SAFARI YA KUUSAKA MWEZI (sehemu ya 12)
hawakukataa walitukumbatia kisha wakatutakia
kila la heri katika safari tuliyotaraji kuianza. Kabla hatujaondoka nilikifuata
kile kijitu ambacho kiliiba mwezi wetu na kuzungumza nacho maneno ya mwisho.
“Mwezi
wenu utakapozima, usiwaze kuja kuiba mwezi wetu, chukua kitabu hiki kinatoa
maelekezo ya jinsi ya kuuwasha mwezi uliozima.” Nilisema huku nikikikabidhi
nakala moja ya kitabu.
Mimi na Minza tulipanda Mapandagila,
nikamweleza Minza kuwa mimi ndiye ningekiendesha chombo kwa wakati huu ili nami
nipate uzoefu wa kuongoza chombo kilichosifika pande zote za Dunia.
Tulipaa mpaka ulipokuwa mwezi wetu, mwezi
ukaongeza tabasamu, Minza akachomoa kamba kubwa iliyokuwa na sumaku maalumu ya
kuunasia mwezi, mwezi ukanasa katika kamba, nasi tukapaa, sisi mbele, mwezi
nyuma tukiuvuta kama mkia. Furaha yetu haikuelezeka kwa wakati huo.
Baada ya masaa mengi ya kupaa angani, hatimaye
tulifika katika eneo ambalo vichawi vya anga viliwahi kunishambulia, mapigo
yangu ya moyo yakaanza kwenda mbio, Minza akanituliza na kunieleza kuwa
mapatano ya amani yalikwisha fanyika kati ya vichawi vya anga na nchi yetu.
Tena akaongeza kuwa nchi yetu haikuwa na adui hata mmoja. Nilifurahishwa na habari
hizo nikaichochea Mapandagila.
Tulifika Duniani saa mbili usiku, Dunia
ilitawaliwa na giza kali ambalo hata almasi isingeweza kuonekana. Lakini ghafla
kwa sababu ya ule mwezi tuliouvuta nyuma ya Mapandagila yetu, mwanga wa kutosha
uliimulika Dunia, nilichungulia chini, mamilioni ya watu walishangilia
kupatikana kwa mwezi. Masikini wengi wao walidhoofika kwa sababu ya madhara ya
kukaa bila mwezi, sasa tulirejesha matumaini.
Tulifika mahala unapokaa mwezi, Minza akaondoa
ile kamba iliyoufunga, ukabaki huru, safari hii haukuishia kutabasamu tu, mwezi
ulicheka na kila ulipocheka mwanga uliongezeka.
Tuliuacha mwezi na kutua chini ya ardhi yetu
tuipendayo, ardhi ya nyumbani, ardhi ya mababu zetu ambayo tuliithamini na
hatukuwa tayari kuishi kokote. Tulipokelewa kishujaa na watu wote, wenye vyeo
na wasiokuwa na vyeo. Nilimuona ndugu yangu Mowasha akishangilia kwa furaha,
lakini kwa bahati mbaya sikukumbuka kumletea zeze kutoka nchi ya vijitu kama
alivyoniagiza, nilipanga maneno mengine ya kumridhisha. Mfalme alikuwepo katika
mapokezi, alijivunia kuwa na taifa lenye watoto imara na wenye maarifa ya
kurejesha chochote kwa maslahi ya nchi yao.
Tulichukuliwa na kikosi maalumu kwa heshima
zote mpaka kwenye gari dogo la kifahari, safari ya kuelekea Ikulu ikaanza.
Kufumba na kufumbua tulifika ikulu, mimi nikapewa chumba changu, Minza binti
mfalme akaenda katika chumba chake cha siku zote. Wafanyakazi sabini na watano
walioajiliwa kuhudumu katika chumba changu walinitaka nilale kwa sababu ya
uchovu wa ile safari ya mafanikio ya kuusaka mwezi.
Nililala kwa furaha nikisubiri kukuche ili
mimi na Minza tufanyiwe sherehe kubwa ya kihistoria katika ardhi ya Lahaja.
MWISHO
Jumapili ijayo itaruka riwaya mpya ya kusisimua, MCHEZO WA JOGOO.
USIKOSE...