RIWAYA| SITASAHAU NILIPOLALA NA MWANAMKE JUU YA KABURI (21)

SITASAHAU NILIPOLALA NA MWANAMKE JUU YA KABURI (21)

Tulifika chumbani. Chumba kilihuzunika na hakikuvutia hata kidogo. Vitu havikukaa katika mpangilio. Nguo zilizagaa chini, nazo suruali zilitumbukia katika masufuria makubwa yaliyobaki mchuzi. Mlikuwa na vitanda viwili, kitanda kikubwa na kitanda kidogo.
“Kitanda hiki kidogo alilala mjukuu wangu Chimota… nilipenda alivyoota! Washenzi wakamchukua. Utalala hapo!”
“Hicho kikubwa alilala nani?” niliuliza swali la utani. Mzee akaujibu utani wangu.
“Nililala na bibi yako!”
Sikujibu. Alizima kibatari, nikalala katika kitanda kidogo, naye akapachika mbavu zake katika kitanda kikubwa.
Asubuhi ilifika. Niliamka taratibu kitandani. Nilipotazama alipolala mzee sikumwona. Kwa kuwa nililala na nguo zangu zote, nilifanya kazi ndogo ya kuvaa kandambili na kuelekea sebuleni. Huku nako hakuwako.
Nikiendelea kutafakari aliko mzee, niliona moshi ukifuka nje, nikaamua kwenda kushuhudia.



Nilimwona mzee akiwa katika mti mdogo wa mwarobaini. Chini aliwasha moto kwa kuni tisa na aliendelea na zoezi la kuchoma samaki. Bila shaka yalikuwa maandalizi ya kifungua kinywa.
Nilikaa pembeni yake. “Mzee Shikamoo!” nilimsalimia.
“Haina haja!” alijibu. Sikujali, nilikaa nikaendelea kumtazama alivyoshughulika na wale samaki.
Hatimaye samaki walikuwa tayari kwa kuliwa. Mzee akanituma chumvi. Nilileta. Akanituma tena pilipili, nikaleta, akanitaka nikae mkao wa kula, nami nikatii.
Samaki walipakwa chumvi na pilipili kiasi kwa ufundi wa hali ya juu, ukiongeza ile harufu yao na njaa niliyoihisi tumboni, nilizidi kukaa mkao wa kula kama nilivyoshauriwa. Mate yalinijaa mdomoni tele.
Mzee alianza kumshambulia samaki mmoja, akachomoa mnofu mkubwa, akatafuna taratibu akifaidi uhondo. Nami nikapeleka mkono katika samaki huyo ili nibebe pande langu la mnofu. Mzee kuona hivyo akausukuma mkono wangu na kunitaka nitulie.
Nilitii amri. Nikatulia ninayesubiri samaki. Mzee akamla samaki wa kwanza nikimshuhudia, akaongeza wa pili nikitazama, mate ya uchu yamenijaa mdomoni.
Alimaliza kula samaki wote wawili mimi nikitazama tu, akanituma maji. Nilikimbia nikayaleta haraka. Akanywa taratibu kisha akabeua kwa shibe. “Gbuuuuuuuh!”
Alinitazama kwa huruma, akasema: “Najua njaa ina kukeketa tumboni, nenda chumbani kwangu chini ya uvungu kuna kiazi kikubwa, chukua ule!”
Kwa jinsi njaa ilivyouma, nilikwenda haraka chumbani. Nikachungulia uvunguni kutafuta kiazi nilichoagizwa, sikuamini nilichokiona uvunguni…

Itaendelea kesho…



POVU LA MWALIMU MAKOBA KWA WASANII WAVAA HOVYO

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne