Roma na Stamina Katika Upumbavu wa Kimkakati| Makala za Mwalimu
Upumbavu wa kimkakati, ni kutumia busara ulizonazo kuupandisha juu
upumbavu, ukasikika na kusifiwa kila pahala na kila mtu isipokuwa sisi!
Msanii yeyote atakaye kuifanya kazi yake kwa misingi na weledi, hana
budi kuwa na falsafa moja inayoeleweka. Roma alianza akiwa na falsafa moja tu,
kulisema tabaka lisilopenda kusemwa. Hata hivyo, mwishoni alianza kubadilika na
nilishangaa lakini niliamini niliposikia wimbo wake uitwao ‘k’ ajabu ya mwaka ule!
Baada ya kutekwa, mambo yamebadilika zaidi! Naona sasa ule msemo wake wa
“nawaachaje wanaobaki” unafanya kazi kwa kasi.
Akishirikiana na msanii mwenzake-Stamina, ametoa wimbo uitwao
‘Kiba_100’. Wakati lengo la Muziki likiwa kuburudisha, kuelimisha na kuonya,
wimbo huu unalengo la peke yake! Kusambaza matusi kwa njia ya kificho.
UPUMBAVU!
Ni aibu kusikiliza wimbo huu ukiwa na watu wanaokuzidi umri. Ni aibu
pia, kuusikiliza pembezoni mwa watu mnaoheshimiana sana. Na itaendelea kuwa
aibu kuusikiliza katika kundi la watoto wadogo! Kama ilivyo kwa ujinga kuvuma
kwa kasi, wimbo huu unasikika kila kona bila kujali uchafuzi wake wa hali ya
hewa.
Sijui wazazi na ndugu za mke wa Roma wanajisikiaje wanaposikia wimbo
huu. Kwa kuwa muziki ni hisia, mara nyingi wanamuziki huimba yale wayafanyayo
katika maisha yao halisi. Huenda kilichoimbwa ni mwigo wa maisha ya vijana
hawa! Kama ni kweli, basi dunia ingali ukingoni na inakwenda kasi.
Miongoni mwa maneno ya hovyo, yaliyofichwa katika kile kiitwacho tafsida
ni: usisite kunipa jicho, walishika fimbo na kuipakapaka mate, chumvini
nitazama sana, zidisha utundu ninyonye mpaka…, nipe nichane nyuzi… na mengine
mengi!
Swali muhimu zaidi ni kwamba, ni lipi hasa lengo la wimbo huu?