Taaluma ya Semiotiki Katika Mazingira Halisi

Ua limeoteshwa katika taa
Eleza kwa mifano muafaka kutoka katika mazingira halisi juu ya taaluma ya semiotiki.

Semiotiki imefasiliwa na wataalamu mbalimbali, na hizi ni maana zilizotolewa na baadhi ya wataalamu hao. Kwa kuanza na mtaalamu Massamba (2004), yeye anasema kuwa, semiotiki ni taaluma ya kisayansi inayojishughulisha na uchunguzi na uchanganuzi wa mifumo ya ishara mbalimbali ikiwa inazingatia zaidi uhusiano baina ya kiwakilishi na kitajwa.

Pia mtaalamu Ferdinand de Saussure kama alivyonukuliwa na Morris (1971) amefasili semiotiki ni uhusiano kati ya alama na kitu, jambo au hali ya kitu inavyowakilishwa, akaendelea alama ni kiashiria na kitu ni kiashiriwa. Hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya kiashiria na kiashiriwa.

Charles (1934), alishughulikia dhana ya semiotiki kwa kuunda tanzu tatu ambazo ni sintaksia, Pragmatiki na semantiki.Sintaksia ni taaluma ya uhusiano kati ya ishara na vitu/ vielezo jinsi vinavyotumika, pragmatiki ni taaluma ya uhusiano kati ya mfumo wa ishara na mtumiaji wake na semantiki ni taaluma ya uhusiano kati ya maana na ishara. Hivyo basi semiotiki ni taaluma inayoshughulikia maana za ishara/ taswira.

Semiotiki hushughulikia neno kama kiwakilishi (utajo) cha kile kitajwa pia hushughulikia maana ya msingi. Hivyo semiotiki inaona maana inapatikana kupitia taswira. Yaani kila taswira lazima inakuwa na maana inayowakilisha. Kwa mfano rangi nyekundu duniani inaashiria upendo hivyo maana ya upendo iliyojitokeza imetokana na taswira ya rangi hiyo. Hivyo katika taaluma hii maana zote za maneno zimefumbatwa katika alama. Ni dhahiri kwamba ingawa semiotiki  na semantiki hushughukia maana, semiotiki kwa kiasi kikubwa hujihusisha na alama za kitaswira na vielezo kwa kiasi  kidogo wakati semantiki huchunguza maana katika mfumo wa ishara wa lugha inayozungumzwa na binadamu.
Mtaalamu Nazarova (1996), anafasili, semiotiki ni nadharia inayohusu mfumo wa alama katika mawasiliano ya lugha.

Kwa ujumla, semiotiki ni taaluma inayojishughulisha na uchunguzi wa ishara na alama pamoja na uhusiano kati ya alama na kitu husika.

Hivyo basi Semantiki inatofautiana na semiotiki kwani semantiki inashughulikia alama za lugha yaani kila lugha huwa na alama zinazoashiria kitu fulani wakati alama za semiotiki hazihusu lugha yaani huwa ni maana za mawasiliano, mfano ishara za mawingu, wanyama kama bundi ishara ya uchawi.

Taaluma ya semiotiki inaweza kuelezwa zaidi kwa kuangalia aina tatu za ishara;

Ishara za usababisho/ asili/ alama halisi. Hizi hueleza kufungamana kwa kiusababisho kati ya alama au ishara na kile kinachoashiriwa. Maana yake ni kwamba, jambo moja husababisha jambo la pili. Mfano, moshi – alama ya moto na mawingu ni alama ya mvua. Vilevile sura yenye makunyanzi huweza kuwa ishara ya mtu mwenye hasira. Kwani si kawaida kwa mtu mwenye furaha au anayecheka kuwa na makunyanzi usoni. Pia jogoo anapomkimbiza tetea ni ishara kwamba anataka kumpanda.

Mfano mwingine wa ishara za usababisho ni mbwa anapobweka sana mawindoni ni ishara kwamba kuna mnyama karibu. Pia nyayo (alama za miguu) ni ishara kwamba kuna mtu kapita, kama nyayo hizo zimefifia huashiria kwamba mtu huyo kapita muda mrefu na kama hazijafifia ni ishara kwamba mtu kapita muda mfupi. Vilevile mionekano ya sura ya mwanadamu ni ishara za usababisho wa hisia, mfano, mtu anapotoa machozi huashiria kuwa ana majonzi, japo kwa wakati mwingine huwa ni kiashiria cha furaha. Tumbo kubwa kupita kiasi kwa mwanamke ni ishara kwamba mwanamke huyo ni mjamzito. Sauti nene kwa mvulana ni ishara kuwa mvulana huyo amebalehe na sasa anaingia katika kundi la watu wazima. Vivyo hivyo, msichana anapokuwa na sauti nyembamba na nyororo huashiria kwamba, msichana huyo si mtoto tena na huenda amekwisha vunja ungo. Hivyo ishara za usababisho ni alama ambazo maana yake huwa ni ileile kwa yeyote anayetazama alama hiyo.

Ishara za ufananisho. Katika ishara hizi, huangaliwa kufanana kwa kipicha kati ya ishara na kinachoashiriwa. Kwa mfano picha ya mtu ke/me katika milango ya vyoo. Au mchoro wa kitu na kitu chenyewe. Mfano ramani ya nyumba ni ufananisho wa nyumba yenyewe, pia picha ya mtu ni ufananisho wa mtu fulani.

Mfano mwingine wa ishara za ufananisho ni ule unaoonesha picha ya sigara ikiwa imekatwa katikati, hii ni ishara ya ufananisho inayotoa amri juu ya zuio la uvutaji wa sigara katika eneo hilo.

Mfano mwingine wa ufananisho ni ule wa michoro ya barabarani, michoro hiyo au alama hizo za barabarani huweza kuwakilisha barabara finyu, kona kali, kituo cha mabasi na amri ya kusimama. Pia bendera huwakilisha chama, nchi, au alama ya kikundi fulani. Pia katika mahusiano rangi nyekundu huweza kuwakilisha ishara ya upendo. Mfano mwingine wa ufananisho ni picha ya injini ya kompyuta, pia alama V katika mkono wa mwanajeshi huonesha anacheo cha sajenti. Pamoja na mifano hiyo, kuna mifano mipya ambayo imeweza kuibuka katika zama hizi kama matokeo ya sayansi na teknolojia. Mfano katika mitandao ya kijamii, kama Instagram, Facebook, WatsApp, Telegram na mingine mingi, kumekuwa na matumizi ya picha ndogo (emoj) ambazo huambatana na maneno au kusimama peke yake. Picha hizi ndogo hubeba hisia fulani kwani zimebeba michoro ya vichwa vya watu, zipo zinazocheka na hutumiwa na mtu anayetaka kuonesha kwamba kafurahishwa na jambo fulani. Lakini pia zipo zinazolia, hizi huashiria kwamba mwandishi wa ujumbe ule hakuwa na furaha au mwenye huzuni. Mbali na hayo picha hizo, huweza kuonesha ramani za nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania. Hivyo hapana shaka mtumiaji wa mitandao hiyo ya kijamii anaweza akatumia picha hizo ndogo na akaeleweka hata bila kutumia maneno kabisa.

Ishara za unasibu. Katika ishara hizi hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya ishara na kitu kinachoashiriwa, lakini uelewekaji wake hutokana na mazoea tu. Hii ni kusema. Uhusiano huo ni wa kiada tu na wala haufuati kanuni yoyote. Alama hizo ni maneno ya lugha ambayo kimsingi yaweza kuandikwa au kutamkwa tu. Mfano jina la mtu, ieleweke kwamba ishara hizi zipo katika lugha kwa kiasi kikubwa ingawa katika ufananisho na usababisho zipo pia. Mfano mwingine wa ishara za unasibu ni neno kiti, neno hili halina uhusiano wa moja kwa moja na kiti halisi katika ulimwengu halisi. Mahusiano haya kati ya alama ya kiisimu, dhana, kitu halisi yaliwahi kuelezwa na wana isimu wa semantiki ambao ni Richard na Ogden (1968) kwa mchoro uliofahamika kama pembetatu ya maana kama hivi;
                                                                                         
D = dhana, A = alama ya kiisimu na K = kitu halisi
Mchoro huu unaonesha kuwa, kwa msitari usioungana na mistari mingine, kuna uhusiano nasibu zaidi kati ya alama ya kiisimu na kitu halisi. Aidha kuna uhusiano dhahiri zaidi kati ya alama ya kiisimu na dhana iliyoakilini halikadhalika na kitu katika ulimwengu halisi.
Hivyo basi semiotiki kwa jina lingine inajulikana kama semiolojia, ambayo inajihusisha na ishara pamoja na alama. Iliyotolewa maana na mmoja kati ya waasisi wa semiotiki, Ferdinand de Sassure. Japo neno semiotiki lilianza kutumika mnamo karne ya kumi na saba na mwana falsafa wa kiingereza John Locke. Lakini wazo la semiotiki kama somo lilitokea katika karne ya mwisho ya kumi na tisa na mwanzoni mwa karne ya ishirini kwa kazi huru ya Ferdnand de Sassure na mwanafalsafa wa kimarekani Charles Sanders. Kwa hakika, aina hizi tatu za ishara zinafanana na kuingiliana kwa kiasi fulani, hivyo umakini mkubwa unahitajika katika kuzielewa.

Marejeo;
Massamba P. B. D (2004) Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha. Dar es Salaam: TUKI.
Morris, Charles W. (1971), Writings on the general theory of signs, The Hague: Mouton.
Peirce, Charles S (1934), Collected papers: Volume V. Pragmatism and pragmaticism. Cambridge, MA, USA: Harvard University Press.
Leech, G. (1981) semantics. The meaning of meaning. (2nd Edn) Harmondsworth: Penguin Books.
Johansen, Jorgen Dines (1988). “The Distiction between Icon, Index, and Symbol in the study of Literature,” Semiotic Theory and Practice, Berlin: Walter de Gruyter.


Popular posts from this blog

Jinsi ya Kuandika Barua ya Maombi ya Kazi Mwaka 2024

Jinsi ya Kuandika CV | Mfano wa CV Wasifu

Uhakiki wa Riwaya ya Watoto wa Maman’tilie