Riwaya| Sitasahau Nilipolala na Mwanamke Juu ya Kaburi (25)


Haikuwa kama nilivyofikiri. Majoka yale hayakuniwinda mie, bali yaligombana yenyewe kwa visasi vya muda mrefu. Nilikaa chini sehemu ambayo isingekuwa rahisi kudondokewa na viumbe hivi hatari.
Majoka yalipigana yakaumizana vibaya. Yaliunguzana mbavu kwa ule uwezo wake wa kutema moto. Mwisho yote yalikuwa hoi, kwa pamoja yakadondoka kwa kishindo, “Puuuuh!”
Niliachana na mkasa ule nikaendelea na safari yangu. Sikumwona tena yule ndege. Nikabaki mpweke msituni.
Wakati nikiendelea kutembea, niliona kikapu kikiwa kimetundikwa juu ya mti. Nilisogea haraka mwenye shauku ya kujua kilichokuwa kikapuni. Nilifika nikasogeza mkono niweze kukigusa. Sikufanikiwa. Kumbe ulikuwa mtego, ulifyatuka ukanifunga kamba miguuni na kunining’iniza kichwa chini miguu juu. Mimi na kikapu wote tukaelea juu kwa juu.
Hali ya kuning’inizwa namna ile ilikera  na yalikuwa mateso makubwa. Nilikwisha choka kutembea, mkasa wa kuning’inizwa kama nyama buchani ulinikata maini. Nikachoka tena na tena!
Baada ya muda mrefu, nilisikia vishindo vikija niliponing’inia. Niliogopa kiasi. Hatimaye walinifikia watu ambao walivaa ngozi ambazo hata hivyo zilitumika kufunika sehemu nyeti pekee. Mwili mwingine ukaachwa upate raha na karaha ya jua.

Walionekana kuwa wawindaji mashuhuri katika msitu ule. Nao wakanisogelea, waliponiona, walinitazama kwa hasira. Nilitambua sababu ya hasira yao. Mtego waliotegemea kupata nyama, alinasa mwanadamu asiyeliwa! Niliwaharibia hesabu zao.
Mmoja wao alizungumza kwa hasira, “We nyau katika umbo la mtu! Ndiyo nini kunasa wakati mtego haukuhusu… jamii yetu inakufa njaa leo siku ya tatu hatujapata chakula kisha unaharibu mtego… umetumwa na Hissopo?”
Aliyezungumza alitaja jina jipya ambalo sikulifahamu. Nadhani watu hawa walikuwa na uhasama mkubwa sana na Hissopo. Nilitamani kujua lakini sikuwa na taarifa. Nikiendelea kushangaa, nilimwona yule mzungumzaji akizungumza na wenzake. Sikugundua mapema alichowaeleza.
Baadaye niliwaona wote wakitikisa vichwa vyao. Kumbe Mzungumzaji aliwashawishi wanile mimi ili kupunguza makali ya njaa ambayo punde ingeiteketeza jamii yao.
Basi nilibebwa mzobemzobe nikaanza kupelekwa nisipopajua. Walinipeleka huku wakiimba nyimbo zisizovutia hivyo haikuwa na maana kuzikumbuka.
Tulitembea mpaka tukafika katika kijiji kilichojengwa nyumba za nyasi. Lango la kuingilia kijijini lilikuwa wazi, lakini badala waingie, walikunja kona, tukaanza kutembea pembezoni mwa ukuta. Nilisimama kuona kilichokuwa ndani ya ukuta ule. Kilikuwa kijiji kizuri sana, lakini watu wake, walikonda vibaya. Niliweza kuhesabu mbavu za ajuza mmoja.
Niligundua kilichowasumbua watu hawa, njaa kali. Hata hivyo sikuwa tayari kugeuzwa kitoweo kuwaokoa.

“Wewe uliyenasa kwenye mtego usiokuhusu nisikilize kwa makini!” alisema Mzungumzaji, “sisi si watu wabaya, ila njaa imetufunza ukatili. Hatujakuingiza kijijini kwa sababu maalumu, jamii yetu haili watu. Hivyo ili watu wasikatae kula nyama yako, tumeamua kukuchinja pembezoni mwa ukuta wa kijiji. Tukuchune, kisha tuwapelekee nyama yako. Tazama jiwe lile mbele yako, utachinjwa pale!”
Itaendelea Jumapili…
Tunaomba radhi kwa simulizi hii kutoruka Jumapili hii kama ilivyokawaida. Tunajitahidi kuhakikisha jambo hili halijirudii tena.
“Si ruhusa kuchukua hadithi hii na kuiweka katika mfumo wa sauti, kutoa kitabu, kuweka katika blogu au ‘website’ nyingine, au kufanya chochote kile bila kuwasiliana na mmiliki! Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka!”

Daud Makoba 0754 89 53 21

TAZAMA POVU LA MWALIMU MAKOBA KWA WASANII WAVAA HOVYO...

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne