KISA CHA DEREVA WA GUTA KUZAMA KISIMANI


Guta ni baiskeli yenye mataili matatu, lakini Bwana Sakasaka hataki kabisa guta lake kuitwa baiskeli, yeye analiita SCANIA. Jana aliitwa na Mama Kidomo ambembee vyombo vyake kwa sababu alikuwa anahamia mtaa wa saba kwa kuchoka chokochoko za majirani.
Vyombo vyote vya ndani ikiwemo kabati, kitanda, na masofa vilienea katika guta! Basi Bwana Sakasaka akaingia barabarani na guta lake likiwa limejaa mzigo. Alipoikamata barabara kuu, alikutana na foleni kubwa akaamua kuivamia barabara ya waenda kwa miguu. Waenda kwa miguu walikuwa wengi, lakini hakujali, akalichochea guta lake likakolea mwendo kwelikweli. Hakuwa na kengele, alisikika akiwaonya waenda kwa miguu, “Tahadhari, SCANIA hii, ikikugonga hunyanyuki!”.
Basi akiendelea na mwendo. Mara  ghafla mbele yake, alitokea mtoto mdogo akikimbia, dereva wa guta akavuta breki lakini haikushika. Akakunja kona ya ghafla, ghuta hilo likatumbukia kisimani! “Chumbwiiiii.”

Kwa sasa tupo hapa tumemrushia kamba ili atoke, lakini akina mama wa mtaani wanalalamika. “Katuchafulia maji mshenzi huyu! Katuchafulia maji mshenzi huyu!”

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Sifa Bainifu za Irabu ya Kiswahili Sanifu