SAFARI YA KUUSAKA MWEZI (sehemu ya saba).






Nilikaa ndani ya chumba kile mpaka nilipopitiwa na usingizi, nikiwa usingizini niliota jinsi watu wa nchi yangu walivyokuwa wakiteseka, kabla ndoto haijaisha niliamshwa na binti waziri, mkononi akanipatia mikate miwili iliyotengenezwa kwa ufuta, nikagundua upembe ndio ulileta chakula hicho.

Nilikula mikate ile mpaka nikaimaliza, wakati nikiendelea kuusikilizia utamu wa mkate, binti waziri alinishika mkono kisha akasema nami taratibu.

            “Hakuna aliyewahi kukataa agizo la mfalme, kesho asubuhi utaondoka kwenda kuvichukua vitabu vya mafanikio… usiogope, utasindikizwa na askari kadhaa.”

            “Siwezi kwenda, watu wangu wanateseka.” Nilibisha, binti akatoka ndani na kuufunga mlango. Nikabaki katika chumba nikiwa mpweke.

Nikiwa ndani ya chumba kile, niliwaza mengi, kubwa zaidi nilifikiri namna ya kutoroka ili niendelee na safari yangu. Ulinzi ulikuwa mkali nilipata hofu kiasi.

Nilikitazama chumba chote, sikuweza kuona upenyo, kwa huzuni nikapitiwa usingizi. Nilistushwa usingizini na ukelele hafifu niliousikia… nilipotazama mbele kidogo niliona sakafu inanyanyuka juu, kisha akaibuka mwana mfalme, Chokusi. Kumbe ndani ya chumba kile palikuwapo handaki!

Chokusi alisogea karibu yangu akanikumbatia, nikafarijika kwani nilipata uhakika kuwa alikuja kunisaidia.

“Rafiki yangu umekula?” aliniuliza.

“Ndiyo.”

“Kesho asubuhi wanapanga kuondoka na wewe, wametumwa askari zaidi kutoka matawi yote waje wahakikishe kuwa hutoroki, nafasi pekee uliyonayo ni sasa. Ukichelewa kidogo tu, hutapata upenyo tena.”

“Nisaidie rafiki yangu…” niliomba kwa sauti ya unyonge.

“Nipo hapa kwa ajili hiyo… haya haraka tuingie katika shimo hili tutembee mpaka tutakapoibuka upande wa pili.”

Chokusi alitangulia, mimi nilifuata, tukazama ndani ya shimo kama nyoka, tukatembea kwa tahadhari kubwa ya kukamatwa na askari. Moyoni nilianza kupata furaha ya kuendelea na safari yangu.

Tulitembea kwa mwendo mrefu mpaka tulipoibuka mahali ambapo sikupafahamu, nilifurahi lakini nilikumbuka jambo moja nikaamua kuuliza.

            “Asante sana… lakini nadhani hapa ni mbali sana, na Mapandagila tumeiacha nyumbani.”


            “Mapandagila? Kile chombo chako cha kuelea angani?... Tazama pale mbele”

itaendelea jumapili...

Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika Risala | Kiswahili Kidato Cha Nne