yafanywe, sasa yanafanywa na Chama Tawala hivyo hawana sababu ya kuendelea kuwa wapinzani. Hoja hii ni dhaifu na ina walakini. Kwani uhai wa upinzani upo pale tu chama tawala kinapofanya madudu? Kama hali ni hii, basi hatujui maana na lengo la vyama vingi.
Hata hivyo, ukweli huwa haujifichi. Sababu moja katika nyingi inayowafanya wanasiasa hawa wahame kutoka huku kwenda kule (chama tawala kwenda upinzani na upinzani kwenda chama tawala) ni ‘maslahi binafsi’. Hapa kuna makundi mawili yanaibuka:
Kundi la kwanza ni lile la wanasiasa wasio na kitu. Hawa hawana mali. Ni masikini ambao wameamua iwe iwavyo lazima watumie umaarufu wao wa kisiasa kujitengenezea kipato ili kupambana na ugumu wa maisha. Hawa wako wengi kuliko aina nyingine yoyote ile.
Kundi la pili ni la wanasiasa wenye kitu. Hawa wana mali nyingi sana. Ni matajiri wanaonesa katika mabembea! Kinachowasumbua hawa ni hofu tu. hofu ya kushuka, hofu ya kufilisika. Hawana amani kuwa katika vyama vyao, suluhisho la kulinda mali ni kusarenda na kusema, ‘tumerudi bwana mkubwa! Tusamehe sana!
Wote hawa si wazuri kuwakabidhi madaraka. Watu wasio na misimamo ni hatari kwa afya ya taifa. Ni watu wanaovutwa na upepo wa fedha, hawana uwezo wa kutafakari sentimita chache mbele ya matumbo yao laini. Wanaisaka shibe, na bila shaka wameipata.
Ugumu wa maisha umetengeneza wimbi kubwa la wanasiasa wasio na upande maalumu. Hawa ni watu ambao wanatumia nguvu kubwa kujifanya wakosoaji wa mambo katika nchi ili waonekane. Wakiisha kuonekana, wanaweka dau mezani wanunuliwe! Inachosha.

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne