Sitasahau Nilipolala na Mwanamke Juu ya Kaburi (27)| Riwaya

Sitasahau Nilipolala na Mwanamke Juu ya Kaburi (27)| Riwaya

Nilishtuka nikaamka. Shingo iliuma lakini nilijikaza. Nilikuwa mahali nisipopafahamu, nazo fahamu zikazidi kunirejea taratibu hata nikagundua palikuwa pangoni.
“Umetumwa kuja kuniokoa! Lakini nimekudondosha kwa kofi moja tu.” Mtoto alizungumza, bila shaka ni Chimota.
“Sijabobea katika ulozi!” nilijibu.
“Nani kabobea?”
“Wewe, inasemekana ulizaliwa nao.”
“Ulishuhudia wakati nazaliwa?”
“Hapana. Niliambiwa tu.”
“Ujinga ni kukubali kila unachoambiwa!” alinijibu. Nikakaa kimya.
Nilizungumza na Chimota mpaka tukazoeana. Nilipomuuliza aliwezaje kuishi pangoni badala ya kuishi katika falme ya Matumbawe, alinijibu kuwa, aliutoroka utawala huo baada ya kugundua walitaka kumtumia katika mambo ya kunyanyasa watu wengine. Pia aligundua siri kuwa, yeye hakuwa mzaliwa wa Matumbawe, bali aliibwa kichawi na kufikishwa huko. Alipogundua nguvu zake za ziada, hakusita kukimbia. Hata hivyo, hakujua hasa ni kwa namna gani angerudi tena nyumbani, ujio wangu mahali pale ulimpa faraja na matumaini makubwa.
Sikutaka kuuliza aliwezaje kunitambua, jibu nilikuwa nalo. Yote yalisababishwa na ulozi. Baada ya muda nilimwona akiwa amelala, nikalala pembeni yake.
Ilikuwa asubuhi tulivu iliyonikuta nikiwa ndani ya pango kama nungunungu. Ajabu ni kwamba, ndege hawakuimba. Palikuwa kimya hata pakaogofya. Mwenyeji wangu hakuwako! Nilishtuka nikatoka ndani haraka. Nilimkuta akiwa nje. Kakaa chini anasoma kitabu nisichokifahamu.
“Chimota,” niliita.
“Mimi hapa,” aliitika.
“Nashukuru nimekupata, naomba tuondoke muda huu tuanze safari ya kurejea nyumbani. Nitajitahidi kubahatisha njia. Hatuwezi kupotea, Samike atasaidia.”
Chimota alinitazama kwa udadisi kisha akaachia tabasamu jembamba. Alionekana kuafiki maneno yangu. Niliinama kumwondoa mdudu mdogo aliyekwama katika mguu wangu wa kulia. Nilipoinuka sikumwona Chimota! Niligeuka nyuma tayari kuanza kumtafuta. Sikuamini nilichokiona!
Askari niliowakimbia msituni wakiongozwa na yule mtu wa kitengo cha kunusa walizikamata vyema silaha zao za jadi. Walikuwa wengi kiasi cha kushindwa kuwaza chochote. Nilipatikana mzima mzima na ujanja wangu wote sasa ulibaki mfukoni.
Nilifungwa kamba ngumu mikononi kisha nikaamrishwa nitembee mbele. Nilitii maagizo nikaongoza njia hata nikafanana na mtumwa anayepelekwa uhamishoni wa kosa la kukataa amri ya bwana wake.
Tulitembea mpaka tulipofika katika lango la kuingilia mjini. Bila shaka lilikuwa lango la kuingia ndani ya utawala wa nchi ya Matumbwe. Tulipoingia, watu walipanga mistari pembezoni mwa njia na wote walinizomea kwa hasira.
Kila nilipokuwa napita, yule askari mwenye pua kubwa aliwaambia watu kuwa, mimi ndiye chanzo cha mvua kutonyesha. Wengi walikasirika, baadhi yao wakanirushia mawe. Hata hivyo, hayakunipata.
Niliendelea kutembea pembezoni mwa umati mkubwa wa watu huku nikizushiwa kashifa mbalimbali zisizothibitika kisayansi. Mwisho niliingizwa katika kasri la mfalme. Nikiwa humo, nilipelekwa mpaka katika chumba kikubwa kilichokuwa bora sana. Kwa jinsi nilivyotekwa, nilistaajabu kuingizwa katika chumba safi kama kile. Kilikuwa kikubwa, pembezoni paliwekwa kitanda murua na godoro, viti vinne vilivyopakwa dhahabu viliizunguka meza ndogo iliyong’aa. Niliona mlango mmoja pembezoni mwa chumba, humo palijengwa bafu la kifahari! Nilifikiri labda watakuwa wamekosea kuniweka mule na punde wangekuja kuniondoa na kunipeleka chumba cha mateso nilichostahili.
Itaendelea Jumanne…
“Si ruhusa kuchukua hadithi hii na kuiweka katika mfumo wa sauti, kutoa kitabu, kuweka katika blogu au ‘website’ nyingine, au kufanya chochote kile bila kuwasiliana na mmiliki! Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka!”

Daud Makoba 0754 89 53 21

Tazama Vichekesho Vinavyotamba Katika Mtandao wa WhatsApp 

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Vichekesho vya Kuchekesha na Kuvunja Mbavu 1