MAYASA UMENIPONZA, MALIPO NI HAPAHAPA DUNIANI!


Nimeumbuka mchana kweupe na kupata aibu ya kufunga mwaka kisa Mayasa huyu niliyemwamini. Kweli tenda wema uende zako ukingoja shukrani utagombana na walimwengu.
Mayasa mchepuko wangu ‘classic’ ambao siku zote nimekuwa nikiuhudumia kwa huduma zenye ubora wa aina yake kushinda hata ninavyomgharamia mke wangu wa ndoa. Sijaamini kabisa kama aibu hii ameisababisha yeye, nami nasema michepuko sasa basi! Hata hivyo sina uhakika kama nitadumu katika kauli hii.
Baada ya kupata kijilikizo cha wiki moja ofisini, nikaamua kukatumia nyumbani kwa mchepuko wangu Mayasa. Haikuwa kazi ngumu kumzuga ‘wife’, nikamwambia nimepata safari ya kiofisi nakwenda zangu Shinyanga kufuatilia ufunguzi wa tawi jipya. Mtoto wa wenyewe hana matatizo, akakubali kwa roho nyeupe kabisa.
Basi nikaondoka na kuelekea zangu kwa Baby Mayasa toto mahsusi! Mambo yalikuwa matamu sana. Ilikuwa raha ya aina yake kula, kunywa, kulala na kuamka nikiwa na mchepuko. Nafasi kama hizi ni adimu mno!
Siku zilikwenda salama kabisa tukila raha kama tuko fungate. Huku nyuma wife alikuwa anaulizia maendeleo yangu ya kiofisi safarini Shinyanga, nami nikamjibu yalikuwa safi na karibuni nitarejea nyumbani.

Basi baada ya siku saba za kuponda starehe na Mayasa, muda wa kurejea nyumbani ukawadia. Nikajizoa na kuelekea nyumbani kama niliyetoka safari ya mbali.
Ile nafika tu nikapokelewa kwa kofi kali lililonifanya nihoji, “Nimetoka safari ya mbali badala ya kunipokea mizigo unanikwaruwa kwa kofi zito namna hii?”
“Mjinga wewe…” wife alifoka. “Hukuwa safari yoyote, ulikwenda kwa malaya wako Gongo la Mboto.”
Mzozo ulikuwa mkali kwa sababu japo alichokisema kilikuwa ni kweli, lakini nilikataa. Ndipo akaamua kuukata mzizi wa fitna kwa kunionyesha meseji.
Nilishtuka, kumbe Mayasa alikuwa akimtumia picha zote nilizokuwa napiga naye wakati nipo kwake. Meseji moja ilisomeka, “Mumeo niko naye, kajileta mwenyewe… unalooo shutu!” chini yake ikafuatiwa na picha yangu niliyopiga nikiwa nimelala na mchepuko huu.

Ilikuwa aibu, nikabaki najiumauma tu, kumbe yote tuliyokuwa tunafanya, Mayasa alipiga picha na kumtumia wife. Sasa nimepata aibu na sina uhakika kama mke hataondoka nyumbani. Nabaki nikijilaumu. Hii yote sababu ya Mayasa, mchepuko usio na siri.






POVU LA MWALIMU MAKOBA KWA WASANII WAVAA HOVYO

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne